Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Simon Songe Lusengekile (12 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Spika, nianze kwa kukushukuru kwa kunipa nafasi kuchangia hotuba ya Mheshimiwa Rais. Pia nimshukuru Mungu sana kwa nafasi hii aliyotupatia ya kuwa mahali hapa leo. Kipekee nikishukuru Chama changu cha Mapinduzi pamoja na wananchi wa Jimbo letu la Busega kwa kuniamini na kunichagua kuwa mwakilishi wao mahali hapa.

Mheshimiwa Spika, 2015 nilibahatika kufuatilia hotuba ya Mheshimiwa Rais wakati akizindua Bunge la Kumi na Moja, tarehe 20 Novemba, 2015. Aliyoyasema nilianza kufikiri kwamba yanaenda kuwezekana vipi, lakini nirudishe shukrani nyingi sana kwa mapinduzi makubwa ya maendeleo aliyotupatia Mheshimiwa Rais kwa kipindi hiki cha miaka mitano iliyopita. Ni Imani yangu kubwa kwamba katika hii miaka mitano kupitia hotuba yake ya tarehe 13 Novemba, 2020 ambayo ilitoa mwelekeo wa nchi yetu yapo maeneo machache naomba nami nichangie.

Mheshimiwa Spika, kuna suala toka asubuhi linaendelea kujadiliwa; habari ya TARURA. TARURA ni pasua kichwa, TARURA ni shida mpaka sasa barabara nyingi vijijini zimekatika. Pia kutokuwepo kwa barabara hizi za vijijini kumesababisha sehemu ya uchumi wa wananchi wetu kushuka kwa sababu hawawezi sasa kupeleka hata mazao yao kwenda kutafuta sehemu ambako kuna masoko, madalali wamekuwa wengi wa bei ya chini kwa sababu ya shida ya barabara ambazo ziko kwenye vijiji ambavyo sisi tunatoka.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano ukiangalia kuna wakati hata hili zao la pamba kwetu kule Usukumani ambapo wananchi wengi wanalima, inafikia sehemu barabara ni ya shida watu wa pikipiki wanakwenda kununua pamba kwa bei ya chini sana, muda mwingine hata nusu ya bei ambayo ni halisia kwa sababu ya kutokuwepo barabara sehemu husika. Tunapotaka sasa kuendeleza uchumi wa wananchi wetu mmoja mmoja lazima tuwatengenezee mazingira mazuri ili wananchi hawa sasa waweze kusafirisha mazao yao ya biashara kwenda sehemu nyingine kwa ajili ya kupata bei iliyo salama.

Mheshimiwa Spika, nataka pia nichangie kidogo eneo la kilimo. Mimi ni muumini sana wa uwekezaji katika sekta ambazo ni productive kwa nchi yetu. Tunapokuwa tunazungumza habari ya ajira milioni nane, ni lazima tufikiri kuelekeza baadhi ya ajira katika sehemu ambazo ni productive kwa nchi yetu ikiwemo na kilimo.

Mheshimiwa Spika, ukienda kwenye halmashauri zetu, halmashauri zilizo nyingi zina shida ya watumishi, hasa Maafisa Ugani. Wananchi wetu wengi hawapati fursa ya kufundishwa na hawa Maafisa Ugani kwa sababu hawapo kila sehemu ni shida. Hii ni sekta ambayo tungeweza kuielekezea watumishi wengi wangeweza kuwasaidia wananchi wetu ambao wanalima kwa kutumia akili zao zilezile ambazo Mheshimiwa Mbunge wa Mbogwe alikuwa anajaribu kugusia.

Kwa hiyo, mimi niseme na niombe, tunapokuwa tunaangalia suala la ajira, lazima pia tuangalie eneo hili ili tuweze kuajiri watu wengi waende wakawasaidie wananchi wetu katika suala zima la kilimo na kilimo kiwe chenye tija na tutakapopata malighafi yetu basi itatumika kwa ajili ya viwanda vyetu vya ndani.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ambalo nataka kulizungumzia ni viwanda. Eneo hili tukitaka tufanye vizuri ni lazima tuhakikishe kwamba tunapata viwanda vyetu vya ndani ambavyo vinatengeneza bidhaa mpaka mwisho. Kama ni pamba basi tutengeneze bidhaa inayotokana na pamba mpaka mwisho tupate nguo ili tuweze ku-export nguo kwenda nje ya nchi, zao ambalo tayari limekamilika kwa kutumia bidhaa zetu za ndani.

Mheshimiwa Spika, pia nataka kuongelea habari ya uvuvi, Mbunge wa Ukerewe amezungumza kidogo. Eneo hili bado lina shida, tozo ni nyingi sana kwa wananchi wetu ambao wanashughulika katika suala zima la uvuvi. Tozo ni nyingi, kuna leseni ya mtumbwi, TASAC Sh.70,000 wananchi wetu wanalipa lakini pia kuna leseni za halmashauri, kuna leseni ya mtumbwi na kuna shilingi 20,000 leseni ya mvuvi mmoja mmoja. Haya maeneo wananchi wetu wanayalalamikia sana kwa sababu tozo zimekuwa nyingi na wanashindwa kuzimudu kutokana na hali ya uchumi ambao wanao. Kwa hiyo, niombe Wizara husika waje na mpango kuona namna ya kupunguza baadhi ya tozo kwa hawa watu wetu ambao ni wavuvi ili waweze kunufaika na kazi ya uvuvi ambayo wanafanya.

Mheshimiwa Spika, nizungumzie sekta ya afya. Eneo hili asubuhi limechangiwa katika hoja mbalimbali kupitia maswali. Huduma ya bila malipo kwa akina mama wajawazito, watoto na hata wazee; ni kweli kuna baadhi ya hospitali zinatoa lakini kuna shida kubwa sana ya upatikanaji wa dawa katika sehemu ambazo wananchi hawa wanatibiwa. Ama dawa MSD hazipatikani lakini hata kama zikipatikana basi mpango mzima wa kando unafanyika na kunakuwa na shortage kubwa sana ya dawa.

Mheshimiwa Spika, tumeona hata Mheshimiwa Waziri wa Afya amejaribu kwenda na hoja ya kutaka kuangalia equation tu iliyopo kati ya uwepo wa panadol na mwananchi kukosa dawa na akasema hii siyo simultaneous. Mimi nimpongeze kwa namna ya pekee sana kwa jinsi ambavyo ameamua kuja kwa kasi na kuhakikisha kwamba sehemu zetu dawa zinaendelea kuwepo na wananchi wetu wanapata dawa.

Mheshimiwa Spika, niombe sasa, MSD bado kuna shida. Tunaweza kwenda na order kubwa ya dawa na fedha ambazo tayari ziko MSD lakini MSD inakosa dawa. Niombe sasa Serikali kupitia Wizara ya Afya kuhakikisha kwamba tunaimarisha MSD ili iweze kuwa na sehemu kubwa ya kupata dawa ili wananchi wetu sasa waweze kupata dawa katika sehemu ambazo wanakuwepo.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ambalo nilitaka kuchangia ni maliasili na utalii. Kuna shida kubwa sana ya tembo kusumbua na kuharibu mazao ya wananchi wetu. Nizungumzie kwa mfano kule kwangu Jimboni Busega kuna Kata za Lamadi, Mkula kwa maana ya Kijereshi, kuna shida kubwa ya tembo. Katika mwaka uliopita 2020, zaidi ya wananchi wanne wameuawa na tembo kwa sababu ya kukaa katika kata hizo ambazo nimeweza kuzitaja.

Mheshimiwa Spika, kuna haja kubwa sana ya kuimarisha ulinzi wa wanyamapori kupitia maaskari wetu. Ninajua Mheshimiwa Waziri Mkuu alipofika pale kwenye jimbo langu aliahidi kutupatia askari 26 ili waongeze kuimarisha ulinzi wa wanyamapori na hii itatusaidia sana wananchi wetu kufanya kazi zao wakiwa na amani. Sasa kwa sababu mazao yao yanaharibiwa tunawapa tena wakati mgumu wa kupata mazao ili waweze kunufaika na mazao yao.

Mheshimiwa Spika, naomba sasa kuunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kwa kumshukuru Mungu kwa kutuwezesha kuwa hapa. Lakini pia nikushukuru wewe kwa kunipa nafasi hii nami kuchangia Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa nchi yetu. Nimpongeze pia Mheshimiwa Vuma kwa kuitambua na kukubali mafanikio ya Timu ya Simba. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijikite katika mambo machache sana kuchangia mpango huu ili kuendelea kuimarisha uchumi wetu. Lakini ijulikane ya kwamba ni lazima sisi kama Wabunge tuendelee kuisimamia Serikali ili tufikie ule mpango ambao unasemwa sasa wa per capita income dola 1,400 katika hii miaka mitano ijayo. Kwasababu sasa ni 1,080 na cut off ni 1,036. Kwa hiyo, bado tuko katika eneo ambalo si salama kwa sababu tofauti yake ni dola 44. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano Nchi ya Algeria mwaka 2019 per capita income ilikuwa 4,060 lakini 2020 ilishuka ikawa 3,970. Kwa hiyo, kushuka pia inawezekana. Kwa hiyo, sisi kama Wabunge lazima tuisimamie Serikali ili uchumi wetu uendelee kupanda kama ambavyo Mheshimiwa Waziri wa Fedha ameeleza katika mambo matano ambayo ameyazungumza yatakayokwenda ku-reflect uchumi wetu. Na ninaomba uchumi huu sasa uende uka-reflect kwa wananchi hawa waliopo huko kwenye majimbo yetu na wananchi kwa ujumla wa nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi watu wa Simiyu ukitafuta identity yetu ni zao la pamba. Lakini wananchi wetu wameshapoteza hope na zao la pamba. Kwa nini; kwasababu ya bei ya zao la pamba. Leo ninataka kuzungumza kidogo kuiomba Serikali kutafuta namna ya kuwezesha Mkoa wa Simiyu kuupelekea kiwanda, hasa cha kuzalisha vifaa tiba vitokanavyo na zao la pamba. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tukipata kiwanda hiki maana yake zao la pamba sasa bei yake itaenda kuimarika. Na zao la pamba likiimarika maana yake sasa tutarudisha morali ya wananchi wetu kulipenda na kulima tena zao la pamba ambalo litaongeza uchumi wa wananchi wetu walioko huko kwenye Mkoa wa Simiyu.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kiwanda hiki kitasaidia nchi yetu kwa namna ya pekee sana kwasababu kitazalisha zaidi ya ajira ambazo ni rasmi 600 na ajira ambazo si za moja kwa moja zaidi ya 1,000. Wananchi watapata ajira, watalipa kodi, watapata kipato, na hii sasa itakwenda kuimarisha uchumi wa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa niombe Wizara ya Uwekezaji iendelee kuhakikisha kwamba inawekeza kiwanda hiki katika Mkoa wa Simiyu ili zao la pamba, kama nilivyosema pale awali, liweze kuimarika.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukitengeneza vifaa tiba vitokanavyo na pamba maana yake tunakwenda sasa kuimarisha kutokuagiza vifaa hivi nje zaidi ya asilimia 38.3. Asubuhi tumesikia hapa, tunaagiza zaidi ya asilimia 80. Sasa tukiwekeza kwenye kiwanda hiki tunakwenda kupunguza uagizaji kwa asilimia zaidi ya 38.3 ambapo tunatumia zaidi ya bilioni 147 kila mwaka kuagiza vifaa tiba nje ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ni imani yangu kwamba Waziri wa Fedha, Mawaziri wanaohusika, mtatusaidia kuhakikisha kwamba tunapata kiwanda kule Mkoa wetu wa Simiyu ili tuweze kuzalisha vifaa tiba vikiwemo cotton gauze, cotton swab na nguo za madaktari na manesi pamoja na mashuka ambayo yanaweza kutumika katika hospitali zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia niombe Wizara ipunguze tozo mbalimbali kwa ajili ya wawekezaji. Lakini pia mamlaka husika ziwe na lugha moja, hasa mamlaka zinazotoa vibali kwa hawa wanaokwenda kuwekeza kwenye miji yetu. Nilitaka nizungumzie sana hapo kwenye eneo la kilimo ili wananchi wetu sasa wakanufaike. (Makofi)

Kwenye eneo la kilimo bado hatujawekeza mahususi katika kilimo cha umwagiliaji. Bado hatujatumia Ziwa letu Victoria, hasa kwenye Mwambao wa Ziwa Victoria, bado hatujalitumia vizuri katika suala zima la kilimo cha umwagiliaji. Ukianzia kule Rorya, ukija Musoma, ukija Bunda, ukija pale Busega, ukienda Magu, Mwanza, Sengerema, Buschosa na huko mpaka Bukoba, bado hatujatumia ziwa letu katika kilimo cha umwagiliaji. Kwa hiyo, niombe Wizara ya Maji ijikite kuhakikisha kwamba tunaimarisha miundombinu ili tuwe na kilimo cha umwagiliaji katika sehemu zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninapongeza mradi ulioko mkubwa wa kuleta maji hapa; mzuri sana. Lakini pia niseme sisi ambao tunazungukwa na Ziwa Victoria bado tuna shida kubwa ya maji. Mfano kwenye Wilaya ya Busega wanaotumia maji safi na salama ni asilimia 42.9; bado tatizo ni kubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo tunapokuwa tunaangalia suala hili la maji pia tuone kabisa kwamba linaenda ku-reflect kilimo cha umwagiliaji kwa wananchi wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la pili ambalo nataka kuchangia hapa ni eneo la asilimia10 ambazo zimepangwa kisera kwenye halmashauri zetu, ambapo asilimia nne ni kwaajili ya vijana, asilimia nne kwaajili ya akina mama na asilimia mbili kwaajili ya walemavu.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii ipo kisheria na imepangwa lakini cha kusikitisha ni kwamba haifuatwi na hakuna anayefuatilia. Unakuta Halmashauri imepata mapato ya ndani safi lakini asilimia ambazo zinaenda kwenye group hili hazifiki hata 10, na hamna anayehoji wala anayesimamia. Wakurugenzi hawaojiwi, business as usual.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo hili lazima tulisimamie. Kama ni asilimia 10 itengwe kweli, kama makusanyo ya ndani ni bilioni moja asilimia 10 ni milioni 100, no discussion kwenye hili, ipelekwe milioni 100 sehemu husika. Lakini sasa hivi inaweza ikawa milioni 100 zikaenda milioni tano, milioni saba, hamna anayehoji, hamna anayechukua hatua, ni lazima eneo hili twende tukachukue hatua ili sasa vijana wetu tuwaimarishe na waweze kupata fedha hizi ili sasa waweze kuzitumia katika kuinua kipato chao pamoja na hawa akina mama na watu wenye ulemavu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nichangie kidogo kwenye eneo la maliasili na utalii. Nimesikia kengele ya kwanza. Ukitoka Lamadi kuelekea Bunda pale katikati ya Lamadi na Bunda kuna wanyama wa Mbuga ya Serengeti. Ningeishauri Serikali, ili kuinua pia uchumi wa maeneo yale tufungue namna ya wanyama wetu waweze kwenda hadi ziwani, ukienda pale Nyatwali wanyama waende mpaka ziwani. Nasema hivi kwasababu itafungua uwekezaji katika Miji yetu ya Lamadi na Bunda na wananchi wa pale watazidi kunafaika na hali halisi ya uwekezaji ambao utapatikana maeneo yale.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo niombe Wizara ya Maliasili iliangalie hili, ni eneo mojawapo ambalo tunaweza kuwekeza na ni eneo mojawapo ambalo linaweza kuipatia fedha Serikali, na hasa hasa katika hizi sehemu ambazo nimezitaja ikiwemo na mji wa Lamadi ambao sasa ni mji mkubwa, pamoja na mji mwingine wa Bunda. Eneo hili lazima tulitazame ili liweze kuingiza kipato katika eneo letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie kidogo habari ya TARURA, TARURA lazima tuitafutie fedha; kama TANROADS wanapata asilimia 70 na TARURA asilimia 30 kuna haja ya kuzungumza hapa tena. Kuna haja ya kuendelea kuingalia TARURA kwa jicho la pili, kuna haja ya kuingozea fedha ili maeneo yetu sasa yatengenezwe. Kule vijijini na kwenye majimbo tatizo la TARURA ni kubwa, tatizo la TARURA linalalamikiwa kila mahali. Barabara hazipitikim ukienda pale jimboni kwangu barabara ya kutoka Mwamanyiri kwenda Badugu haipiki, barabara nyingi hazipitiki. Sasa hata kama wazalishaji wa pamba watazalisha hatimaye tutazungumza tena habari ya barabara. Kwamba sasa gari zinaendaje kuchukua pamba huko ambako pamba imezalishwa kuja hapa mjini.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunapokuwa tunazungumzia kuimarisha uchumi wa watu na kuimarisha uchumi wa mtu mmoja mmoja lazima pia tuziangalie bajeti ya TARURA.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo niombe Wizara ya TAMISEMI, lazima tuje tuzungumze, na hapa lazima tuje tuone hali halisi ya namna ya kuiwezesha TARURA ili iweze kufanya kazi kubwa kwa ajili ya wananchi wetu. Wapo wengine ambao wamekuwa wakisema irudi TANROAD, Wizara ya Ujenzi lakini hapa issue sio kurudi TANROAD issue ni kuiongezea fedha ili iweze kufanya kazi vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja na kazi iendelee. (Makofi).
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia taarifa za Kamati zetu tatu, PAC, LAAC pamoja na PIC. Kwanza nianze kwa kuzipongeza sana Kamati hizi tatu kwa kazi kubwa ambazo wamefanya kuhakikisha kwamba wanapata ripoti iliyo salama na wametuletea hapa leo.

Mheshimiwa Spika, nimshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa anayofanya ya kutafuta fedha, ingawa yapo mambo ambayo yameelezwa kwenye taarifa za Kamati ambayo si mazuri kwa nchi juu ya ubadhirifu wa fedha za Serikali.

Mheshimiwa Spika, katika ripoti hii nitajikita maeneo matatu. Jambo la kwanza ni eneo la Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu. Pia nitachangia uendeshwaji wa Kiwanja cha Ndege Kilimanjaro (KIA) na la tatu kama muda utakuwa bado unaruhusu nitazungumza kidogo Wakala wa Mabasi Yaendayo kwa Haraka (DART).

Mheshimiwa Spika, CAG amefanya ukaguzi wa ufanisi katika Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu. Kuna mambo yamebainika ambayo yanahitaji kupelekewa miongozo ya namna ya uendeshaji wa mifumo ya upatikanaji wa wanafunzi ili waweze kunufaika na mikopo inayotolewa.

Mheshimiwa Spika, jana tumezungumza sana hapa juu ya hoja ambayo ililetwa na Mheshimiwa Ezra juu ya wanafunzi ambao hawajapata mikopo. Katika ukaguzi huu wa ufanisi uliolenga kuangalia ufanisi wa utoaji wa mikopo kwa wanafunzi wetu. Vilevile ukaguzi huu ulilenga kuangalia ufanisi wa namna zinavyoshughulikiwa rufaa pale ambapo wanafunzi wanapokuwa wamekata rufaa juu ya upatikanaji wa mikopo yao.

Mheshimiwa Spika, yapo mambo machache ambayo yamebainika. Kwenye taarifa ile alifanya ukaguzi wa miaka mitano, lakini kuna mwaka 2018/2019 mwaka ule ulikuwa na shida kubwa. Ilibainika kwamba wanafunzi 6,182 walipewa mikopo zaidi ya kiwango walichotakiwa kupewa chenye thamani ya 5,670,000,000, kiwango hiki kama wangepewa wanafunzi wengine ambao hawakupata mikopo tungepata wanafunzi wengine 2,835. Tungegawa katika halmashauri zetu 184, kila halmashauri wanafunzi 15 wangenufaika na fedha hizi ambazo walipewa wanafunzi zaidi ya kile walichokuwa wanahitaji.

Mheshimiwa Spika, nikisema hivi naamanisha nini hapa? Namaanisha kwamba mwanafunzi amekubaliwa kupewa kiasi fulani cha mkopo, lakini katika reality wakati anapokuja kupewa mkopo ule anapewa zaidi ya kile kiwango alichokubaliwa, inapelekea wanafunzi wengine kukosa mikopo na huu ulikuwa ni mwaka mmoja wa 2018/2019. Ukiangalia katika miaka yote mitano aliyofanya ukaguzi wa ufanisi CAG 13,000,000,000 zilizidishwa kwa wanafunzi ambao walikuwa wanapewa zaidi ya mikopo husika.

Mheshimiwa Spika, wanafunzi 2,852 walipewa mikopo chini ya kile kiwango walichokuwa wamekubaliwa pale awali. Hii inaamanisha nini? Maana yake mwanafunzi amekubaliwa atapewa asilimia kadhaa, lakini mwisho wa siku anakuja kupewa chini ya kile kiwango ambacho alitakiwa kupewa. Tunamfanya mwanafunzi asimalize masomo yake au tunamfanya mwanafunzi kuhangaika na masomo yake. Nini kilifanyika hapa? Zaidi ya 1,147,000,000 wanafunzi hawakupewa stahiki waliokuwa wanatakiwa kupewa.

Mheshimiwa Spika, wanafunzi 756 walipewa mikopo bila kuwa na sifa za kupewa mikopo, yaani hawana sifa ya kupewa mikopo lakini wakapewa, thamani yake 2,255,000,000. Hapa napo tungepata wanafunzi wengi ambao wangeweza kunufaika na mikopo hii hata pale Mbeya Jiji nao wangepata kupitia fedha ambazo kuna wanafunzi walipewa ambao walikuwa hawahitajiki kupewa mkopo.

Mheshimiwa Spika, nini sasa hapa tafsiri yake? Tafsiri yake katika Bodi yetu ya Mikopo bado kuna shida ya mfumo unaotumika katika utoaji wa mikopo ya elimu ya juu. Kama mwanafunzi alitakiwa kupewa 1,000,000 anapewa 1,200,000 tafsiri yake ufanisi wa ule mfumo siyo salama. Hapa umefanyika ukaguzi wa ufanisi. Sasa ukifanyika ukaguzi wa hesabu itakuwa tatizo zaidi.

Mheshimiwa Spika, nashauri sasa kama inawezekana tufanye ukaguzi wa kina juu ya mfumo unaotumika wa utoaji wa mikopo kwa wanafunzi wa elimu ya juu. Ukisoma ripoti ya CAG inakupa indication kwamba mfumo siyo salama kwa kutoa mikopo kwa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile katika ukaguzi huu uangalie hizi 5,670,000,000 za 2018/2019 walipopewa wale wanafunzi zaidi hao wanafunzi walikuwepo kule site au kuna watu walikuwa wanawapa halafu baadaye wanakwenda kuzichukua? Hizo ndio indication za hii. Je, hao wanafunzi waliopewa mkopo wakati hawana sifa hao waliowapa bado wako ofisini? Kwa hiyo ukifanyika ukaguzi wa kina utayabaini haya mambo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niende eneo la pili, eneo la uendeshaji wa Kiwanja cha Ndege cha Kilimanjaro unaoendeshwa na Kampuni ya KADCO, hapa bado kuna shida. Kampuni ya KADCO iliingia mkataba na Serikali mwaka 1998 ili kuendesha Kiwanja cha Ndege cha Kilimanjaro kwa miaka 25. Wakasainishana mkataba, ule mkataba Serikali ikawa na hisa asilimia 24 na kampuni ikawa na hisa asilimia 76. Katika kuendesha ule uwanja inaonekana ufanisi haukuwa mzuri. Serikali 2009 kupitia Baraza la Mawaziri wakakubaliana kununua hisa zote za KADCO kwa asilimia 100. Mwaka 2010 Serikali ilinunua hisa zote za KADCO kwa asilimia 100. TAA ililipa fedha milioni 5.3 fedha za Kimarekani sawa na milioni karibu 12.

Mheshimiwa Spika, mwaka 2010 baada ya Serikali kununua zile hisa nini kiliendelea? Uendeshwaji wa Kiwanja cha Ndege cha Kilimanjaro umeendelea kuendeshwa kama private entity. Wameendelea kuwa na mkataba wa concession agreement. Sasa unajiuliza maswali ya kutosha. Swali la kwanza, kama Serikali imenunua hisa zote asilimia 10,0 maana yake Serikali 100% ndio mmiliki wa kiwanja. Kwa tafsiri ya kawaida uendeshwaji wa kiwanja ulitakiwa kuwa chini ya Serikali kupitia TAA. Sasa hii concession agreement iliyopo wanaoendelea kutumia mpaka leo mpaka kesho na jana ni kati ya mkataba wa Serikali na watumishi wa KADCO walioko Kiwanja cha Ndege cha Kilimanjaro au ni kati ya KADCO kama private entity na Serikali? Kama ni hili la pili nini maana ya kununua hisa kwa asilimia 100. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama Baraza la Mawaziri lilishauri kiwanja kile kiendeshwe na TAA kwa nini hakikuendeshwa mpaka leo? Kwanza cha ajabu zaidi hata fedha wanazokusanya KADCO mpaka leo tunaweza kusema wanazitumia fedha mbichi, kwa nini? Kwa sababu hazipiti Mfuko Mkuu wa Serikali, yaani wao wanakusanya kesho wanapanga matumizi, wanatumia. Wana kipengele kidogo tu wanalipa dividend Serikalini kwa TR hapo tu. Mwaka 2021wame-declare kulipa 350,000,000.

Mheshimiwa Spika, sasa nashauri kwamba, kwa kuwa Serikali ilinunua hisa zote asilimia 100, sasa kiwanja hiki shughuli zote za uendeshaji zirudi TAA. Kwa nini nasema hivyo? tulipohoji kwa Afisa Masuhuli kwa nini wameamua kuendeleza hizi alitujibu jibu simple sana anasema kiwanja hiki kipo kimikakati ya kibiashara. Sasa mimi tu wa la saba wa Busega kule inaniingia kweli kichwani kwamba Kiwanja cha Ndege cha Dar es Salaam hakiko kibiashara eti cha Kilimanjaro kiwe kibiashara zaidi? Kama ingekuwa ni kibiashara basi Kiwanja cha Ndege cha Dar es Salaam ndicho kiko kibiashara zaidi kuliko Kiwanja cha Kilimanjaro. Kwa hiyo, nashauri tufanye hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili tufanye special audit ili kuangalia mapato yote yaliyopatikana katika miaka 10 hii yote ambapo KADCO walikuwa wanaendesha kiwanja kile kama Serikali, ili tubaini kama fedha hizi zilitumiwa vizuri na sheria za fedha zilifuatwa. Tukifanya yale yote yatatusaidia kujua ni kwa kiwango gani tumepata hasara kule Kilimanjaro. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kingine ambacho nataka nichangie ni Wakala wa Mabasi Yaendayo kwa Haraka (DART). Tumeona Taarifa ya Kamati imesema hawa DART walilipa 1,700,000,000 kama fidia kwa wananchi kuachia maeneo, lakini CAG anasema fedha hizi zilikuwa nyongeza ya malipo nje ya valuation report iliyokuwepo, yaani Valuation inasema lipa 5,000,000,000 wao wakalipa zaidi 1,700,000,000. Sio hivyo tu, wakalipa na posho za usumbufu 435,000,000. CAG alipoomba kibali, walipata wapi kibali cha kuongeza kulipa fidia hawana. Hivi kweli wanapata wapi ujasiri wa kulipa 1,500,000,000 nje ya valuation report? Wanajibu kirahisi tu waliambiwa na Serikali. CAG anauliza leteni hicho kibali mlichopewa na Serikali, hawana. Hivi tumefika kuendesha taasisi yetu kwa style hiyo?

Mheshimiwa Spika, hapa kuna madudu ya kutosha juu ya malipo ya 1,500,000,000. Vilevile hapa tufanye special audit kuwabaini wale wote waliolipwa 1,500,000,000 kama ilikuwa ni halali. Pia wachukuliwe hatua watumishi ambao wameisababishia hasara Serikali kwa kulipa watu bila kufuata valuation report.

Mheshimiwa Spika, fedha hizi ni fedha za Watanzania na kibaya zaidi miongozo inasema valuation ikifanyika leo baada ya miezi sita, mnaongeza interest kwa wale mliowakadiria. Baada ya miaka miwili, miongozo inasema kurudia valuation. Sasa wale muda umepita miaka 10, hawajafanya tena valuation, wanaibuka tu kulipa zaidi 1,570,000,000. Hili haliwezekani tufanye special audit DART ili tupate taarifa rasmi, fedha hizi wahusika waliolipwa na tuone tija kwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo moja la kumalizia. Ukienda pale Soko la Kariakoo, nafikiri liliungua mwezi Julai mwaka jana, pale napo kuna shida. Tunawaza kwamba, baada ya kufunga mwaka wa fedha 2021 kwa maana Juni, baada ya siku 10 tu soko likaungua, documents zote zikaungua, hamna cha risiti ya mapato, hamna cha risiti ya matumizi. CAG amewapa unqualified report, lakini ni kwa nini? Hapana siyo unqualified report amewapa disclaimer report ameshindwa kutoa maoni kwa sababu hamna document yoyote inayomfanya ku-verify mapato ya 3, 500,000,000 na matumizi ya 3,500,000,000.

Mheshimiwa Spika, sasa hii kwa akili tu ya kawaida inanitafakarisha na kunifanya nione inawezekana Soko la Kariakoo liliungua baada ya documents hizi kutoonekana ofisini. Ni akili tu ya kawaida inanituma hivyo. Kwa nini baada tu ya kufunga mwaka wa fedha Juni, siku 10 tu, halafu mwisho wa siku CAG ameenda pale hamna document yoyote ameshindwa ku-verify matumizi ya 3, 500,000,000. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa leo nimekuja na special audit tu mwanzo mwisho. Hapa napo ifanyike special audit ya 3,500,000,000 tujue tatizo kubwa lilikuwa ni nini. Sasa sijui watapata wapi document, lakini najua kwa sababu itakuwa ni special na kwa sababu special unaweza ukawahoji watu, CAG atajua namna ya kufanya, lakini mwisho wa siku tupate mbichi na nzuri kwa hapa kwenye Soko la Kariakoo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naomba kuunga mkono hoja za Kamati. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi na mimi kuchangia Wizara ya Maji. Kipekee sana nimpongeze sana rafiki yangu Mheshimiwa Aweso kwa kazi kubwa anayofanya pamoja na Naibu Waziri na Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji. Wanafanya kazi kubwa, tunaona kazi zao wanazofanya, kweli zimekuwa ni kazi za msingi. Niwaambie tu kwamba wananchi hasa wananchi wa Busega wana imani kubwa nao kwa sababu wameona mageuzi makubwa ambayo wameyafanya kwenye Wizara ya Maji kwa huo muda mfupi ambao wamekuwa kwenye madaraka.

Mheshimiwa Naibu Spika, mageuze hayo ni Pamoja na namna ambayo wamefanya kuhakikisha kwamba wanapunguza gharama za ujenzi wa miundombinu ya maji, kwa sababu tumeona kuna sehemu zingine ambazo wameenda, gharama zimeshuka, unakuta BOQ ilikuwa bilioni mbili lakini kwa sababu wamenda pale mmefanya revision ya budget zimeshuka mpaka kufikia hata bilioni 1.6. Haya ni mageuzi makubwa sana ya kimkakati ambayo wameamua kuyafanya kwenye Wizara yenu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kipekee pia nimshukuru sana Waziri Mkuu, Mheshimiwa Kassim Majaliwa alipokuja pale kwangu Mkura aliahidi kutupatia mradi wa maji na sasa mradi tayari umeshaanza kazi, tayari wakandarasi wako pale wanafanya kazi. Kwa kweli, tunawapongeza sana na muda ujao naamini kwamba mradi huu utaanza kutoa maji. Nimwombe tu rafiki yangu Waziri, bado kuna shida ya fedha pale. Naomba apeleke fedha ili mradi ule ukamilike kwa wakati na naamini kabisa kwamba Mheshimiwa Waziri ni msikivu na kwa sababu ni kijana na kwa sababu Wasukuma ni wakarimu aende pale akaangalie namna mradi unavyotekelezwa ili umalizike kwa haraka sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nizungumze suala moja ambalo limekuwa likinipa shida kidogo. Kuna baadhi ya miradi ambayo inaenda kutelekezwa kwenye kata, lakini unakuta kata moja ina vijiji vine, lakini mradi unakuwa wa vijiji vitatu, kijiji kimoja kinabaki. Hili limekuwa ni tatizo na niishauri Wizara, kama wameamua kupeleka mradi kwenye kata, basi ni nzuri kata nzima kumaliza vijiji vyake vyote ili kisibaki kijiji na ikaonekana kama wametengwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nina mfano, kwenye Kata ya Kiloleli yenye vijiji vinne, Kijiji kimoja kimeachwa, Kijiji cha Ilumya, lakini kwenye Kata ya Mwamanyili, Kijiji kimoja cha Milambe ambako Mbunge anatoka kimeachwa. Kwenye Kata ya Mkura, Vijiji viwili kwa maana ya Mwang’ale na Chabutwa vimeachwa. Kwa hiyo, nafikiri kwamba tunapokuwa tunafanya designing ya mradi kwenye kata husika basi ni vizuri kata nzima iweze kuchukuliwa na vijiji vyote viweze kupata maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nimefurahishwa sana na namna ambavyo wameanza kuleta mkakati wa mradi mkubwa wa maji wa Ziwa Viktoria kwenda Itilima ambao kwa awamu ya kwanza utaanza na Busega, utaenda Bariadi lakini pia utaenda Itilima. Mradi huu ni mradi mkubwa na ndiyo mradi pekee ambao uta-solve tatizo la maji kwa Wilaya ya Busega, Wilaya ya Bariadi na Wilaya ya Itilima.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimwombe Mheshimiwa Waziri, kwamba, moja ya mradi ambao unatakiwa macho ya Waziri yaende hapo ni huu mradi mkubwa sana, kwa sababu hii miradi mikubwa unapokuwa umemalizika ni mradi ambao utahudumia wananchi wengi. Pale kwangu Jimbo la Busega zaidi ya vijiji 42 vinaenda kupitiwa. Mradi huu kwa Mkoa wa Simiyu utapita kwenye vijiji 256.

Mheshimiwa Naibu Spika,naomba na nimeona Waziri tayari ameweka kwenye Mpango bilioni 19 kwa ajili ya kuanza kati ya bilioni 400. Nimwombe kwamba awekeze sehemu hii ili wananchi wengi, zaidi ya 200,000 wa Wilaya ya Busega waweze kupata maji kupitia mradi huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninavyokwambia sasa Wilaya ya Busega wananchi wanaopata maji safi na salama ni asilimia 52 wengine bado hawapati maji safi na salama na kijiji cha mwisho ni kijiji chenye kilometa 42, leo tunazungumza kuleta maji Dodoma zaidi ya kilometa 800 tunaomba na sisi utukumbuke kwenye kilometa 42 nao waweze kupata maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja asilimia mia moja. Mheshimiwa Aweso karibu Usukumani, karibu Busega. Ahsante. (Makofi)
Hoja ya Dharura (Changamoto ya Kupanda kwa bei za Mafuta ya Petroli, Dizeli na Mafuta ya Taa)
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili nami nijadili hili suala la dharura. Nimpongeze sana mtoa hoja kwa kutoa hoja hii ninaamini sasa sisi kama Bunge tunaenda kuishauri vizuri Serikali ili iweze kuchukua hatua. (Makofi)

Kama alivyosema Mheshimiwa Musukuma, kwamba sasa hivi mafuta yamepanda. Ukiangalia kwenye baadhi ya majimbo huko vijijini; kwa mfano kule ambako hakuna sheli (vituo vya mafuta sasa hivi kule mafuta yanauzwa zaidi ya shilingi 5,000. Jambo hili ni hatari kwa kuwa tunajua mafuta yanapopanda bei kila kitu kitapanda bei. Tunavyozungumza leo, jana kusafirisha cement kutoka Tanga kwenda Mwanza, hapo nyuma walikuwa wanasafirisha kwa tani moja shilingi 130,000 lakini tunavyozungumza leo tani moja ya cement kusafirisha kutoka Tanga kwenda Mwanza imepanda mpaka shilingi 160,000 ambapo inaenda kupandisha mfuko wa cement kwa shilingi 1,500 jambo hili ni kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naishauri sasa Serikali kwa mambo mawili; jambo la kwanza ni kufanya hatua za dharura, kutafuta fedha kwa ajili ya kupeleka ruzuku kwenye mafuta ili walau tuweze kupunguza gharama za mafuta. Tukiweka ruzuku pale maana yake gharama ya mafuta inapungua, na ikishapungua hizi gharama za mafuta zitapunguza gharama za vitu vingine ambavyo sasa vitapanda bei.

Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo, ninajua wazi kwamba tuna tozo nyingi ambazo tumeweka kwenye mafuta kwa ajili ya nchi na kwa ajili ya bajeti tuliyoipitisha. Lakini sisi ndio Wabunge na sisi ndio tuliyopitisha bajeti, hivyo kuna haja sasa ya kuangalia baadhi ya tozo tuweze kuziondoa kwa wakati wa dharura kwa hii miezi miwili; kwa maana ya mwezi wa tano na mwezi wa sita, tuzipunguze takribani kuanzia shilingi 400 mpaka shilingi 500 ili tuwe na unafuu kwenye mafuta. Tukiyafanya haya yataleta unafuu wa maisha kwa wananchi wetu, hamna namna ambayo tunaweza kufanya kwa sababu maisha ya kwetu tunayajua huko vijijini yanategemea mafuta; bila mafuta maisha hayaendi. Kwa sababu gani, kwa sababu leo cement itapanda, nondo zitapanda, sabuni zitapanda kila kitu kitapanda kwa hiyo, lazima tuchukue hatua za tahadhari za haraka ili kunusuru hili janga kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninaomba sasa nami kuunga mkono hoja na tuweze kutafuta fedha za dharura tuweze kunusuru suala hili la dharura katika nchi. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kunipa nafasi hii nami nichangie Wizara hii ya Mifugo na Uvuvi, lakini kipekee nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri kwa kazi kubwa ambayo wanafanya pamoja na Watendaji Wakuu wa Wizara.

Mheshimiwa Spika, leo nataka kuchangia tu mambo mawili katika Wizara hii ya Uvuvi. Hapa nyuma kidogo tumekuwa na wimbi kubwa la upungufu au uhaba wa samaki viwandani, leo nataka niishauri Wizara jambo mojawapo ambalo linalosababisha kuwa na uhaba wa samaki katika viwanda vyetu.

Mheshimiwa Spika, ijulikane ya kwamba tuna samaki aina ya sangara hasa kwenye Ziwa letu la Victoria na samaki huyu kwa kilo moja anauzwa shilingi 9,000 mpaka shilingi 10,000 pale Mwaloni. Sasa chukulia samaki wa kilo tano kwa shilingi 9,000 atauzwa shilingi 45,000; lakini ijulikane ya kwamba bondo ndani ya ile samaki ndio lenye samani kubwa kuliko mnofu. Sasa wanapokuwa wanauza pamoja na bondo lake kwa shilingi 9,000 na akipeleka kiwandani atauza kilo moja kwa shilingi 12,000 ina maana kwa samaki mwenye kilo tano atamuuza shilingi 60,000; lakini bondo linauzwa zaidi ya shilingi 60,000 samaki mwenye kilo tano.

Mheshimiwa Spika, sasa mvuvi amekuja na option ambayo ni ya kawaida tu kwamba badala ya kumpeleka yule samaki kiwandani bora mnofu wake awauzie wananchi halafu yeye anufaike na lile bondo. Anajikuta kwa wananchi anaweza kumuuza yule samaki wa kilo tano mpaka shilingi 40,000 mpaka shilingi 50,000 na bondo pia akauza kwa shilingi 50,000.

Mheshimiwa Spika, hapo atajikuta ameingiza shilingi laki moja kwa samaki mwenye kilo tano, lakini atakapompeleka kiwandani atamuuza kwa bondo lake kwa shilingi 60,000 hata ningekuwa mimi nisingeweza kupeleka samaki yule kiwanda.

Sasa mimi niishauri Wizara, waruhusiwe wavuvi au wafanyabishara ambao wanapeleka samaki kiwandani basi kuwepo na thamani ya mnofu na thamani ya bondo liuzwe peke yake, hii itasababisha kunufaisha huyu mvuvi kwa sababu thamani ya samaki itaongezeka, na kama hazitafanya hivi maana yake wataendelea hao wavuvi kutaka samaki vipande vidogo vidogo, wanawauzia wananchi na viwanda nyetu vitaendele kuwa na uhaba kama ambavyo imeonekana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia ijulikane ya kwamba matumizi ya ndani yameongezeka ya watumia samaki kama kitoweo hata marafiki zangu hapa Wagogo wanataka samaki kutoka Ziwa Victoria kule Usukumani, sasa ni lazima tu viwanda vikose samaki. Kwa hiyo mimi niishauri Wizara kwamba pia lazima tujikite sana kwenye mabwawa ili tuendelee kupata samaki wengi na hawa samaki waweze kutumika katika matumizi yale ya kawaida ya ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia kupunguza ukiritimba hawa wawekezaji wanapokuja kwa ajili ya vizimba, ukija na kizimba utapewa masharti makubwa, tafute eneo kijijini, nenda katafute kibali, lete mtu wa TAFIRI aje apime, huu mlolongo unasababisha wawekezaji wanaondoka; nilitamani sana Wizara iliangalie hili ili mwisho wa siku tuwe na malighafi ya kutosha kwenye viwanda vyetu.

Mheshimiwa Spika, lakini suala lingine ambalo nilitaka kushauri ni tozo kwa wavuvi; kuna tozo nyingi hapa kwa wavuvi kuna tozo inayotozwa na TASAC ambao wanakuja kukagua ubora wa mtumbwi wanatoza shilingi 70,000.

Mheshimiwa Waziri umefika pale kwangu ulikuja wananchi walikulalamikia na ulisema utalishulikia hili lakini bado halijashughulikiwa bado wanatoza shilingi 70,000 kukagua ubora wa mtumbwi. Sasa hapa wananchi wangu wameniuliza swali ndogo sana kama leo mtumbwi ni mpya unakuja kukaguliwa nalipa shilingi 70,000 wakati ni mpya wala haujatumika, sasa wanakagua ubora upi wakati bado ni mpya.

Mheshimiwa Spika, hili swali ni very technque kidogo, mimi niishauri Wizara kwamba wananchi wetu hawajakataa kulipa, lakini wanaona shilingi 70,000 ni kiwango kikubwa sana ukilinganisha na kazi ambayo inakuja kufanyika. Kwa hiyo niiombe Wizara iweze kuliangalia hili.

Mheshimiwa Spika, lakini pia kuna tozo kama leseni ya mtumbwi inayotozwa na halmashauri shilingi 30,000 lakini pia kuna leseni kwa mvuvi mmojammoja shilingi 20,000 hapa pia na penyewe nilitamani sana…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Spika naunga mkono hoja, lakini tuangalie bei ya samaki ukilinganisha na bondo. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi, nami nikupongeze kwa kuwa Mwenyekiti. Nakutakia mema sana katika kazi hiyo. Pia nichukue fursa hii adimu sana kumpongeza Waziri, mtani wangu kwa kazi kubwa sana anayoifanya kwa jamii yetu hii ya Tanzania. Kipekee nampongeza Naibu Waziri kwa kazi
kubwa pia anayofanya na kweli ameonesha hekima kubwa sana hata leo asubuhi, ameonesha upendo wa dhati sana kwenye Wizara yake na hiyo ndiyo tumeona faida kubwa sana ya kuzaliwa usukumani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichangie mambo machache sana kwenye Wizara hii leo. Naishauri sasa Wizara, leo asubuhi hapa Mheshimiwa Mrisho Gambo amesema asilimia 80 ya mapato ya Wizara ya Utalii yanapatikana kule Kanda ya Kaskazini. Hata hivyo, tunaamini kabisa kwamba Kanda ya Ziwa pia tunaweza kuwa na mapato makubwa ya utalii mkitufanyia mambo ya msingi sana ikiwemo na kufungua geti la Ndabaka lililoko pale Lamadi na pia mtufungulie geti la pale Kijereshi. Mageti haya mawili yatakuwa mageti ya msingi sana kwenye pato la Taifa; vile vile yatakuza uchumi wa Kanda yetu ya Ziwa, yatakuza uchumi wa pale Jimbo langu la Busega, hasa pale Lamadi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna hoteli nzuri sana Speke Bay, tuna hoteli nzuri pale Serenity na pia tuna hoteli nzuri pale Ndabaka, zina uwezo kabisa wa kutunza watalii. Naomba mtufungulie yale mageti ili yaweze kupokea watalii mbalimbali. Watalii siyo lazima waende KIA, wanaweza kushukia pale Mwanza Airport na baadaye wakaenda Lamadi kwa ajili ya kufanya tour pale Serengeti.

Kwa hiyo, nawaomba sana, mkitufungulia haya mageti mawili yatafanya kazi kubwa sana ya kukaribisha wale watalii na hasa mkiyatangaza. Myatangaze ili watalii wetu sasa waweze kupitia pale kwenye geti la Ndabaga lililopo pale Lamadi na geti la Kijereshi lililoko kule Kata ya Mkura.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo nataka nichangie ni uvamizi wa tembo kwenye makazi ya watu. Pale kwangu kuna Kijiji kinaitwa Kijereshi, kuna Kijiji kinaitwa Lukungu, kuna Kijiji kinaitwa Mwakiroba vijiji hivi vitatu vinaathirika sehemu kubwa sana na uvamizi wa tembo. Naomba sasa mchukulie hatua za dharula ili wananchi wetu sasa waweze kutokutishwa na hawa tembo. Mwaka 2020 tulikuwa na vifo zaidi ya vinne vilivyotokana na uvamizi wa Tembo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, leo nakuomba sana Mheshimiwa Waziri, wewe ni msikivu, naomba sana kwa mara nyingine tuweze kuangalia namna ya kuleta askari wa kutosha tuweze kutengeneza Stesheni pale Kijereshi ili maaskari waweze kukaa pale. Ikibidi linapotokea tatizo, basi wapatikane kwa urahisi kwa sababu sasa hivi wanakaa Lamadi na Kijereshi ni mbali kidogo, tembo wanapoingia kule Kijereshi, wao mpaka waje wafike ni zaidi ya nusu saa muda mwingine, mpaka saa nzima au saa 1.30 ndiyo wanafika. Tembo tayari watakuwa wameharibu mazao, tayari watakuwa wamewadhuru wananchi.

Kwa hiyo, naomba sana, mtengeneze Stesheni pale Kijereshi kwa sababu ndiyo sehemu kubwa ya hifadhi. Pia muwape gari pale. Kuna shida ya gari kwa ajili ya usafiri wa kukabili hawa tembo. Kwa hiyo, namwomba sana Mheshimiwa Waziri atusaidie hili ili tuweze kupata gari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine nililotaka kuzungumzia ni tatizo la TFS. Mheshimiwa Waziri, TFS ni pasua kichwa kwa baadhi ya watumishi; kuna baadhi ya watumishi sio waadilifu. Ukienda pale Magu, kuna TFS ambao wanalinda Hifadhi ya pori la Sayaka. Pale ni pasua kichwa. Wanakamata wafugaji, ni sawa inawezekana wanasimamia sheria, lakini faini ni kubwa sana. Ni shilingi milioni sita, shilingi milioni nne au shilingi milioni nane. Ni tatizo kubwa. Naomba sana tuliangalie hili, mfugaji akiambiwa kulipa shilingi milioni sita leo, haiwezekani. Mfugaji akiambiwa kulipa shilingi milioni nne leo haiwezekani; yaani how much is milioni nne? Yaani ni fedha nyingi kweli kwa mfugaji mdogo. (Makofi)

Mheshimwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba hawa watumishi kidogo wanapokuwa wanalingalia hili, wawahurumie na wafugaji wetu, wawahurumie na wakulima wetu kwa sababu wanaumizwa sana na faini ambazo wanapigwa. Mheshimiwa Waziri, nimeshazungumza, nawe umeshakubali kuja pale, uje ujionee namna wananchi walivyo na malalamiko juu ya hifadhi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nakuomba sana, wananchi wale walikuwa na shida ya eneo la mita 840. Naomba sana utakapofika pale uzungumze na wananchi, usikie kilio chao na kama utaona inafaa Mheshimiwa Waziri, basi muweze kuwarejeshea eneo hili ili watu wa Nyaruande pale Kata ya Nyaruande katika Jimbo langu la Busega na sehemu ya Jimbo la Magu waweze kunufaika pale Sayaka kwa sababu sasa hivi wanapata shida katika namna ya kupata sehemu za kuchungia ng’ombe, lakini pia sehemu kubwa ya kulima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, namwomba sana Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri; wewe kule ni kwenu, wewe pale ndiyo umezaliwa, hili tatizo unalifahamu, njooni mlitatue ili wananchi wetu sasa waweze kunufaika na hii sehemu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nskushukuru sana, niseme nawapongeza, nawakaribisha Busega mje mtatue huu mgogoro. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru nami kwa kunipa nafasi kuchangia Mpango wa Bajeti 2022/23.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kipekee sana nimshukuru Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama yetu Samia Suluhu Hassan, kwa kazi kubwa anayofanya kwa ajili ya Watanzania. Kipekee pia nimshukuru kwa fedha ambazo ametupatia hivi karibuni kwenye majimbo yetu, trilioni 1.3 katika sekta mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuchomekea hapo eneo la elimu. Ni kweli kuna kazi zinafanyika kubwa kwenye Majimbo sasa, madarasa yanajengwa, tunamshukuru sana. Lakini ukweli lazima tukubaliane kujengwa kwa madarasa lazima kuwe directly proportional na upatikanaji wa Walimu. Kwa hiyo mimi niishauri Serikali ije na mpango katika Bajeti ya mwaka 2022/23 wa namna gani tunakwenda kuajiri walimu ili wakabiliane na wanafunzi wengi ambao wanakwenda kutumia madarasa haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo tunavyokuwa tunamshukuru Mheshimiwa Rais kwa kutupatia madarasa pia tunamshukuru kwa sababu ni imani yangu kwamba tunakwenda ku-create ajira kwa ajili ya Watanzania na Walimu ambao bado hawajapata ajira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichangie maeneo machache sana ya mpango huu. Taarifa ya Kamati ya Bajeti pamoja na taarifa ya Mheshimiwa Waziri imeonesha kwamba mwenendo wa Shilingi yetu ya Tanzania unazidi kuimarika. Lakini niseme tu kwamba ili shilingi yetu iendelee kuimarika zaidi ni lazima tufikirie ku-export final product kuliko kuwa na importation kubwa ya raw material kwa ajili ya viwanda vyetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kwa nini tunazungumza hivi? Ni lazima tuimarishe viwanda vyetu vya ndani na kuendelea kujenga viwanda mbalimbali ambavyo vitatoa final product kutokana na malighafi ambayo sisi wenyewe tunatengeneza hapa, malighafi nyingi zipo zinatokana na kilimo. Tuchukulie mfano kule kwetu Mkoa wa Simiyu na Mikoa ya Tabora, Mara na Mwanza, tunalima sana pamba, lakini pamba bado haina thamani kwa sababu hatutengenezi final products zinazotokana na pamba, isipokuwa tunafanya exportation ya material ambayo kule wenzetu wanakwenda kutengeneza final product.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningeishauri Serikali, kuna andiko lilishaletwa Wizarani, Wizara ya Fedha na Wizara ya Viwanda, kujenga kiwanda Mkoa wa Simiyu ili uweze kuhudumia Mikoa ya jirani, na kiwanda hiki kitakuwa cha vifaatiba vitokanavyo na pamba. Tunajua tunaweza tukapata gozi, tunaweza tukapata mashuka. Tutaokoa fedha nyingi za kigeni ambazo tunakwenda kununua vifaa hivi nje, vitaendelea kupatikana kwenye nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kiwanda hiki pia kitatoa ajira kwa Watanzania, zaidi ya Watanzania 1,000 wataajiriwa kupitia viwanda hivi. Kwa hiyo tunapokuwa tunazungumza habari ya viwanda tunazungumza habari ya ku-maintain fedha yetu ili isiendelee kushuka thamani yake bali iendelee kupanda kwa kuwa na products ambazo zinapatikana kwenye nchi yetu. Mfano umeutoa, hata hivi vyuma ambavyo vinatengeneza reli tungekuwa tumetengeneza kupitia Liganga huko wataalam wanasema wala tusingekuwa na haja ya kuagiza. Maana yake fedha yetu ingeendelea kuimarika zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwenye kuimarika kwa fedha mimi huwa najifikiria swali moja, sijui wataalam wanasemaje, lakini huwa nawaza kwa nini mimi niko kwenye nchi yangu Tanzania ninakwenda hotelini naambiwa charge ni dola 200. Sasa nawaza kwa nini naambiwa dola 200 kwenye nchi yangu, si niambiwe tu laki nne ya Tanzania nijue? Kwa nini, kwa sababu demand ya dola itakuwa kubwa kuliko supply na demand ikiwa kubwa maana yake fedha yako ya Tanzania ina-depreciate.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa najua wataalam haya wanashauri na mimi naomba niseme kama ambavyo amepiga marufuku Mheshimiwa Simbachawene hivi karibuni kutupa pesa chini wakati wa kutunza vikundi mbalimbali, kuna haja sasa Mheshimiwa Waziri kuja na sera ya kukataza charges zozote ambazo wana-charge katika fedha za kigeni. Hakuna sababu ya kwenda kwenye hoteli ukaambiwa dola, maana yake itabidi ukatafute dola ili uende ukalipe hiyo charge ambayo utakuwa umeambiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikwenda siku moja pale…

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Kabla ya taarifa, Wasukuma mtaipata, mlizoea kutupatupa hela chini sasa mtakamatwa wote. Taarifa inatokea upande gani? Mheshimiwa Ester.

T A A R I F A

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nampa taarifa Kaka yangu, jirani yangu pale Mbunge wa Busega, kwamba ukienda nchi zingine ukifika airport lazima utabadilisha dola ili uweze kutumia kwa pesa za nchi husika, kwa hiyo ni jambo zuri.

MWENYEKITI: Unapokea taarifa Mheshimiwa Lusengekile.

MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea kwa mikono miwili kwa sababu nilienda hoteli moja hapa Dar es Salaam nikanywa soda nikaambiwa dola moja, yaani nikawaza kwa nini naambiwa dola moja, si aniambie tu elfu mbili nijue. Lazima tuheshimu fedha yetu, tukiheshimu fedha yetu itakuwa na thamani, hakuna sababu ya ku- undermine fedha yetu. Mheshimiwa Waziri wa Fedha liangalie hili. (Makofi)

MWENYEKITI: Kwa hiyo Musukuma wewe unakwenda kwenye hoteli hujui hata malipo yatakuaje? Endelea mtani. (Kicheko)

MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, issue hapa siyo kujua ni shilingi ngapi, issue hapa ni kuniambia anani-charge kwa dola hiyo ndiyo issue yangu. Mimi hata kama angesema 5,000 sina tatizo mtani, lakini shida ni kuni- charge kwa dola. Kwa hiyo, nataka tuimarishe shilingi yetu kwa namna ya pekee sana ya kuiheshimu fedha yetu. Mtu akifika airport pale ana dola zake atafute benki ilipo abadilishe achukue fedha zetu za ndani aende akaanze kutumia, hapo tutaimarisha shilingi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la riba, tumeona kwenye taarifa ya Kamati ya Bajeti. Wastani wa riba za mabenki kwenye kukopesha sekta binafsi tumeona ni asilimia 16.6. Ni kweli riba hizi ni kubwa na tunatamani mabenki yetu yapunguze riba.

MWENYEKITI: Kengele ya pili hiyo Mheshimiwa.

MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Spika, nami niungane na wachangiaji wengine kukupongeza kwa kuchaguliwa kwa kura nyingi sana. Naipongeza sana Kamati ya PAC na LAAC kwa taarifa ambayo wametuletea hapa inayoleta taswira kwa nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo ninaomba niishauri Serikali jambo moja. Serikali inapotaka kuingia kwenye uanzishwaji wa mifumo kwa ajili ya ukusanyaji wa fedha, naomba ifanye upembuzi yakinifu ili mifumo inayotengenezwa ije kuwa na tija kwa ajili ya Watanzania.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, Bandari mwaka 2010 iliingia mkataba wa miaka minne na Softech, mpaka 2014, kwa ajili ya kutengeneza mfumo wa ukusanyaji wa fedha. Mfumo huu ulikuwa unachukua gharama ya shilingi milioni 694, lakini mpaka kufikia mwaka 2014 mfumo haufanyi kazi na tayari Mkandarasi alikuwa amelipwa shilingi milioni 600 sawa na 87%. Inasikitisha kwa sababu fedha hizi ni za Watanzania, lakini mradi ule haukufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hawa Softech waliongezwa mkataba wa thamani ya shilingi milioni 55 kwa ajili ya kufundisha watumishi wa TPA ambapo mfumo haukufanya kazi. Pamoja na hayo, walilipwa shilngi milioni 55 zote na katika zile shilingi milioni 55 zilitakiwa kulipwa kwenye mkataba wa awali wa shilingi milioni 694. Serikali ikaingia hasara ya shilingi milioni 600 ya kwanza na ikaingia hasara ya shilingi milioni 55 ya pili. Hizi fedha ni za walipa kodi.

Mheshimiwa Spika, bado haitoshi, mwaka 2015/2016 kampuni ya 23rd Century System iliingia mkataba na Serikali ya kutengeneza mfumo pale TPA ambao ungegharimu shilingi bilioni 14, lakini mpaka mwaka 2019 mfumo huu haufanyi kazi, Serikali imelipa shilingi bilioni tisa; hasara kwa Serikali na hizi ni fedha za walipa kodi. Bado haitoshi fedha zililipwa shilingi bilioni tisa, lakini Mkandarasi hakulipa kodi ya zuio (Withholding Tax), akatoroka na fedha za wananchi sawa na shilingi milioni 874. Ni lazima Serikali ichukue tahadhari inapoanzisha mifumo ya ukusanyaji wa mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, bado haikutosha kampuni ya SAP mwaka 2020 ikaajiriwa; kazi yake ni kuangalia kama huyu 23rd Century System Limited alifanya kazi ambayo ilistahili kulipwa zile fedha. Naye akalipwa dola za Kimarekani 433,000 sawa na shilingi milioni 874. Hizi ni fedha za walipa kodi na bado mifumo haikufanya kazi. Tunavyozungumza sasa hivi, ule mfumo haukufanya kazi tena pale TPA na fedha za walipa kodi zililipwa. Katika mifumo hii ni shilingi bilioni 17 zilitumika na mfumo haukufanya kazi.

Mheshimiwa Spika, siyo TPA peke yake, ukienda pale GPSA wamenunua mfumo wa shilingi bilioni 1,087, sasa wamekuja kugundua ule mfumo hautoi yale mahitaji ambayo walikuwa wanayahitaji. Wamekuja kugundua ule mfumo hautawasaidia tena. Sasa wameshindwa kuutumia ule mfumo na fedha za Serikali zililipwa shilingi bilioni 1,087. Wameandika kibali kwenda Wizara ya Fedha, wabadilishe watumie mfumo mwingine na Wizara ya Fedha imewakubalia na hasara tayari imepatikana katika fedha za walipa kodi. (Makofi)

MHE. HUMPHREY H. POLEPOLE: Mheshimiwa Spika, taarifa.

T A A R I F A

MHE. HUMPHREY H. POLEPOLE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Mzungumzaji anateremsha taarifa muhimu sana, nilitaka kumpa taarifa kwamba TANESCO mwaka jana 2021 mwishoni wameingia mkataba na kampuni ya kutoka India kwa zaidi ya shilingi bilioni 69 kwa ajili ya mifumo ya TEHAMA na watu wengi tunajiuliza kama uwezo huo wa kampuni kutoka India haupo nchini Tanzania licha ya kwamba mifumo mingine ya Kiserikali inatengenezwa hapa Tanzania?

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Simon Lusengekile unapokea taarifa hiyo.

MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Spika, ninapokea taarifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa tuone ni namna gani Serikali inaingia hasara katika mifumo ambayo haina tija na haileti matokeo chanya kwa Taifa. Wahasibu wanaita this is nugatory expenditure. The Government incur some expense that cannot generate economic benefit. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninaishauri Serikali kuchukua hatua za haraka kwa wale wote ambao wamesababisha hasara kwa Taifa. Watumishi ambao wapo ofisini wamesababisha hasara kwa Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, namshukuru sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan, tayari ameshaanza kuchukua hatua na kumwelekeza DG wa Bandari kuhakikisha kwamba wafanyakazi waliopo pale waliosababisha hasara hii wanachukuliwa hatua za haraka.

Mheshimiwa Spika, ninaishauri Serikali ichukue hatua kwa makampuni haya ambayo yalilipwa fedha nyingi na Serikali shilingi bilioni 17 na mfumo haukuleta tija ikiwepo na hii 23rd Century System Limited iweze kulipa fedha za TRA ambayo ilikuwa ni Withholding Tax, shilingi milioni 877. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo naomba pia nichangie kidogo kuhusu kiwanda cha sukari pale Mbigiri. Serikali iliingia mkataba wa kusimika kiwanda cha sukari cha kisasa pale Mbigiri, lakini mpaka sasa tunapozungumza, kiwanda kile hakijawahi kusimikwa na Serikali imepata hasara ya fedha kwa sababu walilima miwa wakijua kwamba kiwanda kitawahi kuja, miwa ile imeharibika, tayari Serikali imepata hasara ya zaidi ya shilingi milioni 300. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, haitoshi…

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

T A A R I F A

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, nampa taarifa jirani yangu wa Busega kwa mchango wake mzuri. Siyo Serikali tu, Mifuko ya Hifadhi ya Jamii imelazimishwa kuwekezwa hapo, PSSSF miaka mitatu imetengeneza hasara ya shilingi bilioni 11; na ukiuliza sababu, Serikali haijapeleka mashine.

Mheshimiwa Spika, ahsante. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Simon Lusengekile, unapokea taarifa hiyo?

MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Spika, pale Mbigiri NSSF ina 96% na Magereza wana 4%, tunazidi kudidimiza taasisi zetu. Waliingia mkataba wa kununua miwa ya outgrowers; wakulima wa mazingira ya pale. Wakulima wamekopa fedha benki kwa ajili ya kuwekeza kwenye kilimo cha miwa wakijua kwamba baada ya kiwanda kuja watauza ile miwa. Kiwanda hakijasimikwa mpaka sasa hivi, wananchi wanateseka, wanashindwa kulipa mikopo kwa sababu kiwanda hakijapatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba Wizara husika sasa iharakishe kusimika kiwanda hiki ili kiweze kuleta tija kwa Watanzania. Ninaamini kitaleta ajira nyingi kwa Watanzania.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema haya, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Spika, nami nashukuru kwa kunipa nafasi leo nichangie hotuba ya Waziri wa TAMISEMI. Kwanza nianze kumpongeza sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama yetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa sana anayoifanya katika Taifa letu. Amenikumbusha maneno ya Biblia, ukisoma Ezra 10 mstari wa 4 inasema: “inuka sasa maana kazi hii inakuhusu wewe; na sisi tu pamoja nawe; na uwe na moyo mkuu, ukaitende.”

Mheshimiwa Spika, haya maneno yananikumbusha kazi kubwa anayoifanya Mheshimiwa Rais kwa sababu ameamua kuamka; ameinuka na kazi hii inamhusu yeye na ameenda kuitenda, nasi tuko pamoja naye kuhakikisha kwamba kazi inafanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nawapongeza sana Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI kaka yangu Mheshimiwa Innocent na wasaidizi wake wawili; Mheshimiwa Dugange pamoja na Mheshimiwa David, wanafanya kazi kubwa sana kwenye wizara hii ya TAMISEMI. Tunawapongeza kwa sababu tunaona matunda makubwa ya kazi ambayo mnafanya kwenye Majimbo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nampongeza sana Katibu Mkuu wa TAMISEMI, Profesa Shemdoe. Kwa kweli Profesa ni msikivu sana; tunapoenda sisi Wabunge na kazi zetu pale kwake anatusikiliza na hata ukimpigia simu anapokea wakati wowote, hata akiwa hana nafasi, anasema atapiga baadaye na kweli anafanya hivyo. Nampongeza sana, sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kipekee nampongeza sana Mkurugenzi Mkuu wa TARURA, kaka yangu Seif. Kwa kweli kaka huyu ni wa mfano sana kwetu; ni mtu anayesikiliza, ni mtu ambaye ukipeleka shida yako anatatua. Anawasiliana na watu wa wilaya kuhakikisha kwamba maeneo yetu yanakuwa salama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nami sasa nichangie kidogo kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri, nianze na posho ya Madiwani. Nimezungumza na dada yangu hapa, nami naomba niseme kwamba Madiwani wanafanya kazi kubwa sana kwenye Majimbo yetu na kwenye Wilaya zetu. Ni watu ambao wanasimamia miradi yote ambayo inapelekwa na Serikali. Utamwona asubuhi Mheshimiwa Diwani anajikokota na baiskeli yake, anaenda kuangalia mradi umefikia wapi? Leo sisi kama Wabunge ni lazima tutafakari kwa maslahi mapana sana ya hao Waheshimiwa Madiwani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimekuja na hesabu ndogo hapa. Tuna Madiwani 5,287; ukiwapa tu posho yao hata shilingi 800,000/= kwa mwezi, tutakuwa tunawalipa kwa mwezi shilingi bilioni 4,200. Tuki-calculate hii kwa mwaka, tutawalipa shilingi bilioni 50.7. Ninaamini kwa Serikali yetu inawezekana kuwalipa kiasi hiki Madiwani ili waweze kufanya kazi nzuri kwa ajili ya Watanzania, kwani Madiwani wanafanya kazi kubwa sana.

Mheshimiwa Spika, hata huko Mbeya najua wanakulindia Jimbo na wanafanya kazi kubwa kuhakikisha kwamba wewe unapokuwa hapa wao wanafanya kazi kwa ajili ya kuhakikisha kwamba eneo linabaki kuwa salama. Kwa hiyo, niseme, sasa ni wakati muafaka wa Wizara kulichukua hili na kwenda kulifanyia kazi ili Madiwani wetu posho yao iimarike, nao hata wakienda Halmashauri kusimamia miradi, wawe na kitu ambacho wanaweza kujivunia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Madiwani wengi wanatumia baiskeli, kuna haya hapa mwanzoni wanapokuwa wameshinda watafutiwe hata mkopo wa bila riba, walau wapate pikipiki. Madiwani wanapoenda kusimamia miradi, wawe na usafiri ambao sasa ni chanya kwao kutembelea vijiji na Kata zao ili waweze kusimamia miradi ya maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo lingine naomba nizungumzie kidogo sehemu ya afya. Nimesoma Bajeti ya TAMISEMI, naishukuru sana Serikali kwa kutuletea vituo vya afya. Tuna kituo cha afya pale Busega tunajenga, Ngasamo, lakini kwa bajeti hii Waziri kwa kweli hajaweka kituo cha afya hata kimoja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niseme kwamba Naibu Waziri wa TAMISEMI, kaka yangu, Mheshimiwa Dugange amekuwa Mganga Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, anaifahamu Kata ya Kabita. Hii ni Kata ya kimkakati yenye wapiga kura wengi sana. Ni Kata ya pili kwa wingi wa wapiga kura katika Jimbo la Busega. Ni muda muafaka sasa Serikali ione Kata hii ya mkakati kuipelekea kituo cha afya. Najua hatuwezi kujenga kila Kata lakini walau Kata za kimkakati tuweze kupata kituo cha afya. Nami ukiniuliza leo, nitakwambia kwa Jimbo la Busega kipaumbele kianze pale Kabita. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, cha pili, kwenye Jimbo langu la Busega tuna maboma mengi ya zahanati wananchi wamejenga. Tuna zaidi ya maboma 15, lakini kwenye bajeti hii nimeona ukamilishaji wa maboma ya zahanati katika Jimbo la Busega imepangiwa zahanati moja ambayo itakamilishwa. Sasa kuna haja ya kuhakikisha kwamba tunaongeza walau tufanye kama ilivyokuwa mwaka wa fedha huu unaoisha tupate zahanati tatu ili tuweze kuzipunguza zile zahanati ambazo wananchi wameanzisha. Wananchi wanatumia gharama kubwa, wanajitoa kwa mioyo, muda mwingine hawapati chakula, wanahakikisha kwamba wanatoa michango kwa ajili ya kujenga zahanati. Sisi kama Serikali, kama wadau ambao wananchi wametuchagua, sasa tuweze kuwapangia fedha ili aweze kukamilisha zahanati zao. (Makofi)

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Simon Songe kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Jacqueline Ngonyani.

T A A R I F A

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, anachokisema Mheshimiwa Mbunge wa Busega ni sahihi kabisa kwamba wananchi wamejenga majengo ya zahanati, vituo vya afya na madarasa ambayo wametumia nguvu zao na hata sasa yanashindwa kumaliziwa, nguvu za wananchi zinapotea bure. Ninavyosema hivyo Kituo cha Afya Msindo, Wilaya ya Namtumbo wananchi wamejenga jengo la upasuaji, mpaka sasa hivi bado hawajapata pesa ya kumalizia na jengo lile lipo kwenye hatari ya kudondoka katika msimu huu. (Makofi)

SPIKA: Ahsante sana. Mheshimiwa Lusengekile, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Spika, naipokea.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ambalo nataka nichangie ni eneo la TARURA. Pamoja na pongezi ambayo nimetoa kwa kaka yangu Seif lakini bado tuna kazi kubwa ni lazima tuongeze bajeti sasa eneo hili la TARURA ili tuweze kutengeneza barabara zetu. Vijijini bado kuna kazi kubwa ya barabara. Mfano, katika Jimbo la Busega tumetengeneza barabara za Kata zetu tatu lakini kwenye makutano ya zile barabara kuna tatizo la daraja pale Mwamigongwa.

Mheshimiwa Spika, sasa ni wakati sahihi kutafuta fedha zaidi ya milioni 500 twende tukatengeneze lile daraja ili tuwe na mawasiliano ya hizi Kata tatu, Kata ya Malili, Kata ya Imalamate na Kata ya Mkula pale kwenye makutano ili kata hizi ziweze kufunguliwa ili tuweze kusafirisha mazao na tuhakikishe kwamba wananachi wanasafirisha mazao yao yakiwa salama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia kuna barabara inayounganisha mikoa miwili, Mkoa wa Mwanza na Mkoa wa Simiyu. Barabara inayoanzia pale Sayaka inapita Nyaruande inapita Badugu inaenda mpaka Dutwa mpaka kule Bariadi. eneo hili pia tulitengee fedha ili tuweze kutengeneza kama ambavyo itakuwa imekusudiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo. naunga mkono hoja. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma Kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022, Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi nami nichangie taarifa hizi za Kamati Tatu, nizipongeze sana Kamati kwa kazi kubwa ambazo zimefanya kutuletea taarifa ambayo inaenda kutufungua macho nini kinafanyika kwenye Kamati hizi Tatu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa masikitiko makubwa sana katika taasisi zetu hizi mbili TANROADS pamoja na TAA katika muingiliano wa mamalaka ya utendaji wa kazi, kuna tatizo kubwa ambalo 2016 Mwezi Agosti ujenzi na upanuzi wa viwanja vya ndege ulihamishwa kutoka TAA kwenda TANROADS.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeona matatizo makubwa viwanja wana-delay kufanya kazi lakini bado haitoshi wanaingiliana katika maamuzi. Nikupe mifano michache, mpaka sasahivi tunavyozungumza Kiwanja cha Ndege cha Shinyanga, Tabora, Sumbawanga hakijajengwa kwa sababu ya muingiliano wa majukumu kati ya TAA pamoja na TANROADS nini kilifanyika hapa? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mfadhili aliyekuwa anatuletea fedha kwa ajili ya ujenzi wa viwanja hivi alifanya due-diligence pamoja na TAA mwaka 2017 lakini baadae alivyotaka kuleta fedha akagundua kwamba tayari Mamlaka ya Ujenzi wa Viwanja Vya Ndege umehama kutoka TAA kwenda TANROADS akakataa kuleta fedha na ujenzi haukuendelea, nini kilifanyika hapa? Wamekaa zaidi ya miezi 30 hamna kilichoendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninamshukuru sana Mheshimiwa Rais ameendelea na mazungumzo, mwaka jana Mwezi Februari, wameleta Dola za Kimarekani Million 12 kwa ajili ya Ujenzi wa Viwanja hivi, kwa masikitiko makubwa kwa sababu ya mwingiliano huu mpaka sasa hivi hakuna kinachoendelea na fedha zipo kwa Serikali yetu, ni masikitiko makubwa sana fedha hizi ni za mkopo walipa kodi watakuja kurudisha mkopo huu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo mpaka sasa hamna kinachoendelea itafika sehemu tutalipa riba ya kutokutumia fedha ambazo zimekopeswa. Mpaka sasa hivi Mkandarasi aliyefanya quotations 2017 ameambiwa afanye implementations ya mradi naye amekataa amesema hawezi kwa sababu vitu vimepanda bei hawezi kufanya sasa hivi naye ameongeza bei. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, watu wako ofisini wamekaa, watu wanajadili ofisini zaidi ya miezi 11 wako ofisini wameshindwa kutoa maamuzi kwa ajili ya ujenzi wa Kiwanja cha Ndege Shinyanga, Tabora na Sumbawanga. Mheshimiwa Rais anafanya kazi kubwa sana katika Nchi yetu, lakini Watendaji wa Wizara wanamuangusha Rais kwa kutofanya maamuzi kwa wakati. Leo tuna Dola za Kimarekani Million 12 TANROADS hazijafanya kazi ni kwa sababu ya mwingiliano wa majukumu haya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo tunaomba sasa kama inawezekana tuamue kwa pamoja Wabunge turudishe Mamlaka ya Ujenzi wa Viwanja Ndege tutoe TANROADS tupeleke TAA ili kazi iweze kufanyika la sivyo tutakuwa tunazungumza viwanja havipanuliwi, hakuna kinachoweza kufanyika lakini mwingiliano huu utaona umetupa hasara ya Million 236 Kiwanja cha Ndege cha Dodoma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka jana walipanua wakaweka taa za solar kwa ajili ya kutua hizi ndege kubwa, lakini leo TAA zile taa ziliwekwa na TANROADS leo TAA wamekataa kwamba zile taa hazifai tena kwa sababu Mji wa Dodoma umepanuka sasa hawatatumia tena taa za solar wanaitaji taa za umeme Million 236 za walipa kodi zimepotea na sasa haiwezekani. Kwa nini? Kwasababu wanakati wanaweka hizi taa za solar hawakuwa na mawasiliano na kati ya TAA na TANROADS na fedha Million 236 za walipa kodi zimepotea kwa sababu ya Watendaji ambao hawana mawasiliano, hawawezi kufanya kazi zao kwa ajili ya kumsadia Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni lazima leo tuwe na maamuzi ili tuweze kuisaidia Serikali, hawa wote ambao wanasababisha hasara kwa Taifa hawa wote ambao wanasababisha hasara kwa nchi yetu wachukuliwe hatua ili iwe mifano kwa watu wengine kwa ajili ya kunusuru Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili ambalo nataka nichangie. Limechangiwa kidogo suala la riba katika miradi yetu. Leo nilikuwa natafakari hivi inawezekanaje Afisa Masuuli yeye anajisikiaje moyo wake anasaini vocha ya kupitisha malipo ya nyongeza ya kutokulipa kwa wakati kwa sababu amechelewa! Unapitisha voucher ya Milioni 100, unapitisha voucher ya Bilioni Moja unaenda kulipa kwa sababu wewe mwenyewe ulichelewa kumlipa Mkandarasi, haiwezekani leo Wabunge tuamue! Ni kwanini kila siku tunapiga kelele kwa sababu ya ucheleweshaji wa malipo? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ikiwezekana Bunge hili liamue sasa Wizara ya Fedha ituletee taarifa ya kutupatia sababu kwa nini wanachelewa kulipa Malipo kwa Wakandarasi na kuleta riba. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano Daraja la Busisi wamechelewa siku 30 wamelipa riba ya milioni 58. TAA Bilioni 11 lakini Kiwanja cha Ndege cha Mwanza bilioni mbili. Sasa inawezekanaje Afisa Masuuli unasaini Vocha ya kulipa kwa sababu wewe mwenyewe ulichelewa na wewe uko ofisini haiwezekani! Ni lazima tutafakari tuisaidie nchi, ni lazima tutafakari tumsaidie Mheshimiwa Rais, Mheshimiwa Rais anafanya kazi kubwa, hawa Watendaji hawamsaidii. Leo Bunge tuamue ili tumsaidie Mheshimiwa Rais na wananchi wanamfurahia lakini kuna watu wanamuangusha. (Makofi)

Mheshimiwa Naiba Spika, nizungumze kidogo kwa ajili ya mifuko hii ya wakopeshaji ya wajasiliamali wadogo wadogo. Tumeletewa taarifa kwenye Kamati tuna Mifuko 52 na ilikaguliwa Mifuko 13, lakini nimekuja kugundua katika mikopo waliyotoa bilioni 90 kati ya hiyo bilioni 90, bilioni 50 ni mikopo chechefu haiwezi kukusanyika, inawezekanaje?

Haiwezekani watu wanakopeshwa na mwisho wa siku hawarejeshi! Tumegundua kwa sababu, gani? Ni kwa sababu, wanakopeshwa watu ambao hawana sifa, inafika sehemu wanashindwa kurejesha mikopo ile. Sasa haiwezekani! (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini eneo la pili kwenye hii mifuko; wamekopesha zaidi ya asilimia 72 kwa benki za biashara, jambo ambalo si lengo la mifuko hii. Lengo kubwa la mifuko hii ni kukopesha wajasiriamali wadogowadogo, lakini tumekuja kugundua zaidi ya asilimia 70 zinakopeshwa benki ambayo si lengo la mifuko hii, tunayo ya nini? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mifuko hii imetengenezwa ili iawasaidie wajasiriamali wadogowadogo kule vijijini, lakini hawapati mikopo kwa sababu wanaokopeshwa si wale wanufaika; na ndiyo maana sasa tunakuwa na mikopo chechefu kwa sababu watu wameacha malengo na makusudi ya ile mikopo wameenda kwenye malengo ambayo hawakupanga kuyafanya. Ukiona hivi maana yake hatukujiandaa katika hili eneo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia tunayo mifuko mingi, 52, wote wanafanya kazi moja; na kwa sababu hawawasiliani, hamna sehemu wanaonana; leo Mheshimiwa Songe anakopa mfuko A, kesho akifulia kidogo anaenda kukopa B, keshokutwa akifulia kidogo anaenda kukopa C, mwisho wa siku anashindwa kurejesha.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tunaishauri Serikali, ifike mahali mifuko hii sasa iunganishwe iwe michache, badala ya 52 iwe hata minne ili iweze kuwasaidia wananchi wetu. Hata ikiwa inawezekana basi iweze kusomana ili kama umekopa sehemu A basi usipewe mkopo sehemu B, kwa sababu, hatimaye utashindwa kurejesha mikopo hii, ili iweze kuwasaidia wananchi wengine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo hili linatakiwa lichukuliwe hatua za haraka ili tuinusuru nchi yetu…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi nami nichangie hii Wizara yetu ya Maji. Kwanza nianze kwa kumshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa namna alivyotuletea fedha kwenye majimbo yetu kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maji iliyopo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kipekee nimshukuru sana kaka yangu Waziri Aweso kwa kazi kubwa anayofanya ana sifa nyingi sana. Na hapa majuzi nimegundua sifa yake nyingine ambayo sikuwa naijua na ambayo inanifanya niendelee kumfagilia zaidi, nimekuja kugundua kumbe pia ni mshabiki wa simba. Kwa hiyo, ninazidi kukupongeza sana kwa kazi kubwa unayofanya na ni kweli tumeendelea kuona unavyoishi na misemo yako. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kipekee pia, nimshukuru sana msaidizi wako, Dada yangu Mheshimiwa Injinia Maryprisca, Naibu Waziri wa Maji, anaupiga mwingi sana. Dada huyu sijui kama analala, lakini kwa kweli kazi kubwa anafanya. Nimemuona kwenye jimbo langu amefika tumetembea naye vijiji zaidi ya vinne, hakuchoka, hakula, ameenda kula jioni kule Bariadi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba nimpongeze sana na nikuhakikishie kwamba, ulipofika pale Mkula ulisema ule mradi utafunguliwa hivi karibuni na kulikuwa na tatizo la pump, nikuhakikishie kwamba, pump imeshapatikana na wiki hii tulikuwa tunafanya water test na nina imani kwamba, mpaka mwisho wa mwezi mradi huu sasa wananchi wataanza kutumia maji pale kwa hiyo, nikushukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kipekee pia, nimshukuru Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji, kaka yangu Injinia Sanga. Anafanya kazi kubwa, anatusikiliza Wabunge, anatupa ahadi nzuri na ana ahadi pia amenipa nyingine, ninaomba aweze kufanya utekelezaji wake ndani ya mwaka husika wa fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nimshukuru sana DG wa RUWASA kaka yangu Clement. DG anafanya kazi kubwa sana, upatikanaji wa maji vijijini; 2020 Jimbo la Busega upatikanaji wa maji ulikuwa asilimia 39, tunavyosema leo upatikanaji wa maji ni asilimia 64. Hizi ni jitihada kubwa sana za Mheshimiwa Waziri, jitihada kubwa sana za mkurugenzi wa RUWASA kwa kazi kubwa anayofanya kwenye majimbo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia nimshukuru dada yangu Mariam, Meneja wa RUWASA Mkoa wa Simiyu. Dada huyu anafanya kazi kubwa, anatuheshimisha sisi Wabunge na sisi tunasema tutampa ushirikiano kwa sababu yeye anatupa ushirikiano sana. Na niombe tu kama si namna ya kupanda basi msimuhamishe maana anafanya kazi kubwa, ila kama ni kupanda basi ruksa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia nimpongeze kijana mwenzangu, Engineer Ngangari ambaye ni Meneja wa RUWASA Wilaya ya Busega. Ni kijana msikivu, anasikiliza, ananishauri na mimi ninamshauri mwisho wa siku tunatengeneza kitu ambacho ni kimoja kwa ajili yaw ana- Busega.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiri, ni Mjumbe wa PAC. Tumeenda kutembelea miradi mbalimbali inayotekelezwa na mamlaka, wapo mameneja na wakurugenzi wa mamlaka husika wanafanya kazi kubwa kuhakikisha kwamba, wanasimamia miradi ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano; tulienda Dar-es- Salaam tukakutana na DG wa DAWASA, aisee, brother big up sana, DG wa DAWASA anafanya kazi kubwa na zaidi ya yote amesimamia hata mapato ya ndani kuhakikisha kwamba, anayapeleka kwenye miradi. Hiyo ni sehemu mojawapo ya kuiga kwa wakurugenzi wengine wa mamlaka, ili wanapopata fedha za ndani wapeleke kwenye miradi, lakini pia tumeenda kule AUWASA kule Arusha na kwenyewe wanafanya kazi kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeenda hapa Babati kwa kijana mdogo sana, Msuya, anafanya kazi kubwa sana kule Babati kwa ajili ya upatikanaji wa maji. Lakini Mkurugenzi wa MWAUWASA kule Mwanza anafanya kazi kubwa kwa ajili ya Watanzania wanaoishi pale Mwanza. Na sisi pia kwa mapato ya Wizara alitupatia mradi kule Busega kwa ajili ya kazi kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe mambo machache. Busega ndio kuna chanzo cha Ziwa Viktoria, lakini kuna vijiji ambavyo viko ndani ya kilometa 42 havina maji. Leo nikuombe, majuzi hapa ulijibu mradi wa maji wa Ziwa Viktoria kwenda Bariadi kutokea Busega, Maswa, Itilima na Meatu utaanza hivi karibuni. Niombe sana mradi huu ndio muarobaini wa matatizo ya maji katika Mkoa wa Simiyu, ndio muarobaini wa matatizo ya maji katika Jimbo la Busega. Nikuombe sana kama tayari umeshatangaza atakapopatikana mkandarasi basi aende kwa speed ili wananchi sasa walio wengi katika Mkoa wa Simiyu, hasa Wilaya ya Busega, waweze kupata maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia Mheshimiwa Waziri hivi karibuni mlitangaza mradi mkubwa wa maji pale Jimbo la Busega. Mradi wa thamani ya bilioni sita kwenye kata yetu ya Kabita, lakini mkandarasi hakupatikana, alikosa vigezo. Ninajua mnatangaza tena, niombe sasa speed iongezeke ili mkandarasi apatikane aweze kufanya kazi kwa ajili ya kuanza ule mradi. Nimeona kwenye bajeti tayari umetutengea, bajeti iliyopita milioni 950 na bajeti hii milioni 700. Ni imani yangu kwamba, ataanza kazi mapema ili wananchi waweze kupata maji safi na salama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pale Busega tuna kata kama tatu bado zina shida ya maji. Tuna Kata ya Nyaruhande, tuna Kata ya Igalukilo na Kata ya Ngasamo bado zina shida ya maji. Niombe sasa kata hizi tuziangalie kwa macho mawili ili tuweze kuzipatia maji na wananchi wa pale nao waweze kunufaika na Ziwa Viktoria. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo niunge mkono hoja. (Makofi)