United Republic of Tanzania
Parliament of Tanzania
Spika wa Bunge Mheshimiwa Job Ndugai amekutana na kufanya mazungumzo na wabunge wa Afrika Mashariki kutoka Tanzania ofisini kwake jijini Dar es Salaam.
Katika mazungumzo hayo wabunge hao wamempongeza Mhe. Ndugai kwa kuchaguliwa kuwa spika wa Bunge la 11 na kuahidi kushurikiana nae katika utendaji kazi kwa maendeleo ya Tanzania.
Wabunge hao ambao huchaguliwa na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, pamoja na mambo mengine wamemweleza Spika wa Bunge jinsi uwakilishi wao katika Bunge la Afrika Mashariki hutegemea sana mahusiano ya Karibu na Mabunge wanachama wa Afrika Mashariki.
Katika kikao hicho, wameliomba Bunge la Tanzania kushirikiana na Serikali ili kuweka msukumo mkubwa kwa lengo la kukifanya kiswahili kuwa moja wapo ya Lugha rasmi katika uendeshaji wa Bunge la Afrika mashariki ikiwa ni moja ya njia ya kukuza lugha hiyo.
Kwa upande wake Spika wa Bunge Mhe. Ndugai amewashukuru Wabunge hao kwa kumtembelea na kuahidi kuyafanyia kazi mapendekezo hayo ikiwa ni pamoja na kuweka utaratibu ndani ya Kanuni za Bunge juu ya namna Taarifa na utekelezaji wa majukumu ya Wabunge hao utakavyofanyiwa kazi na Bunge la Tanzania.