United Republic of Tanzania
Parliament of Tanzania

KAMATI ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) imesikitishwa na kitendo
cha kutelekezwa kwa miradi ya Nyumba nane za watumishi wa Wilaya za
Mvomero na Wilaya ya Gairo.
Kamati hiyo ilisikitishwa na hatua
iliyofikiwa ya ujenzi wa miradi hiyo jana wakati ilipotembelea kujionea
ujenzi wa Nyumba hizo ikiwemo nyumba za wakuu wa Wilaya hizo.
Akizungumza
katika ziara hiyo, Mwenyekiti aliyeongoza ujumbe wa Kamati hiyo, Shally
Raymond alisema hawajaridhishwa na hatua ambayo ujenzi wa Nyumba hiyo
ulipofikia.
"Kwa sasa nyumba hizi ni kama vile zimetelekezwa licha ya fedha nyingi za Serikali kutumika katika miradi hii," alisema.
Aidha,
Kamati ilimuagiza Kaimu Meneja wa Mkoa wa Wakala wa Majengo (TBA),
Edward Ngowi kuhakikisha inaipatia Kamati hiyo mapema iwezekanavyo
mchanganuo wa fedha zilizotumika hadi sasa kwa kila nyumba badala ya
kuleta gharama za jumla.
Alisema Kamati inataka mchanganuo huo
ili kujua thamani ya fedha iliyotumika na kulinganisha na uhalisia wa
miradi katika hatua iliyofikiwa.
Awali akitoa maelezo kuhusiana na miradi huo, Ngowi alisema hadi sasa mradi huo umeshatumia Sh. Milioni 184.4 .
Alizitaja
changamoto zilizosababisha kukwama kwa utekelezaji wa miradi hiyo
kwamba ni pamoja na ukosefu wa fedha kutoka Serikalini na kwamba zana ya
ujenzi kwa gharama nafuu kuharibika kutokana na kutopatikana kwa fedha
kwa wakati.
"Mradi umekosa fedha kwa muda mrefu na kuendelea
kusababisha uharibifu kwa hatua iliyofikiwa na pia kuendelea kuongezeka
kwa gharama za ujenzi," alisema.
Kwa mujibu wa Ngowi ujenzi huo
ulianza katika Mwaka wa Fedha 2013/14 na ulitakiwa ukamilike ndani ya
wiki 32 na kwamba hatua iliyofikiwa hadi sasa ni asilimia 30 huku fedha
iliyotolewa ni asilimia 15