Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Jerry William Silaa (17 total)

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma (PIC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021
MHE. JERRY W. SILAA – MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA UWEKEZAJI WA MITAJI YA UMMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue fursa hii kuwashukuru wote, tumepata wachangiaji 20 ambao wamechangia hoja zote mbili lakini katika hoja ya Kamati ya Bajeti wametaja mashirika ambayo na sisi tunasimamia kwa haraka haraka Mheshimiwa Dkt. Faustine Ndugulile, Mheshimiwa Christine Mnzava, Mheshimiwa Subira Mgalu, Mheshimiwa Hyuma, Mheshimiwa Esther Bulaya, Mheshimiwa Joseph Kandege, Mheshimiwa George Malima, Mheshimiwa Issa Mtemvu, Mheshimiwa Dkt. Oscar Kikoyo, Mheshimiwa ShallyRaymond, Mheshimiwa Hamida Mohamed Abdallah, Mheshimiwa Esther Matiko, Mheshimiwa Kwagilwa Reuben, Mheshimiwa Stansalaus Mabula, Mheshimiwa Luhanga Mpina, DKT. John Pallangyo, Mheshimiwa Ally Hassan King, Mheshimiwa Abbas Tarimba na Naibu Mawaziri wawili; Naibu wa Viwanda na Biashara - Mheshimiwa Kigahe na Naibu Waziri wa Fedha na Mipango - Mheshimiwa Chande. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na maoni na mapendekezo yaliyoko kwenye taarifa ya kamati naomba kama walivyosema wachangiaji wengi niseme mambo machache yafuatayo; niombe tuipongeze sana Serikali na tumpongeze kipekee Mheshimiwa Rais wetu Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa aliyoifanya ya kuweka mtaji mkubwa kwenye benki yetu ya kilimo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye taarifa yetu tumeelezea mwezi disemba Serikali imetoa zaidi ya shilingi bilioni 208 kama mtaji kwa benki hii na juzi tumeona ufaransa benki hii imesaini euro milioni 80 sawa na shililingi bilioni 210 tunaamini fedha hizi zitaenda kuleta tija kubwa kwenye sekta ya kilimo kupitia benki yetu ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru wewe binafsi kwa mwongozo wako kwenye kikao cha leo lakini nimshukuru sana Mheshimiwa Dkt. Tulia Acskon, Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, tumshukuru Katibu wetu ndugu Nenelwa Mwihambi, Mkurugenzi wa Idara ndugu Athumani Hussein, Kaimu Mkurugenzi msaidizi ndugu Bisile, makatibu wa kamati yetu wakiongozwa na Zainabu Mkamba, washauri wetu wa mambo ya sheria na wataalamu wengine kwa ushirikiano mzuri wanaotupa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kamati yetu inafanya kazi na Msajili wa Hazina ndugu Mgonya Benedict, tunamshukuru sana kwa kazi kubwa anayotusaidia na wataalamu wake ambao anafanya nao kazi, tuwataje ndugu Lightness Mauki, Mkurugenzi wekezaji wa umma, na Linus Kwakesigabo, Mhasibu Msaidizi wambao wamekuwa wakitusaidia sana kwenye kazi zetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, wachangiaji wengi wamezungumza mambo yale tuliyoyatoa kwenye maoni na mapendekezo itoshekusema tu maeneo yote mlioyataja ya APZA, NHIF, MSB, TARURA, NHC, TPA, kwenye maeneo ya TICTS
na kule kwenye uyejushaji wa mafuta, RUWASA, yote tutayafanyia kazi kwa mashirika yale tunayoyasimamia na tunaamini Msajili wa Hazina atatengeneza utaratibu mzuri wa kamati yetu kuweza kufanya kazi ya kusimamia uwekezaji wa mitaji ya umma na mashirika haya yaweze kuleta tija.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumesema kwenye taarifa yetu kwamba gawiwo la mashirika haya ni moja kati ya chanzo kikubwa cha mapato kwenye mfuko wa Taifa, Kamati yetu itaendelea kufanya kazi kwa moyo na uwadilifu wa hali ya juu katika kuishauri Serikali kuweza kuwezesha mashirika haya yaweze kufanya kazi vyema katika kuleta tija na ufanisi wa hali ya juu.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho siyo kwa umuhimu niwashukuru sana wajumbe wa kamati Makamu mwenyekiti, Mheshimiwa George Malima na wajumbe wote kwa ufinyu wa muda naomba majina yao yaliyokwenye kamati yaingie kwenye Kumbu kumbu za Bunge.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa kutoa hoja.

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, naafiki.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma Kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022, Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022
MHE. JERRY W. SILAA - MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA UWEKEZAJI WA MITAJI YA UMMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa kuja kuhitimisha hoja ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuchukua fursa hii kuwapongeza sana wachangiaji wote waliochangia hoja zote tatu mezani. Tumetambua wachangiaji 24 ambao waamechangia kwenye maeneo mbalimbali ya hoja hizi tatu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kamati hii ni mtambuka. Katika wachangiaji waliochangia zipo taaisi zimetajwa ambazo zinasimamiwa na Kamati ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma. Taasisi hizo ni Mamlaka ya Viwanja vya ndege (TAA), Mamlaka ya barabara kwa maana ya TANROADS, TANAPA, TAMESA, Mfuko wa Bima ya Afya (NHIF), Kiwanda cha Ngozi Kilimanjaro (KLICL), Mamlaka ya Bandari (TPA), Mamlaka ya Mapato (TRA) na Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA).

Mheshimiwa Naibu Spika, baadhi ya wachangiaji wamezungumzia suala la uhamishaji wa Mamlaka ya Ujenzi wa Viwanja vya Ndege toka TANROAD kwenda TAA. Naomba nilikumbushe Bunge lako Tukufu kwamba katika kikao chake cha tarehe 4 Novemba, 2022, katika Mkutano wake wa Tisa, Bunge lilikuwa na Azimio mbalo lilitokana na Mapendekezo ya Kamati yetu Na. 9, kwamba Serikali ihamishie Mamlaka ya Ujenzi wa Viwanja vya Ndege kutoka TANROAD Kwenda TAA.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikuthibitishie, kama alivyosema Naibu Waziri wa Ujenzi, tayari Serikali imeanza mchakato wa kuhamishia na wameleta utekelezaji wa azimio hili kwenye kamati na utekelezaji wake unaridhisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie kwa kifupi maeneo Matano. Eneo la kwanza ni Mfuko Maalum wa Uwekezaji (Investment Fund). Kamati imeleta pendekezo la kuiomba Serikali ianzishe mfuko huu ili kusaidia mashirika na taasisi yenye kuhitaji fedha za uwekezaji kuweza kupata fedha kwa urahisi.

Mheshimiwa Naibu Spika, maeneo haya, ipo Bodi ya Mazao Mchanganyiko (CPB) chini ya Wizara ya Kilimo. Bodi hii ikiwezeshwa fedha za kutosha ina uwezo wa kununua mazao, kwa maana ya mazao ya nafaka na inaweza ikasaidia huko mbele ya safari hata hili tatizo ambalo Waheshimiwa Wabunge leo wamesema la mfumuko wa bei.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tunaamini kama Bunge lako litapitisha azimio hili, basi Investment Fund hii itasaidia siyo tu taasisi za kiuwekezaji za biashara, bali hata taasisi kama CBP ambayo inaweza ikasaidia kwenye mifumuko ya bei ya chakula nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili ni eneo la Mifumo ya TEHAMA. Namshukuru sana Mheshimiwa Simbachawene, amemnukuu Mheshimiwa Rais katika kikao chake cha tarehe 28 Machi, 2021 akipokea Ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali. Hata hivyo, pale alipoishia kunukuu, yapo maneno ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan anasema, “kama mifumo imewashinda, basi ombeni misaada kwa wataalamu.” (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo hili la mifumo limesemwa hapa na Wabunge wengi, na maelezo yake ukitoa majibu yake hapa, hakuna anayeelewa. Ipo mifumo mingi ambayo haieleweki. Leo wafanyabiashara ikifika muda wanaweka return zao TRA, mfumo uko down. Yaani mtu anataka kulipa kodi, anaambiwa mfumo uko chini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumezungumzia Mamlaka ya Bandari (TPA). Pale TRA wana mfumo wao wa TANCIS wa kulipa custom duty; huku bandarini nao wana mfumo wao wa cargo system. Ukishalipa kodi, uende bandarini na wakati mwingine kodi mfumo uko chini. Ukienda bandarini wanaku- charge storage. Kule bandarini nako, ingawa wanaweza kuingia kwenye TANCIS na kwenyewe kuna matatizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ndiyo maana Mheshimiwa Rais anasema, siyo lazima kila jambo ujidai wewe Masoud Mwamba unaliweza. Kama limewashinda, tafuteni wataalamu waliobobea kwenye maeneo haya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mara nyingi tukizungumzia mifumo, tunatoa mifano. Sisi wote hapa tuna simu za mikononi, na wote hapa tukifanya miamala ya simu za mikononi, hakuna siku muamala unazidiwa, hakuna siku unatuma pesa ambayo hauna; hakuna siku unadhulumu muamala unaenda kushughulikia mahali unaambiwa jambo limeshindikana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mifumo ya kitaalamu ikijengwa vizuri; ndiyo maana Kamati inashauri Bunge kwamba uanzishwe mfumo wa single integrated information management system and network ambao utajumuisha mambo yote haya. Ukisikia mtu ana NIDA basi itambulike maeneo yote. Sio mtu wa Halmashauri hii anakopa, halafu anaenda Halmashauri nyingine; au unasikia kuna POS Halmashauri, mtu anaingiza anachokitaka yeye. Leo kuna Halmashauri fedha hazionekani, nyingine zinakusanywa haziendi Benki halafu unaambiwa huo ni mfumo. Hakuna mfumo wenye tabia kama hizo. Hicho ni kitu kingine, labda kitafutiwe jina lingine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaipongeza Serikali na Mheshimiwa Simbachawene kwa kauli hiyo aliyoisema ya Mheshimiwa Rais. Tunaiomba Serikali iende ikawe serious kwenye mifumo ili Watanzania hawa, watu wanaotumia bandari yetu waweze ku-clear mIzigo yao wakiwa Congo. Unaweza ku-trace mzigo kuanzia Congo mpaka unafika Bandari ya Dar es Salaam, lakini ukifika pale ni nenda rudi, mfumo uko chini, baadaye unachelewa kulipa kodi, ukilipa kodi, unakuwa charged kwenye storage, mwisho wa siku bandari inakosa wateja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la tatu ni la utalii. Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan amefanya kazi kubwa sana kwenye eneo hili. Filamu yake ya Royal Tour imeongeza watalii kwa kiasi kikubwa. Leo Ngorongoro mpaka kufikia Desemba wamekusanya zaidi ya shilingi bilioni 98. Leo TANAPA mpaka kufikia Januari 23, wamekuja kwenye Kamati wamekusanya shilingi bilioni 233. Tunategemea hawa kufikia mwezi Juni mwaka huu 2023 watakuwa wamevunja rekodi ya ukusanyaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nenda huko Ngorongoro, pita hiyo barabara, ukienda likizo Serengeti kupumzika na mkeo, zile rasta utakazopiga njia nzima mpaka ufike hotelini, hata hiyo sababu yenyewe ya kwenda kufanya na mkeo inaweza ikakushinda kwenye kufanya huko. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, Ngorongoro waliomba Shilingi bilioni 160 tu kujenga barabara inayoendana na mazingira, na walipata kibali UNESCO, mpaka leo hawajapewa fedha hizo. TANAPA walikuwa na hifadhi 16 zenye jumla ya Kilomita za mraba 57,000, wameongezewa hifadhi sita zenye jumla ya Kilomita za mraba 47,000, karibia mara mbili ya eneo lao. Fedha za maendeleo ni hizo hizo, fedha za matumizi ya kawaida ni hizo hizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukiendelea hivyo, alisema mchangiaji mmoja hapa, fedha za utalii ni Non-Tax Revenue. Ni pesa ambazo tunazipata kwa kile ambacho Mwenyezi Mungu alitujalia kama Rasilimali zetu. Tukiwekeza vizuri TANAPA, Ngorongoro na TAWA, tutapata mapato makubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hawa watalii 1,500,000 tunaozungumzia ni wale tu wenye kiu ya kwenda kuona The Eighth Wonder of the World, Serengeti. Akifika pale, zile rasta atakazopiga saa ya kwenda na kurudi, harudi tena. Kwa hiyo, tunaomba sana Bunge lako Tukufu lipitishe azimio na TANAPA itengewe fedha za kutosha.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile, ule utaratibu wa kukusanya fedha kupitia TRA siyo mbaya, lakini utengenezwe utaratibu mzuri wa Revenue Disbursement Automated System wa kurejesha fedha kwa wakati. Wanakusanya fedha nyingi, wanaomba pesa za maendeleo, mtu akae Hazina apeleke kwa muda anaotaka yeye. Kuhusu mifumo ameleezea vizuri sana kaka yangu Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba, kwamba wakati mwingine inakuwa na first track na mambo mengine mengi ya miradi mikubwa ambayo yanafanya fedha zisiende kwa wakati. Kwa hiyo, tunaliomba sana Bunge lako liazimie fedha ziende kwa wakati. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la nne, ni deni la Pamba. Tunaishukuru Serikali imeonesha jitihada kubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la tano na la mwisho, ni sheria ambazo zimepitwa na wakati, alisema Mheshimiwa Dkt. Kikoyo kuhusu Sheria ya TR, Sheria ya TBS, Sheria ya TRA ya Stamp Duty, tunaiomba Serikali iharakishe mchakato ilete sheria hizi kwa wakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Naomba kutoa hoja.

MHE. MARYAM AZAN MWINYI: Mheshimiwa Naibu Spika, naafiki.
Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii kuchangia hotuba ya Rais aliyoitoa Bungeni akifungua Bunge letu hili la Kumi na Mbili.

Kwanza na mimi kwa sababu ni mara ya kwanza, nitumie fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa fursa mimi kuwa mmoja wa Wabunge wa Bunge lako hili tukufu. (Makofi)

La pili, nikishukuru Chama changu cha Mapinduzi, chama ambacho nimekitumikia kwa zaidi ya nusu ya uhai wangu, kwa kunipa fursa, namshukuru sana Mwenyekiti, navishukuru vikao vya uteuzi na wanachama wenzangu.

Mheshimiwa Spika, naomba kuungana na wenzangu kuunga mkono hoja, lakini vilevile naomba sana kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa hotuba hii iliyobeba dira na maelekeo ya nchi yetu kwa miaka mitano. Hotuba hii ukiisoma na ile ya Bunge la Kumi na Moja, ukisoma utekelezaji wa Ilani, ukisoma machapisho mbalimbali ya taarifa ya uchumi, utaona jinsi gani Rais wetu amefanya kazi kubwa kwa miaka mitano, tunampongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, maeneo ya uchumi, uchumi wa nchi yetu umekua, Pato la Taifa limekuwa, mfumuko wa bei umekuwa uko katika hali nzuri, haujazidi asilimia 4.4, akiba ya fedha za kigeni kwa mara ya kwanza iko juu na inaendelea kuongezeka, thamani ya shilingi imeimarika sana, pongezi kubwa kwa Rais wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika huduma za jamii, kazi kubwa imefanyika, vituo vya afya, zahanati zimejengwa nchi nzima na tumeona kwenye hotuba hii tunayoijadili.

Mheshimiwa Spika, lakini labda kwa kifupi sana ni kuomba Bunge lako tukufu kwamba tuna kazi kubwa baada ya kumpongeza Rais kumsaidia ili malengo aliyoyaweka kwenye miaka hii mitano yatimie na katika kumsaidia wote tuna wajibu wa kumsaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wa kwanza ni wasaidizi wake, na bahati nzuri tunaye Waziri Mkuu mchapakazi, mpenda watu, anafikika na Waheshimiwa Wabunge mtakuwa ni mashahidi. Lakini wako wasaidizi wake wengine, watendaji wa Serikali nao wanafanya kazi nzuri, tumeanza vizuri. Sisi kule Dar es Salaam katika Jimbo langu la Ukonga, Mkurugenzi wetu Jumanne Shauri na watendaji wenzake wanatupa ushirikiano. Ingawa hatuwezi kuacaha kusema wako watendaji ambao inabidi wabadilike kuendana na kasi ya Rais wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, binafsi sina taabu na wewe na ninaamini Wabunge wenzangu hawana shida na wewe, tunafahamu kasi yako. Tumeona juzi hapa Mawaziri walivyokuwa wanajibu maswali ukisimamia Serikali kutoa majibu yanayoendana na shida za wananchi. Niwaombe Wabunge wenzangu, sisi tuna kazi kubwa ya kusaidia Mheshimiwa Rais kufikia malengo haya ya miaka mitano. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Wabunge hawa wamefanya kazi kubwa ya kampeni. Ukiingia hapa asubuhi Wabunge wengi wakiweka sura zao zile mashine zinakataa, siyo kwamba mashine ni mbovu ila sura walizokuja nazo hapa Novemba siyo sura walizonazo leo. (Makofi/Kicheko)

Tumefanya kazi kubwa, Waheshimiwa Wabunge wengine hapa wameosha vyombo, wengine wamepaka rangi kucha, tunayoyasema hapa ndiyo reflection ya matatizo ya wananchi wetu kule tunakotoka, tunaomba tusikilizwe na Waheshimiwa Wabunge, niwaombe tuseme, na wasiposikia tuwafokee. Tufoke kwa niaba ya wananchi tunaowawakilisha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi niliwahi kuwa mmoja wa watu tuliokuwa tunaishauri Serikali kuanzisha TARURA. TARURA imekuja kuondoa matatizo ya urasimu ule wa kihalmashauri wa ujenzi wa barabara, ilikuja kuleta tija kwenye utendaji wa kihandisi, lakini matokeo yake, tulianza vizuri na mameneja wa TARURA wa wilaya, akawa kuna coordinator wa mkoa, leo kumetengenezwa Meneja wa Mkoa, Mhandisi wa TARURA yule Meneja wa Wilaya amegeuka kuwa karani. Hana fedha, hatafuti zabuni, hamlipi mkandarasi, nimshukuru Mheshimiwa Jafo ameanza kulifanyia kazi. (Makofi)

Tulileta jambo lile…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Jerry Silaa.

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Spika, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitoe shukrani kwa kunipa nafasi kuchangia kwenye Mpango wa Serikali wa Miaka Mitano na wa mwaka mmoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niipongeze Serikali,k hotuba ya Waziri ameonesha kazi kubwa iliyofanyika kwa miaka mitano. Tunaipongeza sana Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisoma rasimu hii ya Mpango wa Miaka Mitano, naomba kuchangia kwenye Sura ya Tano; 5.4.10 ukurasa wa 102 kwenye miundombinu ya barabara. Kwenye miaka mitano iliyopita kazi kubwa sana imefanyika kwenye miundombinu ya barabara. Nchi nzima barabara zimejengwa, madaraja yamejengwa na sisi wa Dar es Salaam tumeona ujenzi mkubwa wa miundombinu kwenye Daraja la Mfugale, Ubungo interchange na interchange zingine zinaendelea kujengwa pale Chang’ombe na ujenzi unakaribia kuanza pale Morocco na maeneo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisoma Rasimu hii ya Mpango inaonesha jinsi gani Serikali imejipanga kwa miaka mitano hii inayokuja kukamilisha ujenzi wa barabara za lami lakini vilevile kuondoa msongamano wa magari katika majiji. Mimi naamini Waheshimiwa Wabunge watakubaliana na mimi kwamba unapoongelea mafanikio haya makubwa ya miudnombinu mikubwa ya barabara lazima uoanishe na barabara za ndani ambazo ndiyo zinamhudumia mwananchi katika maeneo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, unapozungumzia barabara hizi za mijini na vijijini, unaizungumzia TARURA. Naomba sana kuishauri Serikali kwamba lazima kwenye mpango huu kuwe na mipango inayotekelezeka ya kuisaidia TARURA iweze kutatua changamoto ya miundombinu kwenye maeneo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo wakazi wa Jimbo la Ukonga tunamshukuru Rais, ile foleni ya TAZARA pale haipo tena. Hata hivyo, leo wakazi wangu akiwemo Mheshimiwa Waitara, akishavuka TAZARA kutoka pale Banana kuitafuta Kivule ama Kitunda kuna kazi kubwa sana. Ukienda TARURA mfumo mbovu lakini na fedha hazitoshi. Leo Dkt. Ndumbaro na wakazi wenzake wa Majohe atavuka vizuri TAZARA lakini nyumbani hapafikiki. Simu zetu hizi ukiona simu yoyote inatoka maeneo hayo unaanza kuomba dua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kifupi yako mambo mawili ambayo Serikali ikijipanga vizuri itafikia malengo haya yaliyowekwa kwenye Rasimu ya Mpango. La kwanza, ni muundo wa TARURA. Tulianza vizuri, tulikuwa na Regional Coordinator na na Meneja wa Wilaya. Kazi ya Meneja wa Wilaya ilikuwa ni kutekeleza miradi ya barabara kule kwenye Wilaya na Majimbo yetu. Hata hivyo, mfumo umebadilika, tumemgeuza yule Regional Coordinator amekuwa Regional Manager na yule Manager wa Wilaya sasa hata ile kazi aliyokuwa anafanya ya kulipa wakandarasi wanaofanya kazi kwenye maeneo yake imehamishiwa mkoani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo kumpata mkandarasi wa kufanya kazi Nachingwea anatafutwa Lindi Mjini, mazingira haya ni tofauti sana. Huwezi ukampata mtu kufanya kazi Ngara kwa kumtafutia pale Bukoba Mjini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru Mheshimiwa Waziri ameliona hili kwenye ziara zake, ameahidi kuanza kulifanyia kazi na mimi naomba kuishauri Serikali. Ili Mpango huu uweze kutekelezeka lazima tuwe na muundo wa uhakika wa TARURA. Yule Meneja wa Wilaya awezeshwe, aweze kupata wakandarasi, fedha zifike, aweze kusimamia miradi yake na aepuke kuwa karani wa kutujibu sisi maswali yetu Waheshimiwa Wabunge ambayo hana utendaji wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakii la pili, ni fedha. Ipo dhana na naendelea kuliomba Bunge lako na Serikali ijenge dhana ya kusikiliza michango ya Wabunge kwa sababu Waheshimiwa Wabunge hawa wanayoyasema hapa siyo mawazo yao ni mawazo ya wananchi wanaowaongoza. Ipo dhana kwamba ukiongeza tozo ya barabara kwa mfano, leo Bunge likashauri kuongeza tozo ya barabara za mjini na vijijini kwenye mafuta, iko dhana kwamba gharama ya usafirishaji itaongeza. Leo kwa miundombinu isiyopitika kwenye maeneo yote ya pembezoni ya mijini na vijijini ya nchi yetu gharama za usafirishaji ziko juu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo mwananchi wa kule Majohe Bomba Mbili kuitafuta Mombasa analipa nauli Sh.700 mpaka Sh.1,000. Naamini barabara ya uhakika ingejengwa leo kungekuwa na daladala zinatoka kuanzia Bomba Mbili mpaka Kariakoo na gharama ya usafirishaji itashuka badala ya kuongezeka kwa kuongeza tozo kwenye mafuta. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Waziri anapokuja ku-wind up Mpango na wewe mwenyewe umesema kwamba Mpango huu ni Rasimu, basi mawazo haya tunayoyatoa yaweze kuchukuliwa kwa uzito na yahusishwe kwenye Mpango huu wa miaka mitano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, iko miradi ya TASAC, miradi ya DMDP Phase II, kule kwetu ni kizungumkuti, inasemekana imekwama kwenye maamuzi kwenye meza za watendaji wa Serikali lakini matatizo kule chini ni makubwa sana. Ni vyema tunavyotengeneza Mpango ukaongeza na kasi ya utendaji kwa watendaji wetu hasa kwenye miradi hii inayowagusa wananchi wa hali ya chini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, katika dhana hii hii ya kusikilizwa na leo wewe nikupongeze kwenye swali lile la Mheshimiwa Gambo asubuhi lazima Serikali ijifunze kusikiliza yale yanayosemwa na Waheshimiwa Wabunge. Ukiingia sasa hivi kwenye mitandao comments za wananchi wa Arusha wanaoathirika na utalii wanasikitishwa sana na majibu yale yaliyotolewa na Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nirudie kuiomba Serikali hii sikivu kwa sababu tunafahamu jinsi gani Rais wetu alivyokuwa msikivu, tunaona anavyotatua matatizo ya wananchi kule anakopita, tuombe na Mpango huu na wenyewe ujipange katika kutatua matatizo ya wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naskuhukuru sana, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kufungua dimba katika uchangiaji wa hotuba ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi. Naomba kuchukua fursa hii kwanza kumpongeza Waziri, Mheshimiwa William Vangimembe Mwalukuvi. Nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri, Dkt Angelina Mabula na wataalam wao wa Wizara. Nimpongeze pia Katibu Mkuu wa Wizara hii, dada yetu Mary Makondo, ambaye pamoja na sifa za kiutendaji lakini ana sifa ya unyenyekevu ambayo ni sifa muhimu sana kwa utendaji wa kazi za Serikali. Vile vile nimpongeze Naibu Katibu Mkuu Nico Mkapa na watendaji wote wa Wizara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitachangia kwenye maeneo matatu, eneo la kwanza ardhi ni rasilimali ambayo kama itapangwa na kutumika vizuri ina uwezo mkubwa wa kuwa chanzo kikubwa cha mapato kwenye Taifa letu. Utaona kwenye mwaka wa fedha uliopita Wizara ilikadiria kukusanya bilioni 200 na mpaka hivi tunavyozungumza zaidi ya shilingi bilioni 110 zimekusanywa kwenye halmashauri zote za nchi nzima, tunawapongeza sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala kubwa hapa ni fedha hizi zinavyokusanywa, uwekezaji wake unaorudi kwenye Wizara kuwekeza katika upimaji wa ardhi ni mdogo sana. Ukisoma bajeti ya mwaka wa fedha uliopita pamoja na fedha za nje, kwenye fedha za ndani Wizara ilitengewa shilingi bilioni 16 kwa ajili ya miradi ya maendeleo. Hata hivyo, mpaka Waziri anawasilisha hotuba yake ya bajeti ni shilingi bilioni tano tu ndiyo zimepelekwa kwenye Wizara kwa ajili ya miradi ya maendeleo sawa na asilimia 30.9.

Mheshimiwa Naibu Spika, wewe ni Mwalimu na moja kati ya wanafunzi wako umemtambulisha hapa asubuhi asilimia 30.9 kule shuleni ukiipata kwenye mtihani nadhani tutakubaliana supplementary. Ninachoomba kusema, lazima Serikali itenge fedha za kutosha kwenye Wizara hii ili Wizara iweze kutekeleza wajibu wake wa kupanga matumizi ya ardhi na kupima ardhi. Mpango huu na upimaji huu utakuja baadaye kuwa mapato makubwa kwa Serikali kwa mapato ya land rent. Kwenye Jiji la Dar es Salaam mpaka hivi tunavyozungumza tayari bilioni 5.6 zimekusanywa kati ya malengo ya bilioni, 11 ni kazi kubwa, lakini zitakusanywa zaidi kama maeneo mengi zaidi yatapimwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimwombe Mheshimiwa Waziri, mimi nilikuwa Meya pale Ilala kabla halijawa Jiji la Dar es Salaam. Nilikaa miaka mitano nakaimu Mkuu wa Idara Mipango Miji. Nimeondoka miaka mitano kuna Kaimu Mkuu wa Idara hivi nimerudi kwenye Ubunge bado kuna Kaimu Mkuu wa Idara. Nimwombe sana Mheshimiwa Waziri, hebu am-confirm mtendaji yule aweze kufanya kazi hizi akiwa tayari amethibitishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili ninalotaka kuchangia, ni eneo la urasimishaji. Kutokana na bajeti finyu na uwezo unaofanya Wizara iwe na uwezo mdogo wa kupima, Serikali mwaka 2015 ilianzisha zoezi la urasimishaji kwenye maeneo mengi ya mijini kwenye Mkoa wa Dar es Salaam, kwenye Jiji la Dar es Salaam, kwenye Jimbo la Ukonga inafanyika kazi ya urasimishaji. Pale Jimbo la Ukonga yako makampuni 24 kwenye mitaa 64 kwenye Kata zote 13 za Jimbo la Ukonga, kuanzia Kitunda, Mzinga, Kivule, Kipunguni, Ukonga, Gongolamboto, Pugu, Pugu Station, Buyuni, Zingiziwa, Chanika na mpaka Kata ya Msongola. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, zoezi hili linasuasua. Ukisikiliza hotuba ya Waziri ziko hatua wameanza kuzifanya. Nimpongeze Waziri, Waziri wetu wa Ardhi ni mtu mwepesi na anajituma sana katika kazi ya ardhi, maana kazi yenyewe hii haitaki sana kukaa ofisini. Tulipata tatizo pale Kata ya Kivule na upimaji wa kile Chuo cha Ardhi Morogoro nilimwambia Waziri na alifika kutatua tatizo lile.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile juzi Naibu Waziri amekwenda Chanika kutatua matatizo haya ya urasimishaji. Nimeona kwenye hotuba ya Waziri wanachukua hatua, lakini tukumbuke kampuni hizi zimechukua pesa za watu, hatua za kuzisimamisha, hatua ya kuzifungia upimaji, hazitasaidia Mtanzania aliyechanga fedha zake kwenye Jimbo la Ukonga na maeneo mengine kupata upimaji wa eneo lake. Nimwombe Mheshimiwa Waziri katika kuhitimisha aje atueleze nini mpango sasa wa kusimamia kampuni hizi ili Watanzania waweze kupimiwa ardhi zao, wapate hati milki, waweze kumiliki maeneo yao kwa mujibu wa sheria.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la tatu ninaloomba kuchangia ni migogoro ya ardhi; migogoro ya mipaka katika maeneo mbalimbali ya nchi yetu. Naomba nijikite kwenye eneo moja tu la migogoro ya mipaka baina ya hifadhi mbalimbali na vijiji na maeneo yetu tunayotoka. Kule Ukonga uko mgogoro wa kudumu baina ya Msitu wa Kazimzumbwi na wananchi wa Jimbo la Ukonga wa Kata za Buyuni, Chanika na Zingiziwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri, maana leo nilikuwa nimeshapanga kabisa jioni hapa, siyo kwa kuwa jana alisikia wachangiaji wachache angedhani bajeti ingepita kirahisi. Nilipanga leo jioni niwaombe Wabunge tushike shilingi kwenye eneo hili, lakini nimpongeze Waziri kwenye hotuba yake ameelezea vizuri sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, The Land Survey Act, Sura ya 324, inampa Mkurugenzi wa upimaji na Ramani mamlaka ya kusimamia upimaji na kutatua migogoro yote ya mipaka. Mheshimiwa Waziri kwenye ukurasa wa 68 ameeleza vizuri na kwenye ukurasa wa 69, naona amelimaliza tatizo hili na naomba nimnukuu Waziri anasema:

“Ni marufuku kwa Idara au Taasisi yenye migogoro kwenda yenyewe uwandani kutafsiri GN zao bila uwepo wa Mkurugenzi wa Upimaji na Ramani ambaye ndiye mhusika mkuu. Aidha Viongozi wa Mikoa, Wilaya lazima washirikishwe wakati wote mipaka inapohakikiwa”.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni marufuku kwa idara yoyote ama taasisi kwenda kunyanyasa wananchi na kujitafsiria GN zao wenyewe. Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt Ndumbaro marufuku, Mheshimiwa Naibu Waziri Mary Masanja marufuku, siyo maneno yangu, maneno ya Waziri mwenye dhamana ya ardhi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye maelezo yake Waziri ametoa wito kwa Viongozi wa Mikoa na Wilaya Wakuu wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya, maana wengine ni mabingwa kuweka watu ndani, sasa hawa ndiyo wa kuwaweka ndani, hawa wanaokuja kutafsiri GN zao wenyewe na migogoro ya mipaka na kunyanyasa wananchi wetu.

T A A R I F A

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Jerry Silaa, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Charles Mwijage

MHE. CHARLES J. MWIJAGE: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda nimpe taarifa mzungumzaji MCC mstaafu kwamba unapotoa taarifa, wale unaowapa taarifa hawapo, tatizo la maliasili hifadhi ndilo tatizo la mifugo ninalolipata kwangu kule, lakini unaowaambia hawapo hawawezi kuelewa unavyopata uchungu, hawapo hapa.

NAIBU SPIKA: Waheshimiwa Wabunge nimeshasisitiza mara kadhaa, Serikali ipo Bungeni na ndiyo maana mnazungumza na mimi, yaani kama kuna mtu yeyote wa Serikali ambaye jambo linamhusu limezungumzwa hajaelewa vizuri hata kama yupo humu ndani ataelezwa vizuri, ni jambo gani limezungumzwa kuhusu yeye. Kwa hiyo msiwe na wasiwasi na michango yenu mnayoitoa, Serikali iko Bungeni.

Mheshimiwa Jerry Silaa, malizia mchango wako.

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Mwijage, kaka yangu, mtaalam wa propaganda, sisi wataalam wa sheria hapa tuna address the chair, tunaongea na kiti na ujumbe utafika.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la mwisho ni eneo la uthamini. Niseme tu kwamba, Wizara ya Ardhi inafanya kazi yake ya uthamini vizuri sana chini ya Ofisi ya Mthamini Mkuu wa Serikali, mama yetu Evelyn Mugasha. Nafasi hizi zenye mambo ya hela hela ama za uadilifu uadilifu, wanapokaa akinamama wanazifanya vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninachoweza kusema ni kitu kimoja, naiomba Wizara ambayo ndiyo wataalam wa masuala haya, waishauri vizuri Serikali. Kulikuwa kuna wakati tunatumia sport valuation kuweza kupata bajeti ili idara ama taasisi inayotaka kufanyiwa uthamini iweze kutenga fedha, lakini tumeona mara nyingi uthamini unafanyika lakini kumbe hata hiyo taasisi inayoagiza uthamini hata fedha kwenye bajeti haijatengewa. Matokeo yake uthamini unafanyika, fidia zinachelewa na wananchi wetu wanapata shida sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, niiombe Serikali iweke utaratibu mzuri wa kufanya uthamini na kulipa wananchi kwa wakati. Ili hili lifanikiwe lazima wakati uthamini unafanyika tayari bajeti iwepo na fedha ziwe zimeshatengwa. Maeneo mengine wawe wanaaminiana, hawawezi wakafanya uthamini ukaidhinishwa, wakaanza uhakiki, ukakamilika, ukaja uhakiki mwingine wakati wananchi wanasubiri fidia zao, ile miezi sita ya kisheria inapita, hela za riba hazipo, tunaanza tena kurudi nyuma na wananchi wanapata shida kwenye maeneo yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho nirudie tena kuipongeza Wizara, inafanya kazi nzuri hasa katika kujikita kuingia kwenye mifumo ya TEHAMA. Tukienda hivi nchi yetu itapata tija kubwa kwenye sekta ya ardhi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja na nakushukuru sana kwa nafasi hii. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021
MHE. JERRY W. SILAA - MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA UWEKEZAJI WA MITAJI YA UMMA: Mheshimiwa Spika, awali ya yote niungane na wenzangu kukushukuru na kukupongeza wewe binafsi kwa kutoa muda wa kutosha wa ripoti za Kamati hizi tatu, kujadiliwa na Bunge kwa kipindi cha siku nne, tunakupongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pili, niwashukuru sana Wabunge kwa michango yao. Tumepata michango ya jumla ya Wabunge 83. Katika hao Wabunge 19 wamechangia hoja mahususi ya Kamati ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma tokea Novemba mpaka leo. ukiondoa waliochangia Taarifa ya Hesabu za Serikali Kuu na Serikali za Mitaa pekee, wachangiaji Taarifa ya PAC waliyagusa mashirika ya umma.

Mheshimiwa Spika, wakati nawasilisha Taarifa ya Kamati, Kamati ilikuwa na mapendekezo nane, baada ya majadiliano Kamati imeboresha mapendekezo kwa michango ya Waheshimiwa Wabunge jumla ya mapendekezo matano hivyo kupelekea jumla ya mapendekezo kufika 13.

Mheshimiwa Spika, pamoja na majukumu ya Kamati yetu ya PIC ya kuangalia ufanisi na tija ya uwekezaji na pamoja kwamba ripoti za ukaguzi zinawasilishwa ila tunazitumia tu kwa ajili ya kukokotoa vigezo vya uwekezaji. Wenzetu wa PAC wana majukumu ya hoja za ukaguzi wa mashirika ya umma.

Mheshimiwa Spika, katika michango ya Waheshimiwa Wabunge, mashirika yafuatayo ambayo tunayasimamia uwekezaji wake, yametajwa na yameonekana yana hoja za ukaguzi wa mabilioni ya shilingi. Mashirika hayo ni pamoja na NHIF, TRA, DART, KADCO, TANROADS, MSD, TPA, TRC, TAMESA, GPSA, Bodi ya Mikopo, Ngorongoro Conservation, REA, DUWASA na TANESCO. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni dhahiri hoja za ukaguzi kwenye ripoti ya CAG ya mwaka wa fedha 2020/2021 ndio yamepelekea kutofikia lengo la makusanyo ya Msajili wa Hazina kwa maana katika lengo la kukusanya gawio la shilingi bilioni 308.82 sawa na asilimia 75 ya lengo ilikusanywa. Katika michango ya asilimia 15 ya mapato ghafi, ni jumla ya shilingi bilioni 202.2 tu sawa na asilimia 51 ya lengo ilikusanywa. Kama mashirika haya yangesimamia fedha vizuri, basi wangeokoa fedha za walipakodi, faida ingeongezeka na mchango kwenye Mfuko Mkuu wa Taifa ungeongezeka.

Mheshimiwa Spika, kabla ya kusoma maoni na mapendekezo ya maazimio ya Kamati, naomba kuzungumzia mambo mawili ambayo yamechangiwa sana na Waheshimiwa Wabunge, ili kama yataboreshwa inawezekana ile mianya ya uvujaji wa mapato, katika hela za umma na matumizi yasiyo ya lazima yanaweza kufikiwa. Maeneo hayo mawili la kwanza ni la mifumo. Wachangiaji wengi wamechangia mifumo mbalimbali na kwenye mifumo nimeona kuna maeneo mawili. Kwanza mifumo mingi ni dhaifu, utasikia POS inaongezwa muda fedha zinafutwa, labda GPSA wanakuwa hawana mifumo mizuri ya uwagizaji, TANePS haijibu majibu ya manunuzi. Kwa hiyo mifumo mingi iliyopo kwenye nchi yetu ni dhaifu.

Mheshimiwa Spika, mifumo inakuwa dhaifu kwa mambo mawili tu, moja, aidha, inapewa udhaifu kwa makusudi katika kutengeneza mianya ya upigaji wa fedha za umma. Kwa sababu mfumo unapokuwa madhubuti kama ilivyo mifumo yetu ya miamala ya simu, sijawahi kumsikia hata Mheshimiwa mmoja huku anasema hela zake zilizopo kwenye miamala ya simu zimepotea, zimevuja, zimefutwa au salio halionekani. Kwa hiyo mifumo inapokuwa dhaifu inawezekana ni kwa makusudi katika kutengeneza utaratibu wa uvujifu wa mapato na matumizi ya Serikali.

Mheshimiwa Spika, eneo la pili, tuliwahi kulizungumza hapa Bungeni, ni Serikali kushindwa kufika mwisho wa mambo mawili. Moja, ni ujengaji wa mfumo wa public infrastructure kwa maana ya PKI ambao ndio mfumo unaweza kusaidia authentication ya transactions zote za kieletroniki kwenye mifumo hii ya mapato na matumizi.

Mheshimiwa Spika, la pili, kutokuwa na centralize ledger, kwa sababu ukisikia hapa kuna mtumishi ana malimbikizo ya mshahara na kuna mtumishi amestaafu amelipwa na kuna mapato yamekusanywa ghafi yameliwa, maana yake hakuna sehemu ya pamoja ambapo Taifa la Tanzania, nchi yetu, tunakuwa na centralized system ambayo inaweza kuona, vitendo kama hivi havifikiwi na kama vinafikiwa vinaweza kuonekana ni nani kafanya nini na lini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nimesema niyaseme haya kwa utangulizi kwenye mifumo na tutakuwa na maazimio mahususi. La pili, ni Bodi za Wakurugenzi. Nadhani nilichangia pale nyuma siyo vyema kwa kuokoa muda, lakini Kamati inaomba kidhati kumpongeza Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan, kwa nia yake na vitendo vyake ambavyo anaonyesha wazi, anaunga mkono si tu uwekezaji kwenye mashirika ya umma lakini sekta nzima ya uwekezaji kwenye Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, pale awali nilieleza kwamba kwenye uteuzi wa bodi Mheshimiwa Rais amewahi kunukuliwa hadharani akieleza ni jinsi gani anatimiza wajibu wake pale tu anapopelekewa uteuzi wa bodi. Kama nilivyoeleza pale awali jumla ya mashirika 23 kufikia Octoba 31, yalikuwa yana bodi zilizomaliza muda wake na hazijateuliwa. Kwa kudhibitisha kauli ile ya Mheshimiwa Rais, yako mashirika 12 yaliyopo kwenye Wizara tisa (9) ambayo tayari Mheshimiwa Rais ameshateua Wenyeviti wa Bodi na Wajumbe ambao ni mamlaka ya uteuzi wa Wizara kuteua, hawajateuliwa.

Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo hayo, naomba kutoa mapendekezo 13 na kati ya hayo kama nilivyosema pale awali nane yalipendekezwa na Kamati na matano yametokana na michango ya Waheshimiwa Wabunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, moja, Taasisi kutokuwa na bodi za wakurugenzi kwa muda mrefu kutokana na kuchelewa kuteuliwa kwa Wajumbe wa Bodi:-

KWA KUWA mashirika mengi yanayotumia mitaji ya umma yameendeshwa bila kuwa na Bodi za Wakurugenzi kutokana na bodi zilizokuwepo kumaliza muda wake;

NA KWA KUWA hadi sasa kuna taasisi na mashirika 12 ambayo yana Wenyeviti wa Bodi na bila wajumbe na taasisi za mashirika 23 ambayo hayana kabisa Wenyeviti wala Wajumbe wa Bodi, jambo ambalo ni ukiukwaji wa misingi ya utawala bora katika uwekezaji wa mitaji ya umma na kwamba ni jambo linalokwamisha upatikanaji wa tija uwekezaji unaofanywa na Serikali;

KWA HIYO BASI Bunge linaazimia kwamba: -

(a) Serikali ikamilishe uteuzi wa wajumbe wa Bodi 12 kwenye Wizara tisa ambazo Mheshimiwa Rais ameshateua Wenyeviti ndani ya miezi 3. (Makofi)

(b) Serikali ikamilishe uteuzi wa Wajumbe wa Bodi 23 kwenye Wizara 12 ambazo hazina bodi ndani ya miezi sita.

(c) Serikali ihakikishe inatimiza utaratibu wa kuanza maandalizi ya uteuzi wa bodi miezi tisa kabla bodi hazijamaliza muda wake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mbili, changamoto ya kupata vibali vya kuajiri: -

KWA KUWA mashirika ya umma yanayojiendesha kibiashara yanakabiliwa na changamoto ya upungufu wa watumishi katika kujiendesha kwake kutokana na kutegemea mchakato wa ajira unaoendeshwa na Sekretarieti ya Ajira ya Utumishi wa Umma katika kupata watumishi;

NA KWA KUWA changamoto hiyo inaathiri tija ya uwekezaji na manufaa yaliyotarajiwa kupatikana kutokana na kukosa watumishi wanaostahili kwa wakati, hata pale ambapo Shirika la Umma linakuwa na uwezo wa mapato wa kuwalipa mishahara;

KWA HIYO BASI Bunge linaazimia kwamba Serikali iweke utaratibu maalum wa kutoa vibali kwa taasisi zinazojiendesha kibiashara ili ziweze kuajiri zenyewe ajira ya moja kwa moja na kuweza kuendana na soko la ushindani kibiashara.

Mheshimiwa Spika, tatu, uwezo wa SGR kuzidi uwezo wa Bandari ya Dar es Salaam: -

KWA KUWA Bandari ya Dar es Salaam ina uwezo mdogo wa kupokea mizigo kulinganisha na uwezo wa SGR iliyoigharimu Serikali kwa uwekezaji mkubwa ilihali bandari hiyo ndio chanzo kikuu cha mizigo. Hii itachangia SGR isipate mzigo wa kutosha kwa ajili ya kusafirishwa pindi itakapokamilika;

NA KWA KUWA changamoto ya SGR kutopata mzigo wa kutosha kusafirishwa ni jambo linalokwamisha kupatikana kwa tija ya uwekezaji uliofanyika na kwamba mkwamo huo unaweza kutatuliwa kwa kuongeza Bandari ya Dar es Salaam na kujenga Bandari ya Bagamoyo;

KWA HIYO BASI Bunge linaazimia kwamba: -

(a) Serikali iharakishe utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa Bandari ya Bagamoyo.

(b) Serikali iharakishe zoezi la kuongeza ufanisi wa Bandari ya Dar es Salaam ikiwa ni pamoja na kuongeza gati za kisasa katika Bandari ya Dar es Salaam na zoezi hilo likamilike kabla ya ujenzi wa reli ya SGR kukamilika. Hatua hii itasaidia SGR kupata mzigo wa kusafirisha na hivyo tija iliyokusudiwa kufikiwa.

Mheshimiwa Spika, nne, umuhimu wa Shirika la Maendeleo (NDC): -

KWA KUWA manufaa ya mradi wowote wa uwekezaji yanategemea kuanza kwa mradi lakini Mradi wa Mchuchuma na Liganga umechukua muda mrefu katika hatua za majadiliano ambayo kwa sasa yanaratibiwa na Kamati ya Majadiliano ya Serikalini (GNT);

NA KWA KUWA kutokukamilika kwa majadiliano hayo yanayoendelea kwa muda mrefu tangu kuanza kwake ni jambo linalochelewesha upatikanaji wa manufaa ya mradi huo;

KWA HIYO BASI Bunge linaazimia kwamba, Serikali ihakikishe kuwa mazungumzo yanayoendelea katika Kamati ya Majadiliano ya Serikali (GNT), yanafika mwisho ndani ya miezi mitatu au yapelekwe NDC, lengo ikiwa kuyamaliza na kupata tija inayokusudiwa katika miradi, kwa sababu Serikali imefanya mabadiliko makubwa katika taasisi hii ikiwemo kuipatia Bodi mpya ya Wakurugenzi pamoja na Menejimenti.

Mheshimiwa Spika, tano, mikopo chechefu (non- performing loans): -

KWA KUWA imebainika kuwa baadhi ya taasisi kama vile Benki ya Maendeleo (TIB) na Benki ya Biashara (TCB) zinakabiliwa na changamoto ya kuwa na kiasi kikubwa cha mikopo chechefu (non-performing loans);

NA KWA KUWA hali hiyo inaathiri mizania ya vitabu vya taasisi hizo jambo ambalo ni hatari kwa misingi ya kibiashara na uendeshaji wa taasisi zinazotumia mitaji ya umma;

KWA HIYO BASI Bunge linaazimia kwamba: -

(a) Serikali ifanye tathmini ya madeni hayo na kuhakikisha wanayaondoa kwenye vitabu vya benki hizo bila kuathiri ulipaji wa mikopo inayolipika (performing loans). Hatua hiyo itasaidia benki hizo kufanya kazi kwa ufanisi na kuleta tija inayokusudiwa.

(b) Serikali itengeneze mfumo fungamanishi kati ya Bodi ya Uhasibu (NBAA), Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), na Taasisi za Fedha na wafanyabiashara ili chanzo cha hesabu zote zinazotumiwa na wafanyabiashara kiwe kimoja. Hii itasaidia kukadiria kiwango halisi cha mkopo kinachoweza kulipika na mkopaji ili kupunguza mikopo chechefu.

Mheshimiwa Spika, sita, upungufu wa mtaji wa Kampuni ya Ndege Tanzania (ATCL):-

KWA KUWA Kampuni ya Ndege Tanzania (ATCL) inakabiliwa na changamoto ya mtaji hasi na changamoto ya uendeshaji wa biashara kutokana na utaratibu wa kukodisha ndege kutoka Wakala wa Ndege za Serikali (TGFA);

NA KWA KUWA utaratibu huo unaongeza madeni wanayodai yaani payables katika vitabu vya TGFA.

KWA HIYO BASI Bunge linaazimia kwamba, Wakala wa Ndege za Serikali Tanzania (TGFA) ikamilishe taratibu za kutekeleza agizo la Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, alipokuwa anapokea Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali tarehe 30 Machi, 2022 la kurudisha umiliki wa ndege kwa ATCL kwani ukiondoa tatizo hili ATCL ina uwezo wa kujiendesha kwa faida. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, saba, kuiwezesha Benki ya Maendeleo ya Kilimo(TADB): -

KWA KUWA TADB ambayo ndio benki pekee inayohusika moja kwa moja na shughuli za kilimo, lakini haijapatiwa mtaji wa kutosha na kuendana na nia ya Serikali ya kuongeza tija kwenye kilimo, kuleta mageuzi ya kilimo na kulisaidia Taifa kufikia usalama wa chakula;

NA KWA KUWA pamoja na jitihada za Serikali kuipatia TADB kiasi cha shilingi milioni 208 mwaka 2021, bado kuna ahadi ya Serikali ambayo kama ingetekelezwa benki hii ingekuwa na mtaji wa jumla ya shilingi bilioni 760. Kutofikiwa kwa mtaji huu kunaathiri ufanisi na tija katika sekta ya kilimo;

KWA HIYO BASI Bunge linaazimia kwamba, Serikali itekeleze ahadi yake (commitment) waliyoitoa kwa TADB ya kuiongezea mtaji kiasi cha shilingi bilioni 100 kwa kila mwaka wa fedha, lengo likiwa ni kuongeza ufanisi katika sekta ya kilimo.

Mheshimiwa Spika, nane, kuathirika kwa kilimo cha pamba kutokana na maelekezo ya Serikali ya mwaka 2019 ya kuuza pamba kwa bei ya juu zaidi ya soko la dunia:-

KWA KUWA agizo la Serikali inayoitaka pamba kununuliwa kwa bei ya juu zaidi ya soko la dunia imeathiri uwezo wa wanunuzi wa pamba kwa kiasi cha shilingi bilioni 21.8, kiasi ambacho Serikali iliahidi kufidia deni hilo;

NA KWA KUWA deni hilo limeathiri taswira ya Bodi ya Pamba kwa wakulima na kuongeza changamoto katika biashara ya kilimo cha pamba;

KWA HIYO BASI Bunge linaazimia kwamba, Serikali iharakishe utekelezaji wa ahadi yake ya kulipa deni la pamba. Hatua hiyo itasaidia kuongeza ufanisi wa sekta hiyo na kurudisha taswira chanya ya Bodi ya Pamba.

Mheshimiwa Spika, tisa, mwingiliano wa majukumu kwa baadhi ya taasisi za umma:-

KWA KUWA mwaka 2017 Serikali iliamua majukumu ya Tanzania Air Port Authority ya kujenga viwanja vya ndege yahamie TANROADS;

NA KWA KUWA jambo hili ni kinyume cha viwango vya kimataifa na ni kinyume cha matakwa ya International Civil Aviation Organization (ICAO) ambayo Tanzania Air Port Authority ni mwanachama wake na ICAO inazitaka Mamlaka za Viwanja vya Ndege kusimamia shughuli zote za viwanja vya ndege ikiwemo ujenzi wa viwanja vyao;

KWA HIYO BASI Bunge linaazimia kwamba Serikali itekeleze haraka agizo la kurejesha jukumu la ujenzi wa viwanja vya ndege kwa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege (TAA) pamoja na rasilimali zake zote ikiwemo watumishi waliohama mwaka 2017. Hii ni muhimu kwa ajili ya kukidhi viwango vya kimataifa katika uendeshaji wa viwanja vya ndege. (Makofi)

(10) Matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA).

KWA KUWA, katika Mpango wa Tatu wa Maendeleo ya Taifa ya Miaka Mitano, Serikali inatekeleza mageuzi ya kidigitali yanayojumuisha teknolojia ya TEHAMA, kuwa nyenzo muhimu katika kuongeza ufanisi kwenye mifumo ya uzalishaji huduma na utawala;

NA KWA KUWA, mashirika mengi ya umma hayazingatii matumizi sahihi ya TEHAMA hali inayopelekea upotevu wa mapato na udanganyifu katika utoaji huduma zake;

KWA HIYO BASI, Bunge linaazimia kwamba: -

(a) Serikali ikamilishe mchakato wa public infrastructure (PKI)

(b) Serikali iunde mfumo wa taarifa ya pamoja (centralized ledger) kuondoa udanganyifu wa mifumo ya taasisi.

(c) Serikali ihakikishe inasimamia kikamilifu taasisi na mashirika ya umma kuimarisha mifumo ya TEHAMA. Hatua hizi zitasaidia kuongeza ufanisi wa utoaji huduma, ukusanyaji wa mapato, kupunguza matumizi yasiyo ya lazima na kudhibiti udanganyifu kwa lengo la kupata tija inayokusudiwa.

(11) Changamoto ya uendeshaji wa Kampuni ya Meli (Marine Services Company).

KWA KUWA, Kampuni ya Meli (MSC) iliyokuwa chini ya usimamizi wa Mamlaka ya Bandari kwa sasa imekuwa Kampuni huru inayojitegemea;

NA KWA KUWA, kitendo cha Mamlaka ya Bandari kuendelea kumiliki baadhi ya mali za (MSC) kunaathiri utendaji wa (MSC) ikiwa ni pamoja na uendeshaji wa mtaji wa umma uliowekwa (MSC);

KWA HIYO BASI, Bunge linaazimia kwamba Serikali iharakishe mali zote za (MSC) zilizopo Tanzania Port Authority zirejeshwe haraka sana (MSC) zikiwemo chelezo, karakana na nyinginezo.

(12) Matumizi ya TEHAMA katika Mfuko wa Taifa ya Bima ya Afya (NHIF).

KWA KUWA, Mfuko wa Bima ya Afya ya Taifa (NHIF) umeonesha udhaifu katika utoaji wa huduma zake jambo ambalo limepelekea Mfuko kupata hasara;

NA KWA KUWA, changamoto zilizojitokeza katika uendeshaji wa (NHIF) kwa kiasi kikubwa imetokana na kutokakuwa na mfumo thabiti wa TEHAMA inayotoa mianya ya kufanya udanganyifu kwa urahisi;

KWA HIYO BASI, Bunge linaazimia kwamba Serikali ihakikishe (NHIF) inaandaa mfumo madhubuti wa TEHAMA na kuanza kuutumia haraka iwezekanavyo kwa lengo la kuboresha utoaji wa huduma wa mfuko na kuziba mianya ya udanganyifu. (Makofi)

(13) Matumizi makubwa ya gharama za bima za Ndege kwa Shirika la Ndege la Taifa - ATCL.

KWA KUWA, Shirika la Taifa la ATCL linalazimika kununua Bima kutoka Shirika la Bima la Taifa (NIC) ambapo NIC ananunua Bima hizo kutoka kwa Wakala wa Nje ya Nchi kwa mfumo wa moja kwa moja single source;

NA KWA KUWA, changamoto zilizojitokeza ni kwa Shirika la Ndege kujikuta linanunua bima hizo kwa gharama kubwa hali inayopelekea kupunguza faida na tija kwa Shirika;

KWA HIYO BASI, Bunge linaazimia kwamba Serikali ielekeze ATCL na NIC kufanya zabuni shindanishi ili kupata wakala mwenye bei nafuu, huduma bora na ambaye atazingatia uwiano wa ndege, shirika anazomiliki, hii italeta ufanisi, tija na kupunguzia shirika gharama za matumizi.

Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja. (Makofi)

MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, naafiki.
Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026
MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Spika, nami nakushukuru kupata fursa ya kuchangia kwenye Mpango huu wa Miaka Mitano. Nakushukuru zaidi kwa sababu pamoja na kupongeza Mpango huu mzuri, nitaanza kuchangia si mbali sana na alipomalizia mchangiaji aliyepita.

Mheshimiwa Spika, kwanza, niipongeze sana Serikali kwa kuja na Mpango huu ambao ukiusoma umezingatia sana michango ya Wabunge waliyotoa wakati Mpango huu umewasilishwa. Pia ukiusoma Mpango huu unakuja kuendeleza pale Mpango wa Miaka Mitano iliyopita; Mpango wa mwaka 2015-2020 ambao tumeona Serikali ikiwekeza kwenye miradi mikubwa ya kimkakati ambayo inaenda kulifanya Taifa letu kuwa na uchumi unaojitegemea.

Mheshimiwa Spika, kazi kubwa imefanyika na inaendelea kufanyika kwenye Bwawa la Stigler’s Gorge. Kazi kubwa imefanyika na inaendelea kufanyika kwenye Reli ya Standard Gauge. Kazi kubwa imeendelea kufanyika katika miradi ya kufufua Mashirika ya Umma ikiwepo Shirika letu la Ndege la ATCL. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na mambo mengine na mimi kidogo ni Mwanasheria. Ukisikiliza mchango wa Mwanasheria mmoja hapa dada yangu nauona kabisa umepungua sana knowledge ya kimkakati kwenye miradi ya kimaendeleo na fedha. Unapoongelea Shirika la ATCL…

SPIKA:Mheshimiwa Halima usikilize vizuri unasomeshwa shule hapa. Hii ni shule unasomeshwa, kwa hiyo tulia. Endelea Mheshimiwa. (Kicheko)

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Spika, kule kwenye sheria tunafundishwa purposive approach ya legal interpretation, kwamba unasoma sheria kama ilivyoandikwa, kwenye fedha hatufanyi hivyo. Unapoongelea Shirika la Ndege, kwanza lazima utambue ni Shirika ambalo lilikuwa lina-operate kwa ndege moja. Katika miaka mitano iliyopita, Serikali imefanya kazi kubwa ya kufufua Shirika hili. Ndege ya kwanza imepokelewa mwishoni mwa mwaka 2017, zimekuwa zikipokelewa ndege mpaka tunavyozungumza zimepokelewa ndege nane (8) na ndege tatu (3) zitakuja kwenye Shirika hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa wale wenye kufanya biashara wanafahamu, huwezi ukawa unafufua Shirika at the same time ukawa unatengeneza faida, haijawahi kutokea. Ziko aina ya biashara ambazo mpaka sheria zetu za kodi zinaruhusu hasara miaka mitatu mpaka miaka mitano. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wako Waheshimiwa Wabunge hapa wamesema, Shirika la Ndege si biashara bali ni huduma inayoenda kuchochea maeneo mengine ya biashara. Ukisoma Ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali, maana Financial Statement hazisomwi kwenye purposive approach, husomi tu ile hasara ukabeba ukaleta hapa Bungeni kuja kupotosha umma wa Watanzania, unasoma uwanda mpana wa ripoti ile.

Mheshimiwa Spika, yapo madeni ya kurithi kwenye Shirika hili, lakini ningetegemea maana na majina tunaitwa wengine Njuka ningetegemea maneno hayo yasemwe labda na Njuka, mzoefu alitakiwa kufahamu kwamba hata ndege hizi zilivyonunuliwa zinamilikiwa na TGFA, ATC inazikodisha. Kwenye Ripoti ile ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali ukiisoma inasema kabisa kwamba kuna deni limetokana na kipindi ambapo TGFA inakodisha ndege ATC lakini wote tunafahamu, si ATC peke yake au hamtembei jamani, dunia nzima ndege zimepaki kwa sababu ya COVID- 19! Hili siyo Shirika pekee lililoathirika! (Makofi)

T A A R I F A

MHE. ELIBARIKI I. KINGU: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Elibariki.

MHE. ELIBARIKI I. KINGU: Mheshimiwa Spika, nataka nimpe msemaji taarifa kwamba dunia kwa ujumla, kwa mwaka huu peke yake ime-accumulate loss ya dola bilioni 118 katika Mashirika ya Ndege. Kwa hivyo, hii haiwezi kutu- discourage sisi tuone kwamba ATC haina faida kwa Watanzania. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Jerry endelea.

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Spika, nimeipokea taarifa. Unaponunua ndege kwenye mizania ya kampuni ni capital expenditure. Kumbuka manunuzi haya yatakuja na mafunzo ya wataalam, marubani, wahandisi, kuboresha karakana; zote hizo huwezi ukaanza kuona faida kwenye miaka hii ya mwanzo. Pia ndege hizi, maana msemaji anasema ndege zimepaki, ndege haziruki kama kunguru zinaruka kwa mpango. (Makofi/Kicheko)

SPIKA: Mheshimiwa Jerry Silaa bado dakika tano zako. (Makofi/Kicheko)

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Spika, sisi wengine tumekulia kwenye familia za aviation. Tumenunua ndege za Bombadier Q4100 kwa sababu ya safari za ndani. Tumenunua Airbus, jamani hata mitandao hamuangalii? Ukiona Mheshimiwa Rais Mama Samia anasafiri ndani anasafiri na Q4100; jana ameenda Uganda na Airbus kwa sababu ndege zile zimenunuliwa kwa sababu ya Regional Flights. Zile Dreamliner, kila siku mnatangaziwa kwamba zilinunuliwa kwa sababu ya safari za masafa, trip za Guangzhou, London, India, ndege ya moja kwa moja toka nchini kwetu. Ukitoka zako ulikotoka ukaja Jijini Dar es Salaam ukakuta zimepaki, usishangae, mashirika haya yameathiriwa na magonjwa ya COVID-19 ambayo imeathiri sana usafirishaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho, tunapofanya capital expenditure yoyote huwezi kuepuka kukopa. Swali huwa unakopa ufanyie nini? Kama tunakopa kwa ajili ya miradi mikubwa ya kimkakati, miradi hii ina tija kubwa kwenye uchumi wa nchi yetu, ni jambo la kupongezwa wala si jambo la kubezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ombi langu kwa sisi tuliopewa dhamana na wananchi wa Tanzania, bila kujali umeingilia mlango gani, maana wako Wabunge hapa Vyama vyao wenyewe vinawakana…(Kicheko)

Mheshimiwa Spika, lakini sisi tunawaheshimu kama Wabunge wenzetu, tukisimama hapa kuchangia tuweke maslahi mapana ya nchi yetu.

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Spika, tuweke maslahi mapana ya legacy aliyotuachia Rais wetu na tuisaidie Serikali.

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha. Naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja iliyoko mezani ya Ofisi ya Rais TAMISEMI.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nichukue fursa hii kuipongeza sana Wizara ya Ofisi ya Rais – TAMISEMI kwa kazi nzuri sana wanayoifanya. Nampongeza kaka yangu Mheshimiwa Innocent Bashungwa, Mbunge kwa kuaminiwa na kuteuliwa kuiongoza Wizara hii na Naibu Mawaziri wake Mheshimiwa Dkt. Festo Dugange na Mheshimiwa David Silinde kwa kazi nzuri wanayoifanya kwa kuwa karibu na Wabunge kwa kutusikiliza na kuwa wanyenyekevu katika kutumikia Taifa letu. Binafsi niwaahidi ushirikiano, vijana wenzetu tupo tutawalinda, tutawatetea katika kutekeleza majukumu yenu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia nimpongeze Rais wetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kuleta fedha nyingi za maendeleo kupitia kwenye Wizara hii. Tumesikia kwenye Hotuba ya Waziri, fedha zilizokuja za barabara kupitia TARURA kila Jimbo tumepata fedha hizi, tunaishukuru na kumpongeza sana Rais. Tumepata pesa za tozo kujenga vituo vya afya, Jimbo la Ukonga tumepata bilioni 1.5, Kituo cha Afya Kipunguni kinajengwa, Kituo cha Afya Majohe na Kituo cha Afya cha Zingiziwa tunaishukuru na kuipongeza sana Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeendelea kuleta fedha za elimu bila malipo, shilingi bilioni 1.2 kwenye elimu ya msingi na shilingi bilioni 3.84 kwenye elimu ya sekondari kwenye Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam zimepokelewa, tunaishukuru na kuipongeza Serikali. Ujenzi wa zile shule za kimkakati kwenye Mradi wa SEQUIP fedha zimeanza kupokelewa na kule Jimbo la Ukonga shule itajengwa kwenye Kata ya Mbondole na kuna mpango mwingine wa shule nyingine kwenye Kata ya Kitunda, tunaishukuru sana Serikali.

Naomba Serikali, niiombe sana tuendelee kutenga fedha hasa za barabara kwenye majimbo yote lakini kwenye Jimbo la Ukonga tunaomba sana Serikali, uendelezaji wa mradi wa DMDP awamu ya pili ambacho ndiyo kilio kikubwa cha wananchi wengi wa Jimbo la Ukonga na Mkoa wa Dar es Salaam kama wenzetu tulivyosikia hapa kwenye hotuba ya Waziri, mradi wa TACTIC ambao ni uendelezaji wa mradi wa Tanzania Strategic City Project ambao umeanza, tunaiombe Serikali ijitahidi kuongeza kasi ya mazungumzo na Benki ya Dunia ili Mradi wa DMDP awamu ya pili na wenyewe uweze kuanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kule Dar es Salaam na kule Jimbo la Ukonga pamoja na fedha hizi za TARURA zilizoletwa na Mheshimiwa Rais, Wabunge wengi hapa alivyotambulishwa Engineer Seif wamepiga makofi kutokana na fedha zile kupokelewa kwenye majimbo karibia yote nchi nzima. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuiombe sana Serikali barabara nyingi za Dar es Salaam kile kigezo cha traffic density, cha wingi wa magari yanayotumia barabara kimezidi yale magari 400 ya kujenga barabara kwa kiwango cha changarawe na kiukubwa ni kujenga barabara kwa kiwango cha lami. Barabara za Pugu - Majohe, barabara za Banana - Kitunda - Kivule tunategemea kwenye mradi huu wa DMDP tukipata fedha zitajengwa kwa kiwango cha lami. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye eneo la barabara niombe mambo mawili; jambo la kwanza niiombe sana Serikali inapogawa fedha hizi basi vigezo vya kitaalam vya wenzetu vya TARURA vizingatiwe. Majimbo mengi yanatofautiana urefu wa kilometa za barabara, majimbo mengi yanatofautiana changamoto za ujenzi wa vivuko na madaraja. Nikuombe radhi hata humu Bungeni kwako ikitokea unagawa huduma yoyote ya mpango ya uzazi salama hauwezi Bi. Asha Mshua ukamuweka kundi moja na Ng’wasi Kamani, lazima utaweka kwa vigezo vyao na umri wao kutokana na hali halisi ya mazingira ya uzazi salama. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikuombe sana kwenye mgao wa fedha hizi ombi la pili na wenzetu wa Zanzibar kwa mahusiano mazuri ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar mnapogawa fedha hizi za barabara, basi kama tulivyofanya kwenye fedha za UVIKO na wenzetu wa majimbo ya Zanzibar nao muangalie jinsi ya kuweza kuwafikishia fedha za barabara ili kuwe na usawa wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi naomba nizungumzie system za structures za Serikali za Mitaa, leo hapa tumeombwa zaidi ya trilioni 4.6 kama mishahara kwenye Serikali za Mitaa kwa jumla ya watumishi zaidi 319,000, tumeombwa fedha za maendeleo zaidi ya shilingi trilioni 3.26 ambazo zinaenda kutekelezwa kwenye Serikali za Mitaa. Lakini Serikali za Mitaa zimeundwa kwa mujibu wa Katiba, zinapata mamlaka yake kwenye Ibara ya sita, Ibara ya nane, Ibara ya 145 na Ibara ya 146 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Wananchi wa Tanzania wenyewe ndiyo wameamua kwenda kutengeneza Serikali za kusimamia maendeleo yao. Fedha hizi zinaenda kule chini kuna Wenyeviti wa Vijiji, kuna Wenyeviti wa Mitaa, kuna Waheshimiwa Madiwani, tujiulize swali moja la msingi je, mifumo na miundo ya Halmashauri hizi inawapa mamlaka ya kutosha ya kusimamia uwezo wa miradi hii ya maendeleo? Halmashauri hizi zinawezeshwa na watendaji hawa kwenda kusimamia watumishi hawa? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kazi kubwa inapaswa kufanyika, kazi ya kwanza kwenye miundo. Muundo wa Halmashauri zetu tukitoka hapo nje getini ukamtafuta Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa kama ana ufahamu wa bajeti hii inayosomwa na Waziri, nadhani majibu yake utayapata. Kuna kazi kubwa ya kurekebisha muundo wa Halmashauri, ili Waheshimiwa Madiwani wapate fursa ya kujadili bajeti hizi kwa kina kabla hazijafika hapa Bungeni.

Mheshimiwa Naibu Spika, kule kwenye Halmashauri imekuwa ni desturi ya bajeti hizi kupita kwa kasi na kuwa na haraka ya kupita yale malengo ya Regional Secretariat na kuleta Bungeni.

Mhshimiwa Naibu Spika, lakini la pili; je, Wenyeviti wa Mitaa, Vijiji na Vitongoji; je, Waheshimiwa Madiwani wanapata mafunzo ya kutosha ya kuweza kusimamia rasilimali fedha na rasilimali watu kule kwenye Halmashauri zetu?

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini jambo la tatu niipongeze Serikali toka mwaka fedha uliopita imeanza kulipa posho za Madiwani. Lakini je, posho hizi zinatosha? Je, posho za Wenyeviti wa Vijiji na Vitongoji zinatosha? Hivi kweli Mwenyekiti wa Mtaa analipwa posho ya shilingi 100,000 kwa mwezi, ataacha kuwa- charge wananchi gharama za kuandika barua ofisini? Ataweza kweli kusimamia maendeleo kwenye eneo lake?

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme ifike wakati Serikali itengeneze muundo mzuri wa kuwawezesha kimuundo, kimafunzo, lakini kimaslahi viongozi wetu hawa wa Mitaa, Vijiji na Vitongoji na Waheshimiwa Madiwani waweze kusimamia majukumu yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho ni Halmshauri zenyewe Serikali kuzitendea haki. Mwaka 2019/2020 kodi ya majengo (property tax) ilikuwa inakusanywa na Halmashauri zetu; na pale Halmashauri nyingi za Dar es Salaam tulikusanya shilingi bilioni tisa, lakini mwaka 2021zilipelekwa TRA. Fedha hizi hazikukusanywa wala hazikuletwa kwenye Halmashauri kuja kutekeleza majukumu yetu. Mwaka 2021/2022 zimepelekwa kwenye LUKU, sijui hii mwaka 2022/2023 mtazileta wapi? Niiombe sana Serikali tuziwezeshe Halmashauri zetu, tuzipe mamlaka ya kukusanya mapato yake, zitengenezewe malengo na zisimamiwe kuweza kutekeleza majukumu kwa wananchi wake. Hata hao Wenyeviti wa Mitaa, Wenyeviti wa Vijiji, Waheshimiwa Madiwani, wawekewe malengo ya kukusanya mapato, kuwe na sera ya retention ili waweze kuendesha shughuli zao kwenye ofisi zao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Ofisi ya Mtaa inapokuwa na retention ya kodi ya majengo haitam-charge mwananchi barua ya dhamana kulipia kwenda kumtoa ndugu yake aliyekuwa na matatizo mahakamani. Watakuwa na uwezo wa kujiendesha, kutoa mafunzo kwa wananchi wao, hata kusimamia vikundi vya kina mama na vijana na walemavu wanaopata mikopo ya Halmashauri hata kuwaandikia katiba, kuwasajilia vikundi; na huu uwezeshaji wa wananchi utafika kwenye maeneo ya mitaa, vijiji na vitongoji na Waheshimiwa Madiwani leo watakuwa na uwezo wa kusimamia halmashauri zao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuheshimi muda na kwa wachangiaji waliopo leo, naomba niseme naunga mkono hoja iliyowekwa mezani na Waziri wa Nchi, naomba kuwasilisha. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Fedha wa Mwaka 2020 (Toleo la Kiingereza)
MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa nafasi kuchangia kwenye Finance Bill ya Mwaka 2021. Kama muda utaruhusu nitachangia kwenye maeneo manne; Part VIII, The Amendment of Income Tax Act, Chapter 332 ambayo nitachangia kwa pamoja na Part XXI, Amendment of the Tax Administration Act.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Sheria ya Income Tax ndiyo inakusanya kodi na Tax Administration Act ndiyo inatoa utaratibu wa kukusanya kodi pamoja na adhabu. Ukisoma bajeti, ukurasa wa 52 kuna maneno ya kufanya marekebisho kwenye Regulation ama the Transfer Pricing Regulation za Mwaka 2014 kuondoa adhabu ya asilimia 100 kwa wale watakaobainika kufanya vitendo hivi vya Transfer Pricing. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mambo makubwa yanayopoteza kodi ya nchi yetu hasa kwenye makampuni makubwa ni Transfer Pricing. Ukisoma ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali, Audit on Transfer Pricing, kwenye Executive Summary Part XVI, Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali ametoa mapendekezo kwa Wizara kui-support Mamlaka ya Mapato Tanzania kuongeza nguvu kwenye suala la kusimamia Kitengo cha International Tax Unit katika kuhakikisha tunaondosha utoroshwaji wa fedha nchini kupitia Transfer Pricing.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa bahati mbaya sana, naamini taarifa hii tutaijadili Bunge linalofuata, Wizara ya Fedha badala ya kutengeneza utaratibu wa kutoa support inaleta mabadiliko ya kwenda kuondoa adhabu kwenye jambo ambalo ni kosa kisheria. Ukurasa wa 23 wa Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali inaonyesha Kitengo hiki cha ITU kwa miaka zaidi ya mitatu kimefanya ukaguzi kwenye asilimia 33 tu ya makampuni ambayo yameainishwa kama the most risk companies kwenye Transfer Pricing. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuombe na niliombe Bunge hili na Mheshimiwa Waziri wa Fedha kwa lugha ya mjini tunasema hii umechomekewa, usisaini kanuni hii, ukisaini unaenda kuipa Serikali hasara kubwa ambapo siku za nyuma tulikuwa tumeshaondoka. Niseme tu na Mheshimiwa Waziri wa Fedha atakuwa anafahamu, ipo kesi, The Civil Appeal Case No. 144 ya Mwaka 2018 ambayo imetolewa hukumu tarehe 20 Agosti, 2020 na panel ya Majaji watatu wa Mahakama ya Rufaa ikiongozwa na Jaji Mkuu Ibrahimu Juma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kesi hii imeenda kutoa hukumu ya kodi ya zaidi ya dola za Kimarekani milioni 900 kwa kampuni ya African Barrick ambayo kwa miaka mitatu mfululizo ili-declare loss hapa Tanzania, lakini iligawa dividends kwa wanahisa wake kule Uingereza. Kampuni ile haina mali yoyote duniani zaidi ya ile migodi mitatu na ukitaka kujua fedha hizi ziliondokaje nchini ziliondoka kwa Transfer Pricing. Sasa mnapoenda kusema mnataka kufuta kanuni hii ya adhabu kwa kigezo cha kusema eti unaenda kuhamasisha uwekezaji, aliyeandika hili Mungu anamuona, ameandika akijua wazi haendi kukuza uwekezaji.

T A A R I F A

MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa.

MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimpe taarifa mzungumzaji kwenye kesi hiyo ambayo anaizungumzia hapa ni kwamba pia hawa Barrick wali-declare kwenye kesi ile kwamba walitumia kiasi cha asilimia 2 kama fedha za CSR katika ujenzi wa miradi mbalimbali katika Jimbo langu la Msalala, Kata ya Bulyankulu. Hata hivyo, mpaka hivi tunavyozungumza zile asilimia 2 ambazo walizi-declare kule mahakamani zile nyumba ambazo walijenga kwa fedha hizohizo za CSR walienda kuziuza tena kwa wafanyakazi na sasa hatujui hizo fedha ziko wapi. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante. Mheshimiwa Jerry.

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa taarifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, labda niseme tu kwamba masuala haya ya Transfer Pricing siyo mambo ya kujifungia sisi wenyewe. Kuna mkutano ulifanyika Addis Ababa unaitwa The Addis Ababa Action Agenda ulifanyika tarehe 15 Julai, 2015. Mkutano huu labda kwa sababu muda tu ni mfupi ulieleza mambo mengi sana kuhusiana na Transfer Pricing, ilieleza ni jinsi gani fedha nyingi zinatoka Africa kila mwaka katika utaratibu huu. Niliombe Bunge hili lakini nimuombe Waziri kwamba jambo hili likienda kufanyika tunaenda kutengeneza hasara kubwa sana kwa Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu, ile ni adhabu kwa yule anayebainika amekwepa kodi ile siyo kodi. Tumetoa hapa ada ya faini za barabarani kwa bodaboda toka shilingi 30,000 mpaka shilingi 10,000, lakini adhabu bado ipo, unaenda kuondosha adhabu maana yake unaenda kuhalalisha kosa, unaenda kumfanya mtu sasa afanye kosa kwa amani kwamba hata akikamatwa hakuna adhabu. Ningetegemea labda adhabu hii itoke asilimia 100 iende zaidi ya hapo ili kutengeneza uwoga kwa makampuni haya makubwa ambayo kwa miaka mingi yanalipa kodi ndogo kuliko Watanzania wazawa wanaofanya biashara hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo wafanyabishara wa Tanzania wa kawaida kabisa wana adhabu ukichelewesha returns una adhabu…

MHE. DKT. PINDI H. CHANA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa

MWENYEKITI: Taarifa.

T A A R I F A

MHE. DKT. PINDI H. CHANA: Mheshimiwa Mwenyekiti, msemaji anazungumza point nzuri sana, muhimu sana, tuna vijana takribani asilimia 50 ya idadi ya watu wa Tanzania. Nampa taarifa kwamba tunavyopunguza adhabu ya pikipiki na kufanya shlingi 10,000 ni lazima tujue taarifa ni ajali ngapi zilikuwepo wakati faini ni shilingi 30,000 na faini ikiwa shilingi 10,000 kutakuwa na ajali ngapi? Hii ni taarifa sisi kama Bunge na msemaji lazima aizingatie wakati anachangia ili kuokoa watu wasikatwe miguu kwenye ajali za pikipiki, nampa taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Jerry, taarifa.

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru naamini dakika zangu unazilinda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mimi nilikuwa na mengi sana ya kuchangia hata dakika zikiniishia kwenye hili la Transfer Pricing nitasimamia na nimuombe Waziri asijaribu kuingia kwenye historia hiyo. Kama hilo litafanyika na wewe utaingia kwenye historia kwamba uli-chair kikao ambacho kimeenda kufanya jambo hilo la kuweza kudhulumu haki za Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili nataka kuchangia ni Part IX ya Amendment ya Local Government Authorities (Rating) Act, Chapter 289. Kodi ya Majengo ina historia yake, inapata historia kwenye karne ya 17. Kule Uigereza Malkia Elizabeth I mwaka 1601 walipitisha sheria inayoitwa The Poor Relief Act iliyokuwa inatoa mamlaka kwa mamlaka za Local Government kukusanya kodi kwenye majengo ili kuwatengenezea huduma wakazi wakazi wa maeneo yale, The Property Tax. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye hii Part IX, Serikali imeleta mabadiliko inataka kuongeza section 31A inayotaka fedha hizi na wewe uko pale Ilala unafahamu majengo pale wapiga kura wako wanavyotaka huduma kupitia Property Tax zao, kifungu hiki cha 31A kinakwenda kupeleka pesa hizi kwenye Consolidated Fund na inarudishwa asilimia 15 si kwenye mamlaka husika zinarudi TAMISEMI zigawiwe nchi nzima. Labda watafute jina lingine la kodi hii na mimi nitaunga mkono kama ni Kodi ya Maendeleo au Kodi ya Miradi, naomba nilindie dakika zangu, hizo ni kumi zile za mwanzo bila taarifa. Kama tunataka kuipa jina lingine tuipe kodi jina lingine, lakini kama itaitwa The Property Tax msingi wake ni Kodi ya Majengo na wenye majengo yao kwenye mamlaka zile za Serikali za Mitaa wanasubiri huduma, wanasubiri barabara na mitaro, niiombe Serikali iliangalie hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la mwisho kwa dakika moja naomba nichangie Part XIII. Serikali inataka kurekebisha The Non-Citizen Employment Regulation na kutengeneza faini ya shilingi laki tano kwa wafanyakazi wageni. Tarehe 6 Aprili, mmemsikia Mheshimiwa Rais akitoa wito kwa wenzetu wa vibali vya kazi kutaka kuondoa urasimu kuwasaidia wawekezaji kupata vibali vya kazi. Kibali Class A ni dola 3,050, kibali Class B ni dola 2,050 bado Labour wanachukua dola 1,000 na unreturn fees ya application, halafu unataka umdai mwekezaji huyu shilingi laki tano eti hajaleta return ya watumishi wake. Tunaenda kukwamisha uwekezaji kwenye nchi hii, kila mwezi mnaenda kuwagongea milango yao. Hatuwezi tukawa tuna nchi ambayo mtu anakuja serious investor anaomba serious permit analipa three thousand dollars halafu kuna mtu anataka kwenda kumgongea mlango wake kila mwezi amdai laki tano kwa sababu hajaleta return ya watumishi wake, mnaenda kukwamisha uwekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa huku kwenye Transfer Pricing mnaenda kupoteza mabilioni mnasema mnakuza uwekezaji mnakuja huku mnachukua shilingi laki tano kwa mwezi. Naomba Waziri wa Fedha hii Amendment ya Part XIII aiondoshe, hatuwezi kuwa na nchi ya aina hii ya kwenda kusumbua watu wanaokuja na mitaji yao. Tutakuwa ni nchi ya kipekee duniani ambayo tuna tamaa na fedha za watu na tutakwamisha uwekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nikushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia bajeti hii ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI. Nami niungane na wenzangu kumpongeza sana dada yetu Mheshimiwa Ummy Mwalimu na wenzake wote kwa nafasi na fursa waliyoipata kutumikia Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wangu nitauelekeza kwenye maeneo matatu lakini kwanza ni kwenye Jiji la Dar es Salaam. Jiji la Dar es Salaam lina historia ndefu kuanzia mwaka 1920 lililopata hadhi ya kuwa mji mpaka lilipokuwa Manispaa ya Dar es Salaam mwaka 1949 na lilipopata hadhi ya kuwa Jiji tarehe 10 Desemba 1961. Mafunzo tuliyoyapata kutoka mwaka 1972 mpaka mwaka 1978 kwenye Madaraka Mikoani na mafunzo tuliyoyapata kuanzia mwaka 1996 mpaka 2000 kwenye Tume ya Jiji, naamini tunaweza kuyatumia kwa upana wake katika kuhakikisha tunatengeneza mbinu bora zaidi ya kutengeneza mazingira ya uongozi na utawala kwenye Jiji la Dar es Salaam.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie fursa hii kuishukuru Serikali kwa kuanzisha ama kwa kuipandisha hadhi Manispaa ya Ilala kuwa Jiji la Dar es Salaam. Tunapozungumzia masuala ya majiji, tunazungumzia maisha ya watu na makazi kwa maana ya urbanization, lakini niseme tu kwamba Dar es Salaam kwa kipindi kirefu imekuwa ikiendeshwa bila master plan. Master plan ya mwisho iliandikwa mwaka 1979 na kwa bahati mbaya hizi master plan huwa zinatakiwa kuhuishwa kila baada ya miaka mitano. Hata hivyo, master plan hii ilikuja kutangazwa kwenye Gazeti la Serikali mwaka 1984 miaka mitano muda ambao ulitakiwa master plan hii ihuishwe lakini tokea wakati huo jiji hili limekosa master plan. Naomba nichukue fursa hii kuipongeza Serikali kwamba mwezi Juni, 2020 katika Gazeti la Serikali tumetangaziwa master plan ya Jiji la Dar es Salaam. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunavyozungumzia master plan ya Jiji la Dar es Salaam tunazungumzia Mkoa mzima wa Dar es salaam, lakini tunazungumzia wilaya za jirani ambazo kutokana na ongezeko la makazi, sasa zimeungana na Jiji la Dar es Salaam. Wilaya za Bagamoyo, Kibaha, Kisarawe na Mkuranga, zote sasa zimeungana na Jiji la Dar es Salaam. Sasa tumepata Jiji pale kwenye Manispaa ya Ilala imekuwa Jiji la Dar es Salaa lakini juzi tumeona Manispaa ya Temeke nayo imeomba na ina vigezo vya kuwa jiji naamini Kinondoni nayo itafika wataomba jiji na naamini kuna siku Ubungo nao wataomba jiji, tutakuwa na majiji mengi. Dhana hasa ya kuwa na jiji ni ya kupata mamlaka yenye uwezo wa kusimamia master plan hii ya Jiji la Dar es Salaam.

Mheshimiwa Naibu Spika, yuko Mheshimiwa Mbunge hapa alichangia kwenye mpango wenzetu kwenye majiji mengine wamewahi kutafuta namna bora zaidi ya kuhakikisha majiji haya yanakuwa na miundombinu ya uhakika na uongozi ambao unaweza kusaidia maisha ya wakazi wa jiji lile kuwa maisha yanayoendana na maeneo mengine. Ziko nchi zimetengeneza Wizara za masuala ya jiji, ziko nchi zimetengeneza mamlaka ya kusimamia jiji. Niombe Serikali iiangalie Dar es Salaam na maeneo yanayozunguka maana jiji hili ndiyo linazalisha zaidi ya asilimia 70 ya mapato ya nchi yetu iweze kutengeneza mfumo ambao utasaidia kuboresha makazi ya wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Zungu hapa amesema, leo Dar es Salaam tunavyozungumza mvua zimenyesha, Dar es Salaam haipitiki, maisha ya wananchi yamekuwa ya tabu. Leo mtu kutoka kule Mzinga Magore, Bomba Mbili Majohe, Mpemba Majohe, Mkolemba anatumia zaidi ya shilingi 1,000 kupanda bajaji imfikishe kwenye eneo la kupata usafiri kwenda mjini.

Mheshimiwa Naibu Spika, nami nitaungana na wenzangu kuendelea kuisii Serikali iangalie umuhimu wa Mradi wa Dar es Salaam wa Metropolitan Development Project (DMDP II). Nami niseme tu pamoja na kuungana na wenzangu kwamba tunapozungumza kwenye bajeti ya TAMISEMI, dada yetu Mheshimiwa Ummy Mwalimu ni mchapakazi, hilo hatuna shaka na ana Manaibu Waziri wazuri lakini wenzetu hawa ni watumiaji wa bajeti kama sisi wengine tujipange vizuri kwenye kuishauri Serikali jinsi ya kupata fedha kwenye bajeti ya Wizara ya Fedha na bajeti kuu ya Taifa ili miundombinu ya Dar es Salaam iweze kuboreka, wananchi wale waendelee kuzalisha uchumi na mapato ya Taifa hili yazidi kuboreka kupitia miundombinu ya barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge katika kipindi cha kampeni na katika michango yetu mingi humu ndani tunasema kwamba Serikali imefanya kazi kubwa sana kwenye sekta ya afya, elimu na sekta nyingine zinazosimamiwa na Wizara ya TAMISEMI. Zimejengwa zahanati nyingi, vituo vya afya vingi, hospitali za wilaya, shule Kongwe zimekarabatiwa na kazi ya ujenzi wa miundombinu ya elimu na afya inaendelea. Naomba kusema jambo moja hasa katika nyakati hizi ambapo miradi yetu mingi hii inatekelezwa kwa force account, kazi hizi zimefanywa na Wakurugenzi na watendaji wa halmashauri zetu nchi nzima. Sikatai, yawezekana wako watendaji wachache wenye upungufu lakini wako watendaji wengi wanaofanya kazi nzuri ya ujenzi wa Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge na Serikali, nawaomba; Waheshimiwa Wabunge ni Wajumbe wa Kamati za Fedha na Utawala kwenye Halmashauri zetu; na kamati hizi ndiyo Mamlaka ya Nidhamu kwa watumishi wote ndani ya Halmashauri. Nawaomba sana, mnyonge mnyongeni, haki yake mpeni. Wale watumishi wenye upungufu tuwachukulie hatua kwa mujibu wa Kanuni za Utumishi wa Umma na Sheria ya Utumishi wa Umma; na wale wanaofanya vizuri tuwapongeze. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tusimbebeshe Waziri wa TAMISEMI mzigo wa kuwa disciplinary authoriry ya mpaka Mtendaji wa Kata majukumu ambayo ni ya kwetu kule Halmashauri. Tusigueze Bunge hili ikawa ni sehemu ya kuja kusulubu watu ambao bahati mbaya wengine hawana uwezo wa kuja kujitetea.

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali iendelee kusimamia nidhamu ya watumishi, lakini na sisi tuwaangalie tuwaangalie wenzetu amabo ni wadau wenzetu…

MHE. MUSSA A. ZUNGU: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

T A A R I F A

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Jerry Silaa kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Mussa Azzan Zungu.

MHE. MUSSA A. ZUNGU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumpa taarifa msemaji, lakini kwanza nampongeza kwa alivyoanza. Ila naomba amalizie kwa kusema Dar es Salaam isiwe mamlaka, iwe na Wizara ya kuiendesha Dar es Salaam. (Kicheko/Makofi)

NAIBU SPIKA: Sasa unaipokea hiyo taarifa ambayo imekuja kwa namna ya wazo jipya! (Kicheko)

MHE. JERRY W. SILAA Mheshimiwa Naibu Spika, naipokea kwa mikono miwili; na ametujenga, ndiyo maana nikasema iko Miji ilichukua mbinu tofauti hili Serikali iangalie maeneo haya, kwa maana ya Wizara, kama ni Dar es Salaam Metropolitan Authority ili tupate mamlaka nzuri ya kusimamia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naomba kuwasilisha, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji
MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi kuchangia katika hotuba hii ya bajeti ya Wizara ya Maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, niungane na wenzangu, kwanza kipekee kuipongeza Wizara, Mheshimiwa Waziri Jumaa Aweso; Naibu Waziri wake, Mheshimiwa Mhandisi Maryprisca Mahundi na watendaji wote wa Wizara wakiongozwa na Katibu Mkuu, Eng. Sanga na mwanamama machachari Naibu Katibu Mkuu, Eng. Nadhifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lazima tuseme kwenye Wizara hii kazi kubwa imefanyika. Serikali imefanya kazi kubwa ya kufanya utambazaji wa maji kwenye nchi yetu. Na wote mmesikia kwenye hotuba kwamba malengo ya kusambaza maji vijijini kwa asilimia 85 kufikia 2025 mpaka kufikia mwezi Machi tayari asilimia 72.3 maji yamesambazwa. Lakini malengo ya kusambaza maji mijini tumefikia asilimia 84; tunaipongeza sana Wizara ya Maji kwa kazi kubwa waliyoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kipekee niipongeze Serikali, zaidi ya shilingi bilioni 200 zimewekezwa katika kazi ya kusambaza maji safi na salama kwenye Mkoa wa Dar es Salaam. Lakini iko miradi mingi mikubwa; upo ule mradi wa Arusha, zaidi ya shilingi bilioni 520; upo Mradi mkubwa wa Tabora – Igunga – Nzega, zaidi ya bilioni 600; lakini iko miradi ile ya miji 28 ya zaidi ya Dola za Kimarekani milioni 500, kazi kubwa sana imefanyika kwenye sekta ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye wanufaikaji wa miradi hii na Jimbo la Ukonga ni wanufaikaji. Sisi kwa miaka yote tulikuwa tukipata maji toka Ruvu chini, maji ambayo yalikuwa mpaka yapite katikati ya Jiji la Dar es Salaam yapandishe Mlima wa Magereza – pale Magereza kulikuwa na mashine ya maji – yaje mpaka Gongo la Mboto – pale Gongo la Mboto kulikuwa na mashine ya maji, na mtafahamu Jimbo la Ukonga lina asili ya Milima ya Pugu mpaka Milima ya Kisarawe kwa kaka yangu, Mheshimiwa Selemani Jafo. Na kwa kipindi kirefu tokea miaka tisini hatukuwahi kupata maji safi na salama ya bomba. Katika uwekezaji huu wa Serikali, Mradi wa Maji wa Ruvu Juu na Ruvu Chini imeboreshwa na uzalishaji umeongezeka kwa kiasi kikubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini maji haya yalipofika Kibamba ukabuniwa mradi mwingine ukatoa maji Kibamba mpaka Kisarawe na Kisarawe imejengwa njia ya maji mpaka Pugu limejengwa tanki kubwa la lita milioni mbili na tayari mradi ule umezinduliwa, na hivi ninavyozungumza Jimbo la Ukonga linapata maji safi na salama.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutoa shukrani kwa niaba ya wananchi wa Ukonga, Mheshimiwa Waziri alifika, alikuja na Mheshimiwa Rais akiwa Makamu wa Rais kuzindua mradi ule; tunawashukuru sana. Na DAWASA kupitia Mhandisi Cyprian Lwemeja, wanafanya kazi kubwa ya kuendelea kusambaza maji yale kwa uwezo wao wa ndani. Tayari kazi ya transmission imekamilika na hivi wmaeshapata fedha wanaanza kazi ya distribution. Sisi tunaamini katika malengo ya 2025 tutakuwa wa kwanza kuyafikia kabla ya wakati na maji yatasambaa kwenye Jimbo la Ukonga. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukisoma hotuba ya Mheshimiwa Waziri, mpaka kufikia mwezi huu Aprili, fedha za maendeleo zilizopokelewa ni asilimia 54.1. Katika fedha zilizopangwa za Mwaka wa Fedha 2020/2021 mpaka kufikia mwezi huu wa Aprili ni asilimia 54.1 tu ndiyo zimepokelewa na Wizara. Imebaki miezi miwili, siamini kwamba kufikia mwisho wa bajeti hii Wizara ya Maji itakuwa imepata fedha zote za maendeleo.

Mheshimiwa Naibu Spika, na Wizara hii isipopata fedha maana yake maombi yote uliyoyasikia hapa Waheshimiwa Wabunge wakiyaomba, miradi yote ambayo umeisikia inaendelea kwenye majimbo yote ndani ya Bunge hili haitakamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hawa wenzetu wa Wizara ya Maji ni waombaji kama sisi tunavyoomba, inapokuja hapa bajeti kuu ya Serikali naomba tusimame tuseme Wizara hii ipatiwe fedha za kutosha. Pia isipatiwe tu fedha kwa maana ya kuzitenga kwenye bajeti lakini na fedha zenyewe zipelekwe tena kwa wakati ili miradi ya kuwasambazia maji Watanzania iweze kufanyika kwa ufanisi mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nirudie pia ama kuongezea pale alipochangia Mheshimiwa Anne Kilango Malechela, miradi ya maji hasa vijijini ukiondoa hii ya mijini ambayo inasimamiwa na Mamlaka ni kweli inagharimu fedha nyingi. Niungane na mama yangu Mheshimiwa Anne Kilango, Wizara ya Maji, RUWASA, Menejimenti ya RUWASA na DG yupo hapa nadhani anasikia, Clement anafanya kazi nzuri kujenga taasisi hii mpya na changa iliyoanzishwa muda mfupi uliopita, mjitahidi mtengeneze mfumo utakaofanya wale akina Ali Mabomba waliokuwa Same waweze kupatikana kusimamia miradi hii nchi nzima. Itakuwa ni kichekesho kutengeneza miradi ya thamani kubwa ya mabilioni ya shilingi lakini kuiacha kwenye mikono ya watu ambao hawana utaalamu, lakini hawana usimamizi wa kitaalamu chini ya taasisi yetu hii ya RUWASA.Ni vyema tukajipange na hili litawezekana kama Wizara hii itakuwa na fedha za kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikiendelea kusisitiza RUWASA kutengeneza utaratibu wa kuwa na wataalam wa kutosha kusimamia miradi lakini nitaendelea kuliomba Bunge lako na tutakutana tena hapa kwenye bajeti kuu ya Serikali kuendelea kuitaka na kuishauri Serikali itenge fedha za kutosha kwa ajili ya miradi ya maji ili utendaji huu uliotukuka tunaouona wa Waziri wetu Mheshimiwa Jumaa Aweso uweze kwenda kwa vitendo akiwa na fedha za kulipa makandarasi wanaofanya kazi kule chini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa nafasi hii, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari
MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kunipa nafasi kuchangia hotuba ya bajeti ya Wizara ya Mawasiliano, Teknolojia ya Habari ya mwaka wa fedha 2021/2022.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nichukue fursa hii kuipongeza sana Serikali kwa kugundua mchango wa sekta ya TEKNOHAMA katika uchumi wa Taifa letu. Kwa kuunda Wizara hii, ni matumaini yetu sasa kwamba Serikali itatengeneza utaratibu mzuri ili sekta hii iweze kutoa mchango chanya kwenye uchumi wa Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye hotuba ya Waziri ameainisha takwimu za watumiaji ambao mpaka hivi tunavyozungumza wanatumia line za simu. Mpaka kufikia anasoma hotuba hapa leo wapo watumiaji 53,063,000 wanaotumia line za simu. Kuna Watanzania 29,071,000 wanaotumia mtandao wa internet lakini zaidi ya Watanzania 32,000,000 wanatumia miamala ya fedha kwa maana ya fedha za kwenye simu. Ukiangalia takwimu zote hizi za mamilioni utagundua kwamba tayari Tanzania ipo na wenzetu wa duniani, kwamba sasa tumehama toka kwenye mifumo tuliyoizoea (traditional systems) kwenda kwenye mifumo ya kimtandao kwa maana ya online systems, tutakutana kwenye bajeti kuu ya Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka hivi tunavyozungumza wenzetu wa Mamlaka ya Mapato wanao Watanzania wenye Tax Identification Number kwa maana ya TIN Number milioni mbili na laki tano. Ukiangalia takwimu hizi za online na takwimu zetu zile tulizozizoea za makaratasi, utakubaliana na mimi kwamba tayari dunia imehama na ni wajibu wetu kama Watanzania kuwekeza nguvu kubwa zaidi ya kutumia advancement hii ya teknolojia kuendesha uchumi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nitachangia kwenye maeneo matatu. Eneo la kwanza, tumeona kwenye Finance Act nyingi kwamba wenzetu wa Serikali wanatumia takwimu hizi za wingi wa watumiaji wa simu, internet, mitandao ya fedha kwenye simu kama ndiyo mtaji na kuweka makodi mengi ambayo yanawaumiza watanzania. Wanasahau kwamba takwimu hizi zinapaswa kutumika kama platform ya kutengeneza system nzuri zaidi ya kuwa kwanza na tija kwenye matumizi yenyewe ya mitandao, lakini pili kama kuna ukusanyaji wa mapato, kukusanya mapato stahiki kwa wale ambao wamebeba ama wale ambao ndiyo online platform prayers kwa maana wale ambao ndiyo hasa wamiliki wa mitandao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzetu wa Ufaransa ndiyo walikuwa wa kwanza (pioneers) wa kuanzisha Kodi ya Mitandao, kwa maana ya Digital Service Tax (DST). Waliseti asilimia tatu, kwa mtu yeyote anayefanya biashara ya mtandao lakini biashara hiyo inafanyika na wananchi wa Ufaransa. Tukisema watu hawa ni watu kama YouTube, Facebook, Instagram, Amazon na watu wote wale ambao ndiyo wenye biashara zao za mtandao. Wenzetu wakenya kwenye Finance Act ya mwaka 2019 wame-introduce Digital Service Tax.. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Nayasema haya kwa sababu tutakuja kukutana kwenye Bajeti Kuu ya Taifa kuiomba na kuishauri Serikali kuanza kuondoa fikra kwenye kumbana Mtanzania wa kawaida anayetumia mtandao na kupeleka fikra kwenda kuwabana wale wanaopata pesa kupitia mtandao. Tukitumia takwimu hizi vizuri na tukiweza kutengeneza mifumo mizuri ya kuhakikisha biashara zinazofanyika duniani kupitia mitandao ambazo wateja na watumiaji wake ni wananchi wetu wa Tanzania hawa tunaowataja milioni 53, milioni 29, milioni 32 tuna uwezo kwanza kumsaidia Mtanzania kupata mawasiliano mazuri zaidi lakini kuiongezea Serikali mapato bila kumuumiza Mtanzania wa kawaida anayetumia mtandao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi tunavyozungumza content nyingi za habari zinapita kupitia mitandao. Hata Waheshimiwa Wabunge humu ndani michango wanayoitoa, kazi wanazozifanya asilimia 90 zinapita kwenye mitandao na siyo kwenye traditional media systems. Hapa tunapozungumza TCRA waje watuambie wakati tunahitimisha hotuba hii ya bajeti, hatuna aggregator wa YouTube ndani ya nchi yetu, wote hawa unaowasikia wanaotusaidia na sisi, ukisikia Millard Ayo YouTube Channel wanafanya aggregation yao ya content wanayoi-air kwenye online platforms kupitia nchi nyingine. Wapo wanaofanya Kenya, Afrika ya Kusini na wapo wengine vijana wa Kitanzania wanaofanya Marekani na hata kulipwa inabidi walipwe kwa accounts za Marekani. Hii si tu inatupunguzia mapato lakini inatengeneza urasimu mkubwa kwa vijana wetu ambao wangeweza kupata tija kubwa zaidi kwenye sekta hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini eneo la pili, nizungumzie maeneo ya Pay TV. Zipo leseni TCRA wanazitoa za Pay TV ambapo moja kati ya TV hizi ni kama Wasafi. Moja kati ya masharti wanayopewa kwanza hawaruhusiwi kutoa any live coverage including coverage za matamasha yao ya muziki wanayoifanya. Leo tuna vijana wasanii wanafanya kazi kubwa, wametoa ajira kwa vijana wengi, lakini matamasha hata ya kwao yenyewe wanashindwa kuyaonyesha live kwa masharti wanayopewa na TCRA. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu pekee kinachoruhusiwa kuonyeshwa live ni mpira wa miguu. Sasa wakati tunaendelea kuuenzi mpira kama ajira kwa vijana tukumbuke vilevile na tasnia ya sanaa ya muziki na yenyewe ni ajira kwa vijana wetu. Inapoonyeshwa live Pay TV zinazoonekana kwenye mitandao ya DSTV zinaonekana Afrika na dunia nzima, wataitangaza nchi yetu na tija tutaiona hata kwenye utalii wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapotengeneza masharti haya tuangalie Wizara hii kwa suala mtambuka kwa maana inagusa maeneo yote ya uchumi wa Taifa hili. Tunapokuwa na mifumo ambayo utekelezaji wake unabana fursa badala ya kutanua fursa tunawaumiza wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la mwisho niungane na wewe na wachangiaji waliotangulia na Mwenyekiti wa Kamati ya Miundombinu ni shirika letu la TTCL, kama kweli Serikali inataka kufanya biashara ifanye biashara. Hatuwezi kuwa na Shirika ambalo fedha haziendi, tumechukua deni la Mkongo tumepelekea Shirika kulipa tabu, sisi wenyewe Serikali ni wateja wa Shirika hatulipi madeni yetu, naomba tuweze kutengeneza seriousness katika kusaidia Shirika letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wengine itafika wakati tutalichukulia hili suala hili kidogo personal kwa sababu tushukuru Serikali tunaye Mkurugenzi kijana na masuala ya TEKNOHAMA haya huwezi kuyatofautisha sana na vijana hata mtaalam wangu Mheshimiwa Getere angekuwepo angesema, ni masuala ambayo yanaendana na vijana. Sasa tumuunge mkono, tusiwe sisi wenyewe Serikali tunataka tufanye biashara, lakini sisi wenyewe tukidaiwa madeni hatulipi, sisi wenyewe hatuwekezi na ndiyo wa kwanza kuwasema kwamba hawatekelezi majukumu yao ipasavyo. Kwa hiyo, Waziri utusaidie na useme humu Bungeni maana mengine inawezekana na wewe yapo nje ya uwezo wako kwa maana ya Wizara yako inatakiwa iwezeshwe, Wabunge tulisaidie Shirika letu la TTCL liweze kupewa uwekezaji wa kutosha liweze kushindana kwenye ushindani wa kibiashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kurudia tena kwamba tunavyotengeneza masharti yanayosimamia tasnia hii ya mitandao, basi tutengeneze masharti ambayo yanaendana na masuala mengine ya kidunia.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. Ahsante sana kwa kunipa nafasi. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi kuchangia bajeti hii ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa.

Mheshimiwa Spika, kwanza nichukue fursa hii kuwapongeza Mheshimiwa Balozi Libelata Rutageruka Mulamula kwa uteuzi wake wa kuwa Waziri wa Wizara hii, lakini na Mheshimiwa Naibu Waziri, Mheshimiwa Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk.

Mheshimiwa Spika, nichukue fursa hii vilevile kuwapongeza Watendaji Wakuu wa wizara, kaka yangu na rafiki yangu Balozi Joseph Edward Sokoine na Mheshimiwa Balozi Fatma Mohammed Rajabu kwa kuteuliwa kuwa Naibu Katibu Mkuu wa Wizara hii ya Mambo ya Nje. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini nichukue fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kuteua wanadiplomasia wabobezi kwenye Wizara hii, lakini kwa kuzingatia si tu mgawanyiko wa Muungano wa nchi yetu lakini vilevile na jinsia kwenye teuzi zake. (Makofi)

Mimi naamini kama wachangiaji wengine kwamba ubobezi wa wana diplomasia hawa kwenye Wizara hii utaleta matokeo chanya kwenye utendaji wa kazi wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa na kazi yetu sisi ni kuwaunga mkono, kuwatia moyo na kuendelea kuwasadia kuhimiza Serikali kutenga fedha za kutosha kama walivyoomba kwenye bajeti yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimeisikiliza kwa makini hotuba ya Mheshimiwa Waziri na mimi niungane na wenzangu kupongeza kazi kubwa Wizara hii inayofanya kwenye eneo la economic diplomacy, wamefanya kazi kubwa, miradi mingi inatekelezwa na Wizara hii inaratibu na yapo mambo mengi baadhi ya Wabunge walioanza kuchangia wametoa wito, namie nitoe wito kwa Wizara hii kuongeza nguvu kwa kuisemea na kuitangaza nchi yetu. Na mimi naamini kama Serikali itachukua ushauri wa Mheshimiwa Mbunge Balozi Pindi Hazara Chana na kufungua Balozi nyingi zaidi, lakini si tu kufungua Balozi na kuziweka strategic, umetolewa mfano mzuri sana hapa, leo watanzania wengi wanakwenda China kufanya biashara, lakini ukimuuliza mtanzania wa kawaida kama amewahi kufika ubalozini Beijing hata hafahamu ni eneo gani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Watanzania wangi wanafanya biashara kweye Miji ya Guangzhou, Shenzhen, Yuan na hata kama tutashindwa kupata Balozi mdogo basi hata ukipata Honorary Consular maslahi ya Watanzania kibiashara yatalindwa kwenye maeneo yale. (makofi)

Mheshimiwa Spika, ningeomba Wizara imefanya kazi kubwa kwenye utalii, lakini iongeze kazi kubwa ya kutangaza utalii kwenye balozi zetu kwa sababu utalii ni moja ya kati ya sekta ambazo inategemewa sana kwenye uchumi wetu kutuingizia pato la kigeni.

Mheshimiwa Spika, katika mchango wangu ningeomba kuchangia kwenye eneo la itifaki, ukurasa wa 87 wa hotuba ya Mheshimiwa Waziri. Na ningemuomba Waziri pamoja na ubobezi wao wa diplomasia nimrudishe kwenye sheria, kwenye Katiba ambayo ndio sheria mama ya nchi yetu. Nimuombe Waziri nimrejeshe kwenye Ibara ya 4(2) ya Katiba yetu ambayo inaeleza utawala wa nchi yetu ulivyogawanyika katika mihimili yake mitatu; kwa maana ya Serikali, Bunge na Mahakama. (Makofi)

Lakini nimrudishe kwenye Ibara ya 62 ya Katiba yetu ambayo inalitaja Bunge na kuelezea kazi na mamlaka ya Bunge letu. Lakini Ibara ya 66 inayowaelezea Waheshimiwa Wabunge, Ibara ya 84 inayomwelezea Spika wa Bunge letu hili la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Lakini na Ibara ya 85 inayomwelezea Naibu Spika na Ibara ya 105 inayoelezea Baraza la Wawakilishi la Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa nini naeleza ibara hizi? Kumekuwa na dhana na wenzetu wanaosimama itifaki ya shughuli zetu za kitaifa. Unakwenda kwenye shughuli ambayo Mheshimiwa Spika amehudhuria, unafanyika utambulisho Mheshimiwa Spika hatambulishwi. Si tu kutokumtambulisha ni fedheha kwake yeye binafsi, maana inawezekana Spika wetu Job Ndugai wote mnafahamu ni mtu rahim na mtu ambaye hana makuu. Lakini usipomtambulisha Spika maana yake umeamua wewe mwenyewe kuandika Katiba yako mpya na kuondoa Bunge ambalo linawakiwalisha wananchi wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini haiishii kwa Spika, zipo shughuli nyingi wanakwenda Waheshimiwa Wabunge na Waheshimiwa Wabunge wakienda vilevile tusiangalie wao kwa majina yao, wanakwenda kuwawakilisha wananchi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwenye shughuli zile. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ziko shughuli anakwenda Mheshimiwa Naibu Spika, ziko shughuli wanakwenda Wenyeviti wa Kamati za Kudumu za Bunge. Ziko baadhi ya shughuli ambazo uratibu wa itifaki una-fail na Waheshimiwa Wabunge wanakuwa kama ma-gate crasher kwenye shughuli zile. Kuingia tabu mpaka watu waulizane wee mtu asimame pale mlangoni kila anayepita anakushangaa, bwana vipi! Tupo tumekuja kwenye shughuli. Kila anayepita anakuonea imani, wamekuona? Enhee wameniona wanashughulikia. Mpaka itokee hisani ama kiongozi wa itifaki afike aseme basi andika jina lako uingie. Lakini ndani ya shughuli ile utambulisho utatambulishwa sisemi kwa sababu Babu Tale hapa hayupo mpaka wasanii watatambulishwa, Mheshimiwa Mbunge hajatambulishwa.

Sasa hatusemi haya kwa maana tu ya kusema labda Wabunge wanataka makuu, hapana. Nayasema haya kwa kuwa Katiba inatambua nafasi hizi. Shughuli inapoandaliwa, viongozi wanapoalikwa, wanapofika wapate heshima na stahiki inayostahili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikiri Mheshimiwa Waziri ameliona, Mheshimiwa Naibu Waziri ameliona na Mheshimiwa katibu Mkuu ameanza kulifanyia kazi, ni Mabalozi wazuri wanafanya kazi vizuri sana. Nalisema kuweka kumbukumbu sahihi kwa kuwa nawaamini sana viongozi hawa niliowapongeza mwanzo wa mchango wangu. Kulikuwa na dhana kwamba shughuli hii inaandaliwa na Ofisi ya Waziri Mkuu, shughuli hii inaandaliwa na TPDC, shughuli hii inaandaliwa na TANESCO, ukisoma vizuri utaratibu wa shughuli za Kitaifa na za Kimataifa huwezo ukaondoa majukumu ya Idara ya Itifaki ya Wizara ya Mambo ya Nje katika kusimamia itifaki ya shughuli zile. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nimuombe Waziri bahati nzuri umekuja na mzee na nilidhani atatoka baada ya kutambulishwa, lakini amebaki. Kwa heshima yake, twende kwa utaratibu wa kushauri, naamini ukija kuhitimisha hotuba yako utahitimisha vizuri na kunyoosha itifaki ya shughuli zetu.

Mheshimiwa Spika, na nikuambie kwa dhati ya moyo wangu, ikitokea tena Spika wangu wa Bunge hili aidha kwa makusudi ama kwa bahati mbaya kwenye shughuli yoyote hakutambulishwa au hakupewa itifaki inayostahili Mheshimiwa Waziri utakutana na jambo linaitwa Azimio la Bunge na wala usitafute mchawi, mimi nimeamua kununua hiyo kesi. Lakini sina shaka na wewe, sina shaka na Naibu Waziri wako na watendaji wako, naamini mtajipanga vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, yako hayo na mengine madogo madogo tu, hata Rais wetu anaenda kwenye shughuli haijulikani gari linasimama wapi, anashuka watu wamejipanga upande huu anashukia upande mwingine. Ni majukumu yenu, chukueni role yenu ya itifaki na msikubali mtu yeyote akachukua majukumu ambayo sio ya kwake kwa kuwa majukumu ya itifaki ni majukumu yenu chini ya Wizara yenu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi naamini haya yakifanyiwa kazi na yale ambayo wachangiaji wenzangu wamechangia, Wizara hii ikawezeshwa kwa fedha sit u kutengewa fedha lakini kuhakikisha fedha zinapelekwa hasa katika uwekezaji wa majengo ya ubalozi kwenye nchi ambazo tuna uwakilishi na kufungua Balozi nyingine za ziada. Wizara hii ikija hapa mwakani itakuja na mafanikio makubwa kuliko ilivyofanya hivi sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati
MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Spika, nami nakushukuru kunipa nafasi kuchangia bajeti hii ya Wizara ya Nishati. Kwanza, niungane na Wabunge wengine kuipongeza Serikali kwa kazi kubwa iliyofanya katika usambazaji wa umeme wa REA. Sisi Wabunge wa majimbo ya mijini tunanufaika na usambazaji wa umeme wa Mradi wa Peri- Urban kwenye kata zote za Jimbo la Ukonga na kazi inaendelea vizuri.

Mheshimiwa Spika, mchango wangu napenda kujikita kwenye maeneo mawili. La kwanza ni ujenzi wa LNG Plant kule Lindi.

Niipongeze Serikali na Mheshimiwa Waziri kwenye hotuba yake ukurasa wa 68 ameelezea hatua zilizofikiwa na mipango ya Serikali ya kuhakikisha ujenzi huu unakwenda kwa kasi ama mazungumzo baina ya Serikali na wawekezaji yanakamilika kwa wakati kama vile Mheshimiwa Rais wetu Samia Suluhu Hassan alivyoelekeza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niipongeze Serikali kwa kutumia timu ile iliyopata uzoefu kwenye Mradi wa Bomba la Mafuta la Uganda ama East Africa Crude Oil Pipeline kuitumia katika negotiation ya mradi huu. Niiombe Serikali ifanye kila liwezekanalo kuhakikisha mazungumzo haya yanafanyika kwa wakati, lakini katika kuzungumza huko Serikali ijitahidi sana kutotumia haraka lakini kuweka mbele maslahi mapana ya Taifa. Kwenye hotuba ya Waziri ameelezea kwamba tayari fidia ya eneo imeshafanyika sasa zile hatua zilizobaki za pre- FEDD decision, FEDD decision yenyewe lakini final investment decision na mpaka mradi uanze zifanyike kwa utaratibu mzuri ili Taifa liweze kunufaika.

Mheshimiwa Spika, vilevile naomba kuishauri Serikali wakati negotiation zinaendelea ifanye micro and macroeconomic study ili kuweza kuona mradi ule pamoja na faida zile za kifedha zitazopatikana kwenye mradi lakini faida nyingine mtambuka kwenye maeneo yale ya Lindi na Mtwara na maeneo mengine ya Taifa letu. Faida hizo ni muhimu ziweze kufahamika na kujulikana ili Serikali inapoingia kwenye mradi ule iingie kwenye jambo ambalo ukiangalia mtazamo mzima wa negotiation kwenye open book economic model haziangaliwi basi ziweze kuwa covered kwenye micro and macroeconomic study.

Mheshimiwa Spika, lakini tujifunze kwa Mozambique, wenzetu wameanza wako katika hatua nzuri sana na hivi tunavyozungumza mnafahamu vinafanyika vikao vya SADC katika kuangalia hali ya usalama ya Msumbiji. Niiombe Serikali itumie vikao hivi hivi kuweza kujifunza kwa wenzetu ili na sisi tufahamu hivi tunavyo-negotiate hatuhitaji msaada wa utaalamu maeneo mengine, hatuhitaji ushauri wa majirani zetu ili mradi huu uweze kufikiwa na Tanzania iweze kupata mapato.

Mheshimiwa Spika, kwenye huu ukurasa wa 68 mradi huu utagharimu siyo chini ya dola bilioni 30 sawa na trilioni 70 za kitanzania. Mradi huu ukianza kuzalisha mapato yanakadiriwa kuwa siyo chini ya dola bilioni 3 kama trilioni 7 kwa taifa letu. Niombe kuungana na wachangiaji wa jana akiwemo Mheshimiwa Getere kama itaipendeza Serikali akina Mheshimiwa Kalemani hawa wakipatikana wawili mmoja akahangaika na huu umeme wa REA akapatikana Kalemani mwingine kuhangaika tu na mradi huu wa gesi asilia itasaidia taifa kuweza kuongeza kasi na ufanisi katika kutekeleza mradi huu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile napenda kuchangia kama walivyosema wachangiaji wenzangu, niipongeze Waziri, Naibu Waziri na uongozi wa Wizara kwa kushirikisha Shirika la Viwango Tanzania (TBS) katika kufanya kazi adhimu ya kulinda kodi na mafuta ya nchi yetu. Ziko dhana nyingi wakati mwingine sisi wenyewe Watanzania tunapenda kujidharau na kuthamini vitu vya nje. Naomba Serikali katika jambo hili ilitilie mkazo na ilifanye kwa ufanisi.

Mheshimiwa Spika, naomba niseme Waziri wa Viwanda na Biashara ama Serikali kwa ujumla TBS iwezeshwe iweze kufanya kazi hii kwa ufanisi. Nasema hivyo maana hivi tunavyozungumza vifaa vidogo tu vya detection ya vinasaba bado TBS hawajapeleka EWURA. Wizara ya Viwanda na Biashara iko hapa, Serikali iko hapa iweze kuongeza nguvu, jukumu walilopewa ni kubwa iongeze nguvu TBS ifanye kazi hii kwa ufanisi kwanza kwa usalama wa Mtanzania lakini pili kwa usalama wa Taifa letu lakini tatu tunaamini Shirika hili ni la kizalendo na ni la Tanzania ambapo manufaa yoyote yatayopatikana yatakuwa kwa Watanzania. Serikali ifungue macho zaidi maana inawezekana Shirika hili likakwamisha mradi huu ili kuonekana tumefeli kuweza kujenga hoja maeneo mengine.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja, nakushukuru sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi kuwa mchangiaji wa kwanza kwenye hotuba hii ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 iliyowasilishwa hapa Bungeni na Waziri wa Fedha tarehe 10, Juni.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naomba kidhati kuipongeza Serikali ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kuja na bajeti iliyobeba matumaini mapya kwa Watanzania.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niongelee maeneo mawili makubwa ambayo bajeti hii imekuja na matumaini mapya. Mosi; bajeti hii imekuja kujibu lile swali ambalo Watanzania wamekuwa wakijiuliza kuhusiana na uendelezaji wa miradi yetu ya kimkakati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiisoma bajeti hii – naomba kunukuu – inasema hakuna mradi hata mmoja utakaokwama bila kusimama hata kwa mwezi mmoja. Na maneno haya yanachukua uhalali wake kwenye maneno aliyoyasema Rais wetu tarehe 06, Aprili, pale Ikulu, Dar es Salaam akiapisha Makatibu Wakuu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais alisema, naomba kunukuu;

“Tuna urithi aliyotuachia marehemu Rais wetu; miradi mikubwa miwili” – akimaanisha Mradi wa Bwawa la Nyerere na Mradi wa Standard Gauge – “na miradi mingine midogomidogo.”(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais anaendelea kusema; wanasema ukifanya vibaya kwenye urithi, Mungu anakulaani. Aliyekuachia urithi hana radhi na wewe, na Mungu atakulaani.

Mheshimiwa Naibu Spika, ingawa siyo maneno ya Mheshimiwa Rais, lakini naamini neno urithi unaweza ukaliondoa ukaweka neno wosia. Kwa maana yako maneno aliwahi kuyasema mwendazake. Naomba kunukuu;

Mheshimiwa Hayati Dkt. John Pombe Magufuli aliwahi kusema, akizungumzia miradi hii mikubwa ya kimkakati, alisema;

“Mimi ni dereva tu, lakini pia najiuliza, ikiwa siku moja Mungu atanichukua hawa wanaokuja watakuja kuyamaliza kweli?”(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni imani yangu tarehe 06, April wakati Mheshimiwa Rais anaelezea ule urithi, alikuwa anazungumzia kauli hii. Na ukisoma sentensi hizi, maneno aliyoyasema Hayati Magufuli, liko neno ikiwa siku Mungu atanichukua. Hakuelezea kwamba ikiwa atafika mwisho wa ukomo wa utawala wake kwa mujibu wa Katiba; ni maneno mazito sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ndiyo maana nasema bajeti hii imekuja kujibu kiu ya Watanzania, imekuja kujibu wosia aliotuachia Hayati Magufuli na imekuja kutekeleza kauli ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuhakikisha miradi yote ya kimkakati inakwenda kutekelezwa na kukamilika kwa asilimia 100. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili; bajeti hii imekwenda kutoa majibu ya kero zilizosemwa hapa Bungeni na Waheshimiwa Wabunge. Ukiangalia mijadala yote, kuanzia tunajadili Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano, mjadala wa bajeti mbalimbali, siamini kuna Mbunge yeyote alisimama hapa hakuzungumzia barabara zetu zinazotekelezwa kwa kusimamiwa na TARURA. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Wabunge hapa waliongea kwa hisia kubwa. Na mimi nilikuwa mmoja wao na nilikuwa nasubiri bajeti hii niangalie Serikali imejipangaje kuongeza fedha kwa TARURA. Ukurasa wa 72 zimetengwa shilingi bilioni 322,158,000,000 kwa ajili ya barabara zetu za TARURA. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kila siku hapa hakukosi swali la Wizara ya Maji. Na hisia za Wabunge zilijionesha sana kwenye bajeti ya Wizara ya Maji. Bajeti hii imekuja kutenga fedha za kutosha kwa ajili ya kutekeleza miradi ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la afya; kwenye majimbo yetu wananchi wamejenga maboma, Serikali imeshindwa kumalizia. Pamoja na ujenzi mkubwa wa miundombinu ya afya, vituo vya afya, vifaatiba, wataalam, dawa; bajeti hii imekuja na mwarobaini wa kutatua kero hizi za afya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, yako maeneo mengi ambayo bajeti hii imeyagusa. Lakini naomba niseme; ili kufadhili miradi ya maendeleo – wataalam wa uchumi wanafahamu na Mheshimiwa Waziri wa Fedha ni mtaalam wa uchumi – ziko njia nne. Njia ya kwanza ni mikopo, ya pili ni misaada, ya tatu ni fedha zetu za ndani, na ya nne ni venture capital ama PPP ama miradi inayosajiliwa na sekta binafsi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mikopo hii tunayoikopa tukisema tutatekeleza miradi yetu kwa mikopo tunabebesha Taifa letu mzigo wa uchumi wa sasa, watoto wetu na wajukuu zetu. Leo kwenye bajeti hii deni la Taifa ni himilivu kwa mujibu wa international standards ambazo zinataka deni la nje lisizidi asilimia 50; deni la Taifa letu ni asilimia 17. Deni la nje na ndani ukichanganya kwa pamoja kwa vigezo vya kimataifa halipaswi kuvuka asilimia 70; leo sisi tuko asilimia 27, tunafanya vizuri sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini ziko nchi za majirani zetu, takwimu hizi zipo, zimekopa mpaka sasa ziko nje ya vigezo hivi. Lakini maeneo mawili salama, ukiacha eneo la misaada ambalo wote mnafahamu misaada hii inakuja na masharti, na masharti mengine ni magumu, hatuwezi hata kuyataja humu kwenye Bunge hili, tunabaki na maeneo mawili salama zaidi ya ku-finance miradi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo kwanza ni kodi zetu sisi wenyewe. Naomba ninukuu maneno ya Hayati Dkt. Magufuli aliyoyasema kule Kyela; alisema tunajenga vituo vya afya, barabara kwa fedha zetu. Alisema Tanzania inatakiwa iwe mfano kiuchumi katika dunia, yale mawazo ya kufikiri kuna mtu ataleta misaada tuyapoteze kichwani, ule ni ugonjwa mkubwa. (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Naibu Spika, Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere aliwahi kusema; Serikali isiyokusanya kodi ni Serikali ya wala rushwa. Lakini pamoja na TRA na Serikali kupambana kuongeza wigo wa kodi, mpaka sasa walipa kodi walioko kwenye tax base ya TRA ni watu milioni mbili na laki saba. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa nini? Kwa sababu tulikuwa kwenye semina pale Ijumaa; sekta kubwa ya Watanzania iko kwenye sekta isiyo rasmi. Kwa hiyo, ukisema unapanua wigo wa kodi utabaki palepale kwa watumishi, palepale kwa walimu wetu, palepale kwa wafanyakazi wetu, palepale kwa kuwaumiza wafanyakazi kwa kodi za mishahara yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini upande wa pili…

NAIBU SPIKA: Sekunde 30.

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini upande wa pili, tunao mtandao mkubwa wa watumiaji wa simu za mkononi kwa laini zisizopungua milioni 52; hawa ndi Watanzania wanaoteseka kukosa dawa. Tunayo miamala ya fedha kwa Januari mpaka Desemba, 2020 ya jumla ya trilioni 201; hapa wako wanaotuma miamala tukiwemo wale tunaotuma na ya kutolea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana Watanzania tukubaliane kugharamia bajeti yetu sisi wenyewe. Waziri wa Fedha ameupiga mwingi sana tarehe 10, ametoa hotuba nzito sana, ameupiga kama Bernard Morrison, siyo Morrion huyu, Morrison yule aliyekuwa Dar Young Africans. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza sana Serikali, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi/Vigelegele)
Azimio la Bunge la Kuridhia Itifaki ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ya Kuongeza Mamlaka ya Mahakama ya Afrika Mashariki
MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa nafasi katika kuchangia na kuliomba Bunge lako pamoja na kuunga mkono hoja ya kuridhia kuiongezea The East African Court jurisdiction ili iweze kufanya kazi ya kutoa tafsiri na kutatua migogoro itakayotokana na zile protocol ambazo wachangiaji wengi wamezitaja nami nitazitaja hapo baadaye.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niungane na wenzangu kumpongeza kwa dhati Dkt. Damas Ndumbalo, Waziri wa Sheria na Katiba kwa uwasilishaji wake mzuri wa hoja ambayo imetupa uelewa mpana wa Itifaki hii ambayo tunaenda kuiridhia. Vilevile nimpongeze mdogo wangu Keisha kwa uwasilishaji wenye ueledi mkubwa alioutoa hapa kwa niaba ya Kamati ya Bunge na Sheria ya Katiba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kupongeza; nimpongeze sana ndugu yangu Abdullah Mwinyi, maana yeye leo hakuchangia ametoa lecture na nimemwomba aandae notisi kina Kingu wangependa kuzisoma, zilete uelewa mpana zaidi na ametueleza na tumepata fursa ya kuona Wabunge wa Afrika Mashariki wenye sifa tunaowapeleka kule wanapokuja kuleta tija kwenye Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Nchi yetu ni Mwanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki kwa mujibu wa the East African Treaty tuliyotia saini mwaka 1999 na ilivyoanza rasmi mwaka 2001 kama walivyoeleza wachangiaji wengine. Article 9 ya Treaty hiyo ndiyo inayoanzisha vyombo mbalimbali vya kiutendaji, The East African Legislative Assembly, The East African Court of Justice na ukisoma article ile inaipa mamlaka mahakama hii kuweza kutafsiri mambo yanayotokana na treaty ile. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wachangiaji wote wamesema, mwaka 2004 tumeingia kwenye common customs, tumeridhia kuwa na common custom kwa maana ya custom union ya pamoja, rates za forodha na nadhani Mheshimiwa Abdullah ameelezea vizuri zaidi na ndio maana hapa tukiwa tunapitisha bajeti zile custom measures (jitihada) za Serikali za forodha zinakuwa zimeridhiwa na Nchi zote za Afrika Mashariki na sisi kama Nchi Wanachama tunatakiwa tuendane nazo kwa jinsi Mawaziri wa Fedha wa Nchi za Afrika Mashariki walivyokubaliana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2010 tumeingia kwenye common market na mwaka 2013 tumeenda kwenye single currency ambayo imeelezewa mchakato wake wa kufikia kule kwa kufanya integration ya chumi za nchi zote wanachama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kinachoombwa hapa leo ni nini? Amekisema vizuri Wakili Msomi Zainab Katimba, ni ile article 27(2) ambayo inaipa Nchi Wanachama ya ile East African Treaty tuliyoingia mwaka 1999 uwezo wa ku- extend jurisdiction ya Mahakama hii ili iweze kutoa majibu kwenye hizi protocols nyingine ambazo kabla ya kuomba ridhaa hii, masuala yote yaliyokuwa ya kimgogoro wa protocol hizi yalikuwa yanaamuliwa na Mahakama za partner state na madhara yake ni nini? Madhara yake kila Mahakama ya Nchi Wanachama itatoa tafsiri kwa kadri ya busara ya Mahakama husika kama mhimili unaojitegemea wa Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, suala moja linaweza kujitokeza kwenye nchi mbili tofauti kwa item moja ya common customs, lakini ikapata maamuzi mawili tofauti kwa Mahakama ya Nchi Wanachama na ku-set precedent mbili kwa jambo linalofanana kwa protocol moja. Kwa hiyo, kinachoombwa hapa ni nini? Kinachoombwa hapa ni jambo la kisheria ambalo lipo kwenye treaty la kutaka ku-extend jurisdiction ya Mahakama hii ya Afrika Mashariki ili sasa iwe na nguvu ya kufanya tafsiri na maamuzi wa hizi protocol tatu tulizozieleza kwa maana ya common custom, common market na monitory union na hilo nilishawishi Bunge hili lina faida kubwa katika ule uwanda mpana mzima wa ile nguvu ya kiuchumi tunayoitafuta kama Jumuiya ya Afrika Mashariki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana hata leo tulipokaa hapa Babu Tale hajakaa, tumekaa katika safu moja tu ya kutafuta ile mantiki ya kutengeneza jambo hili kwenye uwanda wake wa kisheria na Mheshimiwa Kingu amekiri kwamba kuna kiti kilikuwa wazi lakini ameshindwa kuja kukaa kwa sababu amesema yeye ameona ajikite na Ole-Lekaita kwenye uchangiaji wa mwisho yeye amejitolea kwenye suala la kupiga makofi. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunawashawishi sana Waheshimiwa Wabunge kuweza kuridhia hoja hii iliyopo mezani ili nchi yetu kama wanachama tuliyoridhia ile East African Treaty mwaka 1999, tuweze ku- extend jurisdiction ya Mahakama hii kwa faida pana ya Jumuiya yetu ya Afrika Mashariki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maneno hayo, naunga mkono hoja na nirejee tena kuomba Bunge lako liliridhie protocol hii. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru na mimi kwa kunipa nafasi ya kuchangia bajeti hii ya Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora.

Mheshimiwa Spika, Bunge lako hili linafanya kazi kwa mujibu wa Ibara ya (63) (2), (3) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambayo inaipa mamlaka na madaraka kwa niaba ya wananchi kuisimamia na kuishauri Serikali.

Mheshimiwa Spika, nimesikiliza kwa makini sana hotuba ya bajeti iliyosomwa hapa Bungeni leo na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa bajeti ya Mwaka wa Fedha 2022/2023.

Mheshimiwa Spika, nimegundua yapo mambo makubwa ambayo Serikali Awamu ya Sita chini ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan ameyafanya kwenye utumishi wa umma. Mambo haya yamefanyika katika kipindi hiki cha mwaka mmoja ambapo Serikali Awamu ya Sita imekuwa madarakani.

Mheshimiwa Spika, mwaka jana naamini si watumishi wa umma pekee lakini Watanzania wote walipata mshtuko kwa msiba wa kuondokewa na Rais wetu Dkt. John Pombe Joseph Magufuli.

Mheshimiwa Spika, kazi iliyofanywa na Serikali ya Mheshimiwa Samia kwa mwaka mmoja, naamini imeleta matumaini makubwa kwenye sekta ya Utumishi wa Umma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, yako maandiko kwenye Quran Tukufu iko sura alishushiwa Mtume Muhammad (S.A.W) Mwenyezi Mungu akitaka kumtia moyo na sura hii nitaisema hapa. Sura inasema walaak ahkirut kairulaka minaluula. Bila shaka wakati ujao utakuwa ni bora zaidi kuliko wakati uliotangulia. Serikali ya Awamu ya Sita imefanya kazi kubwa. (Makofi/Vicheko)

MHE. MOHAMED SAID ISSA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Jerry Silaa ukae kuna Wabunge wawili wamesimama hapa. Mheshimiwa Mohamed.

T A A R I F A

MHE. MOHAMED SAID ISSA: Mheshimiwa Spika, naomba kumpa taarifa mzungumzaji kwamba hii aya ambayo ameinukuu, ameinukuu vibaya. Sasa kwa mujibu wa Quran Tukufu na kwa mujibu wa dini yetu ya Kiislam ukibadilisha herufi moja, umebadilisha maana. Kwa hiyo naomba kumpa taarifa kwamba aya hii inatamkwa walal- akhiratu khairulaka minal uula. (Makofi)

SPIKA: Haya sasa, Mheshimiwa Jerry Silaa hiyo ilikuwa ni taarifa ambayo nafikiri sasa hili jambo ili likae vizuri chukua yeye alivyoinukuu halafu iseme kwa tafsiri. (Vicheko/Makofi)

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Spika, nimshukuru sana mtoa taarifa, Kiiarabu changu kidogo kimechanganyika. Kwa hiyo niombe kumbukumbu sahihi za Bunge zichukue kiarabu cha mtoa taarifa. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, kwa nini nasema wakati huu umekuwa bora kuliko wakati uliotangulia? Ni kwa mambo makubwa ambayo yamefanyika kwenye utumishi wa umma. Kwenye Hotuba ya Mheshimiwa Waziri tumeona watumishi 190,781 wamepandishwa madaraja na Mheshimiwa Waziri ametueleza hapa kwamba watumishi wengine 92,619 watapandishwa madaraja kabla ya mwezi Juni mwaka huu 2022, ni kazi kubwa sana, tunaipongeza sana Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri vile vile kwenye Hotuba yake ameeleza kwamba wako watumishi 13,495 wamepata ajira mpya, maana yake nini? Wako Watanzania 13,495 waliokuwa tegemezi na leo nao wamekuwa wanategemewa kwa kupata mishahara kupitia utumishi wa umma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wako watumishi 21,127 wamefanyiwa recategorization kwenye kada zao za utumishi. Sasa maana sahihi ya recategorization nadhani Mheshimiwa Dullo utamtafsiria Babu Talle ili aelewe kazi kubwa iliyofanywa na Serikali hii ya Awamu ya Sita. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, yako mambo Serikali imefanya, siyo kwenye Wizara hii lakini yana impact kwenye Wizara ya Utumishi wa Umma. Serikali ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan imetoa non cash bond ya trilioni mbili kwa Mfuko wa Pensheni wa PSSSF ambayo imefanya Mfuko huu kuweza kulipa pensheni kwa wakati. Jana nimezungumza na Mkurugenzi Mashimba, leo tunavyozungumza hapa wastaafu wa mwezi wa tatu tayari wanalipwa pensheni zao, ni kazi kubwa sana imefanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais alitoa agizo la kuongeza wanufaikaji wa Mfuko wa Bima ya Afya, wale wategemezi toka umri wa miaka 18 mpaka umri wa miaka
21. Hivi tunavyozungumza wako watu 77,345 ambao walikuwa wamevuka miaka 18 na ilimpasa mtumishi kama ni mtoto wake atoe pesa mfukoni kumuhudumia matibabu, leo wanahudumiwa na Mfuko wa Bima ya Afya na yenyewe ni jambo kubwa kwenye utumishi wa umma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, yako mambo mengi kwa sababu ya muda niseme tu, Mheshimiwa Rais kwa kuthibitisha mapenzi yake na watumishi wa umma wa nchi hii amemteua mtu bingwa kabisa, mwanamke aliyehudumu ndani ya Bunge hili kwa muda mrefu kuliko akinamama wengin,e amekuwa Mbunge wa Viti Maalum lakini amekuwa Mbunge mbobezi wa Jimbo la Peramiho. Amepita Wizara ya Elimu anajua matatizo ya watumishi Walimu. Amekuwa Chief Whip hapa Bungeni na tumeona wote kazi yake. Amekuwa mjumbe wa Kamati Kuu ya Chama cha Mapinduzi, siyo mwingine ni binti wa Katekista wa Peramiho, Mheshimiwa Jenista Joakim Magigi Mhagama ambaye watu wa namna hii ndiyo wale King Kiba (Ally Kiba) aliwaimba kwenye kibao chake cha utu. Pamoja na upole na uzuri wake lakini amejaliwa utu na utulivu wa hali ya juu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Serikali imetangaza ajira mpya 32,604. Nimwombe Mheshimiwa Waziri, niiombe Serikali ajira hizi ziende kuajiriwa kwa haki. Ningetamani sana ajira hizi 32,604 kama vile zigawanywe kama zile pesa za TARURA kila Jimbo lingepata. Nafahamu ziko sheria za Utumishi wa Umma, nia yetu ni kuona kwamba ajira hizi zikitoka maana nadhani kila Mheshimiwa Mbunge hapa ana meseji ya ajira hizi za 32,000. Ni ombi langu, ama ni ushauri wangu kwa Serikali ajira hizi zikitoka tuzione zimetapakaa nchi nzima kwa usawa. Tuone kwenye Majimbo yetu kama kweli ajira 32,604 basi kila Jimbo takribani watu 100 wawe wamepata ajira. Ikifanyika hivyo italeta usawa kwa Taifa, italeta uhimilivu kwa Taifa na itaondoa ile kero ya unemployment kwetu sisi sote kwa umoja wake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho, nilipita Tabora tarehe 12 Aprili nilikutana na mzee Ramadhani Ally Mkwande, yeye ni mstaafu wa TTCL. TTCL ilikuwa na mkataba na NSSF kulipa pensheni za watumishi wake na wao ni moja kati ya wale watumishi ambao bado wanalipwa shilingi 50,000 kwa mwezi, aliniomba nije kusema Bungeni na nimeona nimtendee haki. Tunaiomba Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma ijaribu ku-standardize watumishi wote wafike kile kiwango cha shilingi 100,000 wanachopata pensioners wengine ili na wenyewe waweze kuendesha maisha yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, labda la mwisho la kusema, niliongea kidogo pale kwenye Mfuko wa PSSSF kwenye ile bond ya two trillion aliyoitoa Mheshimiwa Rais kupitia Serikali yake. Niseme tu Kamati ambayo Bunge lako limekasimia kazi ya uwekezaji inasimamia Mifuko hii, kazi kubwa imefanyika lazima tuseme. Kazi kubwa imefanywa na Serikali kuweza kutengeneza liquidity kwenye Mifuko hii na kazi kubwa inaendelea kufanyika. Nikuombe na niliombe Bunge lako Tukufu, tuendelee kuwatia moyo, tuendelee kuikumbusha Serikali kwa adabu, lakini mwisho wa siku naamini pensioners wa nchi hii wataendelea kupata pensheni zao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)